Part 26

 

46 - AL - AH'QAAF

KWA JINA LA MWENYEZI MUNGU MWINGI WA REHEMA MWENYE KUREHEMU. 

 

1. H'A MIM 

2. Uteremsho wa Kitabu umetoka kwa Mwenyezi Mungu, Mwenye nguvu, Mwenye hikima. 

3. Hatukuziumba mbingu na ardhi wala yaliyomo baina yake ila kwa haki na kwa muda maalumu. Na walio kufuru wanayapuuza yale wanayo onywa. 

4. Je! Mwawaona wale mnao waomba badala ya Mwenyezi Mungu? Nionyesheni wameumba nini katika ardhi; au hao wanayo shirika katika mbingu? Nileteeni Kitabu kilicho kuwa kabla ya hiki, au alama yoyote ya ilimu, ikiwa mnasema kweli. 

5. Na nani mpotofu mkubwa kuliko hao wanao waomba, badala ya Mwenyezi Mungu, ambao hawatawaitikia mpaka Siku ya Kiyama, na wala hawatambui maombi yao. 

6. Na ambao watu watakapo kusanywa watakuwa maadui zao, na wataikataa ibada yao. 

7. Na wanapo somewa Aya zetu zilizo wazi, walio kufuru husema juu ya haki inapo wajia: Huu ni uchawi dhaahiri. 

8. Au wanasema: Ameizua mwenyewe! Sema: Ikiwa nimeizua mimi, basi nyinyi hamwezi kunifaa chochote mbele ya Mwenyezi Mungu. Yeye anajua zaidi hayo mnayo ropokwa; anatosha kuwa shahidi baina yangu na nyinyi. Na Yeye ndiye Mwenye kusamehe, Mwenye kurehemu. 

9. Sema: Mimi si kiroja miongoni mwa Mitume. Wala sijui nitakavyo fanywa wala nyinyi. Mimi nafuata niliyo funuliwa tu kwa Wahyi, wala mimi si chochote ila ni mwonyaji mwenye kudhihirisha wazi. 

10. Sema: Mwaonaje yakiwa haya ni kweli yametoka kwa Mwenyezi Mungu, nanyi mmeyakataa, na akashuhudia shahidi miongoni mwa Wana wa Israili juu ya mfano wa haya, na akaamini, na nyinyi mnafanya kiburi? Hakika Mwenyezi Mungu hawaongoi watu wenye kudhulumu. 

11. Na walio kufuru waliwaambia walio amini: Lau kuwa hii ni kheri, wasingeli tutangulia. Na walipo kosa kuongoka wakasema: Huu ni uzushi wa zamani. 

12. Na kabla yake kilikuwapo Kitabu cha Musa, kuwa chenye uwongozi na rehema. Na hichi ni Kitabu cha kusadikisha na kilicho kuja kwa lugha ya Kiarabu, ili kiwaonye walio dhulumu, na kiwe ni bishara kwa watendao mema. 

13. Hakika walio sema: Mola wetu Mlezi ni Mwenyezi Mungu; kisha wakatengenea, hawatakuwa na khofu, wala hawatahuzunika. 

14. Hao ndio watu wa Peponi, watadumu humo, kuwa ni malipo kwa waliyo kuwa wakiyatenda. 

15. Na tumemuusia mwanaadamu awatendee wema wazazi wake wawili. Mama yake amechukua mimba yake kwa taabu, na akamzaa kwa taabu. Na kuchukua mimba kwake hata kumwachisha ziwa ni miezi thalathini. Hata anapo fika utu uzima wake, na akafikilia miaka arubaini, husema: Mola wangu Mlezi! Niwezeshe nishukuru neema zako ulizo nineemesha mimi na wazazi wangu, na nitende mema unayo yapenda. Na unitengenezee dhuriya zangu. Hakika mimi nimetubu kwako, na mimi ni miongoni mwa Waislamu. 

16. Hao ndio tunao wapokelea bora ya vitendo vyao walivyo vitenda, na tunayasamehe makosa yao. Watakuwa miongoni mwa watu wa Peponi. Miadi ya kweli hiyo walio ahidiwa. 

17. Na ambaye amewafyonya wazazi wake na akawaambia: Ati ndio mnanitisha kuwa nitafufuliwa, na hali vizazi vingi vimekwisha pita kabla yangu! Na hao wazazi humwomba msaada Mwenyezi Mungu (na humwambia mtoto wao): Ole wako! Amini! Hakika ahadi ya Mwenyezi Mungu ni kweli. Na yeye husema: Hayakuwa haya ila ni visa vya watu wa kale. 

18. Hao ndio ambao imehakikikishwa hukumu juu yao kama mataifa yaliyo kwisha pita kabla yao miongoni mwa majini na watu. Hakika hao wamekuwa wenye kukhasiri. 

19. Na wote watakuwa na daraja zao mbali mbali kwa waliyo yatenda, na ili awalipe kwa vitendo vyao, na wala hawatadhulumiwa. 

20. Na siku watakapo letwa walio kufuru kwenye Moto wataambiwa: Nyinyi mlitwaa vitu vyenu vizuri katika uhai wa duniani, na mkastareheshwa navyo. Basi leo ndio mnalipwa adhabu ya fedheha kwa mlivyo kuwa mkitakabari katika ardhi bila ya haki, na kwa sababu mlikuwa mkifanya upotovu. 

21. Na mtaje ndugu wa kina A'di, alipo waonya watu wake kwenye vilima vya mchanga. Na kwa yakini waonyaji wengi walitokea kabla yake na baada yake kuwaambia: Msimuabudu isipo kuwa Mwenyezi Mungu. Hakika mimi nakukhofieni isikupateni adhabu ya siku iliyo kuu. 

22. Wakasema: Je! Umetujia ili ututenge mbali na miungu yetu? Basi tuletee hayo unayo tuahidi ikiwa wewe ni miongoni mwa wasemao kweli. 

23. Akasema: Hakika ujuzi uko kwa Mwenyezi Mungu. Mimi nakufikishieni niliyo tumwa. Lakini nakuoneni kuwa nyinyi mnafanya ujinga. * 

24. Basi walipo liona wingu likielekea kwenye mabonde yao, walisema: Wingu hili la kutunyeshea mvua! Kumbe sivyo, haya ni hayo mliyo yahimiza, upepo ambao ndani yake imo adhabu chungu! 

25. Unaangamiza kila kitu kwa amri ya Mola wake Mlezi. Wakawa hawaonekani ila nyumba zao tu. Hivyo ndivyo tuwalipavyo wakosefu! 

26. Na bila ya shaka tuliwaweka vizuri sio kama tulivyo kuwekeni nyinyi; na tuliwapa masikio, na macho, na nyoyo. Na hayakuwafaa kitu masikio yao, wala macho yao, wala nyoyo zao kwa lolote. Kwani hao walikuwa wakizikataa Ishara za Mwenyezi Mungu, na yale waliyo kuwa wakiyafanyia maskhara ndiyo yakawazunguka. 

27. Na hakika tuliiangamiza miji ilio jirani zenu, na tulizitumia Ishara ili wapate kurejea. 

28. Basi mbona wale walio washika badala ya Mwenyezi Mungu, kuwa ati hao ndio wawakurubishe, hawakuwanusuru? Bali waliwapotea! Na huo ndio uwongo walio kuwa wakiuzua. 

29. Na wakati tulipo waleta kundi la majini kuja kwako kusikiliza Qur'ani. Basi walipo ihudhuria walisema: Sikilizeni! Na ilipo kwisha somwa, walirudi kwa kaumu yao kwenda kuwaonya. 

30. Wakasema: Enyi kaumu yetu! Sisi tumesikia Kitabu kilicho teremshwa baada ya Musa, kinacho sadikisha yaliyo kuwa kabla yake, na kinacho ongoza kwenye Haki na kwenye Njia Iliyo Nyooka. 

31. Enyi kaumu yetu! Muitikieni Mwenye kuitia kwa Mwenyezi Mungu, na muaminini, Mwenyezi Mungu atakusameheni, na atakukingeni na adhabu chungu. 

32. Na wasio mwitikia Mwitaji wa Mwenyezi Mungu basi hao hawatashinda katika ardhi, wala hawatakuwa na walinzi mbele yake. Hao wamo katika upotovu ulio dhaahiri. 

33. Je! Hawaoni ya kwamba Mwenyezi Mungu, aliye ziumba mbingu na ardhi, na hakuchoka kwa kuziumba, kuwa ni Muweza wa kuwafufua wafu? Kwani? Hakika Yeye ni Muweza wa kila kitu. 

34. Na siku watakapo letwa makafiri Motoni wakaambiwa: Je! Haya si kweli? Watasema: Kwani? Tunaapa kwa Mola wetu Mlezi, ni kweli! Atasema: Basi onjeni adhabu kwa sababu ya kule kukataa kwenu. 

35. Basi subiri, kama walivyo subiri Mitume wenye stahmala kubwa, wala usiwafanyie haraka. Siku watakayo yaona waliyo ahidiwa itakuwa kama kwamba hawakukaa ulimwenguni ila saa moja ya mchana. Huu ndio ufikisho! Kwani huangamizwa wengine isipo kuwa walio waovu tu ?

 

47 - MUH'AMMAD

KWA JINA LA MWENYEZI MUNGU MWINGI WA REHEMA MWENYE KUREHEMU. 

 

1. Walio kufuru na wakazuilia njia ya Mwenyezi Mungu, Yeye atavipotoa vitendo vyao. 

2. Na walio amini, na wakatenda mema, na wakaamini aliyo teremshiwa Muhammad - nayo ni Haki iliyo toka kwa Mola wao Mlezi - atawafutia makosa yao na ataitengeneza hali yao. 

3. Hayo ni kwa sababu walio kufuru wamefuata upotovu, na walio amini wamefuata Haki iliyo toka kwa Mola wao Mlezi. Hivyo ndivyo Mwenyezi Mungu anavyo wapigia watu mifano yao. 

4. Basi mnapo wakuta walio kufuru wapigeni shingoni mwao, mpaka mkiwadhoofisha wafungeni pingu. Tena waachilieni kwa hisani au wajikomboe, mpaka vita vipoe. Ndio hivyo. Na lau angeli taka Mwenyezi Mungu angeli washinda mwenyewe, lakini haya ni kwa sababu akutieni mitihani nyinyi kwa nyinyi. Na walio uliwa katika njia ya Mwenyezi Mungu hatazipoteza a'mali zao. 

5. Atawaongoza na awatengezee hali yao. 

6. Na atawaingiza katika Pepo aliyo wajuulisha. 

7. Enyi mlio amini! Mkimnusuru Mwenyezi Mungu naye atakunusuruni na ataithibitisha miguu yenu. 

8. Na walio kufuru, basi kwao ni maangamizo, na atavipoteza vitendo vyao. 

9. Hayo ni kwa sababu waliyachukia aliyo yateremsha Mwenyezi Mungu, basi akaviangusha vitendo vyao. 

10. Kwani hawakutembea katika ardhi wakaona ulikuwaje mwisho wa walio kuwa kabla yao? Mwenyezi Mungu aliwaangamiza, na kwa makafiri hawa itakuwa mfano wa hayo. 

11. Hayo ni kwa sababu Mwenyezi Mungu ni Mlinzi wa walio amini. Na makafiri hawana mlinzi. 

12. Hakika Mwenyezi Mungu atawaingiza walio amini na wakatenda mema katika Bustani zipitiwazo na mito kati yake. Na walio kufuru hujifurahisha na hula kama walavyo wanyama, na Moto ndio makaazi yao. 

13. Na miji mingapi iliyo kuwa na nguvu zaidi kuliko mji wako huu ulio kutoa; nao tuliwateketeza na wala hawakuwa wa kuwanusuru. 

14. Je! Mwenye kuwa na bayana kutoka kwa Mola wake Mlezi ni kama aliye pambiwa uovu wa vitendo vyake, na wakafuata pumbao lao? 

15. Mfano wa Pepo walio ahidiwa wachamngu ina mito ya maji yasiyo vunda, na mito ya maziwa isiyo haribika ladha yake, na mito ya mvinyo yenye ladha kwa wanywao, na mito ya asali iliyo safishwa. Na wao humo watakuwa na kila namna ya matunda, na maghfira kutoka kwa Mola wao Mlezi. Basi hao ni kama watakao dumu Motoni na wakinyweshwa maji yanayo chemka ya kuwakata matumbo yao? 

16. Na wapo miongoni mwao wanao kusikiliza, mpaka wakiondoka kwako huwauliza walio pewa ilimu: Amesema nini sasa hivi? Hao ndio ambao Mwenyezi Mungu amepiga muhuri juu ya nyoyo zao, na wakafuata pumbao lao. 

17. Na wale walio ongoka anawazidishia uongofu na anawapa uchamngu wao. 

18. Kwani wanangojea jengine isipo kuwa iwafikie Saa (ya Kiyama) kwa ghafla? Na hakika alama zake zimekwisha kuja. Na itapo wajia kutawafaa wapi kukumbuka hapo? 

19. Basi jua ya kwamba hapana mungu ila Mwenyezi Mungu, na omba maghufira kwa dhambi zako na za Waumini wanaume na Waumini wanawake. Na Mwenyezi Mungu anajua mahali penu pa kwenda na kurudi, na mahali penu pa kukaa. 

20. Na Waumini wanasema: Kwa nini haiteremshwi Sura? Na inapo teremshwa Sura madhubuti na ikatajwa ndani yake khabari ya vita, utawaona wenye maradhi katika nyoyo zao wanakutazama mtazamo wa anaye zimia kwa mauti. Basi ni bora kwao 

21. Ut'iifu na kauli njema. Na jambo likisha azimiwa, basi wakiwa ni wakweli kwa Mwenyezi Mungu, bila ya shaka itakuwa ni kheri kwao. 

22. Basi yanayo tarajiwa kwenu mkitawala ndio mfisidi katika nchi na mwatupe jamaa zenu? 

23. Hao ndio Mwenyezi Mungu alio walaani, na akawatia uziwi, na akawapofoa macho yao. 

24. Je! Hawaizingatii hii Qur'ani? Au kwenye nyoyo (zao) zipo kufuli? 

25. Kwa hakika wanao rudi nyuma baada ya kwisha wabainikia uwongofu, Shetani huyo amewashawishi na amewaghuri. 

26. Hayo ni kwa sababu waliwaambia walio chukia aliyo yateremsha Mwenyezi Mungu: Tutakut'iini katika baadhi ya mambo. Na Mwenyezi Mungu anajua siri zao. 

27. Basi itakuwaje Malaika watakapo wafisha wakawa wanawapiga nyuso zao na migongo yao! 

28. Hayo ni kwa sababu wao waliyafuata yaliyo mchukiza Mwenyezi Mungu na wakachukia yanayo mridhisha, basi akaviangusha vitendo vyao. 

29. Je! Wenye maradhi nyoyoni mwao wanadhani kwamba Mwenyezi Mungu hatazidhihirisha chuki zao? 

30. Na tungeli penda tungeli kuonyesha hao na ungeli watambua kwa alama zao; lakini bila ya shaka utawajua kwa namna ya msemo wao. Na Mwenyezi Mungu anavijua vitendo vyenu. 

31. Na bila ya shaka tutakujaribuni mpaka tuwadhihirishe wapignao Jihadi katika nyinyi na wanao subiri. Nasi tutazifanyia mtihani khabari zenu. 

32. Kwa hakika walio kufuru na wakazuilia njia ya Mwenyezi Mungu na wakapinzana na Mtume baada ya kwisha wabainikia uwongofu, hao hawatamdhuru Mwenyezi Mungu kwa lolote. Naye ataviangusha vitendo vyao. 

33. Enyi mlio amini! Mt'iini Mwenyezi Mungu, na mt'iini Mtume, wala msiviharibu vitendo vyenu. 

34. Hakika walio kufuru na wakazuilia njia ya Mwenyezi Mungu, kisha wakafa na hali ni makafiri, Mwenyezi Mungu hatawasamehe makosa yao. 

35. Basi msiregee na kutaka suluhu, maana nyinyi ndio mtakao shinda. Na Mwenyezi Mungu yu pamoja nanyi, wala hatakunyimeni malipo ya vitendo vyenu. 

36. Hakika uhai wa duniani ni mchezo na pumbao. Na mkiamini na mkamchamngu Mwenyezi Mungu atakupeni ujira wenu, wala hakutakeni mali yenu. 

37. Na akikutakeni hayo na kukushikilieni mtafanya ubakhili, na atatoa undani wa chuki zenu. 

38. Angalieni! Nyinyi mnaitwa mtumie katika njia ya Mwenyezi Mungu, na wapo katika nyinyi wanao fanya ubakhili. Na anaye fanya ubakhili basi anajifanyia ubakhili mwenyewe. Na Mwenyezi Mungu si mhitaji, na nyinyi ndio wahitaji. Na mkigeuka atawaleta watu wengine badala yenu, nao hawatakuwa kama nyinyi. 

 

48 - AL FAT-H'I

KWA JINA LA MWENYEZI MUNGU MWINGI WA REHEMA MWENYE KUREHEMU. 

 

1. Hakika tumekufungulia Ushindi wa dhaahiri 

2. Ili Mwenyezi Mungu akusamehe makosa yako yaliyo tangulia na yajayo, na akutimizie neema zake, na akuongoe katika Njia Iliyo Nyooka, 

3. Na Mwenyezi Mungu akunusuru nusura yenye nguvu - 

4. Yeye ndiye aliye teremsha utulivu katika nyoyo za Waumini ili wazidi Imani juu ya Imani yao. Na Mwenyezi Mungu ndiye mwenye majeshi ya mbingu na ardhi. Na Mwenyezi Mungu ni Mwenye ujuzi, Mwenye hikima - 

5. Ili awaingize Waumini wanaume na Waumini wanawake katika Bustani zipitazo mito kati yake, wadumu humo, na awafutie makosa yao. Na huko ndiko kufuzu kukubwa mbele ya Mwenyezi Mungu. 

6. Na awape adhabu wanaafiki wanaume na wanaafiki wanawake, na washirikina wanaume na washirikina wanawake, wanao mdhania Mwenyezi Mungu dhana mbaya. Utawafikia mgeuko mbaya, na Mwenyezi Mungu awakasirikie, na awalaani, na awaandalie Jahannamu. Na hayo ni marudio maovu kabisa. 

7. Na Mwenyezi Mungu ana majeshi ya mbingu na ardhi. Na Mwenyezi Mungu ni Mwenye nguvu, Mwenye hikima. 

8. Hakika tumekutuma wewe uwe Shahidi, na Mbashiri, na Mwonyaji, 

9. Ili mumuamini Mwenyezi Mungu na Mtume wake, na mumsaidie, na mumhishimu, na mumtakase asubuhi na jioni. 

10. Bila ya shaka wanao fungamana nawe, kwa hakika wanafungamana na Mwenyezi Mungu. Mkono wa Mwenyezi Mungu uko juu ya mikono yao. Basi avunjaye ahadi hizi anavunja kwa kuidhuru nafsi yake; na anaye tekeleza aliyo muahadi Mwenyezi Mungu, Mwenyezi Mungu atamlipa ujira mkubwa. 

11. Watakuambia mabedui walio baki nyuma: Yametushughulisha mali yetu na ahali zetu, basi tuombee msamaha. Wanasema kwa ndimi zao yasiyo kuwamo katika nyoyo zao. Sema: Ni nani awezaye kukusaidieni chochote kwa Mwenyezi Mungu akitaka Yeye kukudhuruni au akitaka kukunufaisheni? Bali Mwenyezi Mungu anazo khabari za mnayo yatenda. 

12. Lakini mlidhani kwamba Mtume na Waumini hawatarudi kabisa kwa ahali zao, na mkapambiwa hayo katika nyoyo zenu, na mkadhania dhana mbaya, na mkawa watu wanao angamia. 

13. Na asiye muamini Mwenyezi Mungu na Mtume wake, basi kwa hakika Sisi tumewaandalia makafiri Moto mkali. 

14. Na Mwenyezi Mungu ndiye mwenye ufalme wa mbingu na ardhi. Humsamehe amtakaye, na humuadhibu amtakaye. Na Mwenyezi Mungu ni Mwenye kusamehe, Mwenye kurehemu. 

15. Walio baki nyuma watasema: Mtapo kwenda kuchukua ngawira, tuacheni tukufuateni! Wanataka kuyabadili maneno ya Mwenyezi Mungu. Sema: Hamtatufuata kabisa. Mwenyezi Mungu alikwisha sema kama hivi zamani. Hapo watasema: Bali nyinyi mnatuhusudu. Siyo, bali walikuwa hawafahamu ila kidogo. 

16. Waambie walio achwa nyuma katika mabedui: Mtakuja itwa kwenda pigana na watu wakali kwa vita, mpigane nao au wasalimu amri. Basi mkimt'ii, Mwenyezi Mungu atakupeni ujira mzuri. Na mkigeuka kama mlivyo geuka kwanza, atakuadhibuni kwa adhabu iliyo chungu. 

17. Kipofu hana lawama, wala kiguru hana lawama, wala mgonjwa hana lawama. Na mwenye kumt'ii Mwenyezi Mungu na Mtume wake, atamuingiza katika Mabustani yapitayo mito kati yake. Na atakaye geuka upande atamuadhibu kwa adhabu chungu. 

18. Kwa hakika Mwenyezi Mungu amewapa radhi Waumini walipo fungamana nawe chini ya mti, na alijua yaliyomo nyoyoni mwao. Basi akateremsha utulivu juu yao, na akawalipa kwa Ushindi wa karibu. 

19. Na ngawira nyingi watakazo zichukua. Na Mwenyezi Mungu ni Mwenye nguvu, Mwenye hikima. 

20. Mwenyezi Mungu anakuahidini ngawira nyingi mtakazo zichukua, basi amekutangulizieni hizi kwanza, na akaizuia mikono ya watu isikufikieni, na ili hayo yawe ni Ishara kwa Waumini, na akakuongozeni Njia Iliyo Nyooka. 

21. Na mengine hamwezi kuyapata bado, Mwenyezi Mungu amekwisha yazingia. Na Mwenyezi Mungu ni Muweza wa kila kitu. 

22. Na lau makafiri wangeli pigana nanyi basi bila ya shaka wangeli geuza migongo, kisha wasingeli pata mlinzi wala msaidizi. 

23. Huo ndio mwendo wa Mwenyezi Mungu ulio kwisha pita zamani, wala hutapata mabadiliko katika mwendo wa Mwenyezi Mungu. 

24. Na Yeye ndiye aliyeizuia mikono yao kwenu, na mikono yenu kwao, katika bonde la Makka baada ya kukupeni Ushindi juu yao. Na Mwenyezi Mungu ni Mwenye kuyaona myatendayo. 

25. Hao ndio walio kufuru na wakakuzuieni msiingie Msikiti Mtakatifu, na wakawazuilia dhabihu kufika mahala pao. Na lau si wanaume Waumini na wanawake Waumini msio wajua mkawasaga na mkaingia makosani kutokana nao bila ya kujua ...Mwenyezi Mungu (amefanya haya) ili amuingize amtakaye katika rehema yake. Lau wangeli tengana bila ya shaka tungeli waadhibu walio kufuru kwa adhabu chungu. 

26. Pale walio kufuru walipo tia katika nyoyo zao hasira, hasira za kijinga, Mwenyezi Mungu aliteremsha utulivu juu ya Mtume wake na juu ya Waumini, na akawalazimisha neno la kuchamngu. Na wao walikuwa ndio wenye haki nalo na wenye kustahili. Na Mwenyezi Mungu ni Mjuzi wa kila kitu. 

27. Hakika Mwenyezi Mungu amemtimizia Mtume wake ndoto ya haki. Bila ya shaka nyinyi mtauingia Msikiti Mtakatifu, Inshallah, kwa amani, na hali mmenyoa vichwa vyenu na mmepunguza nywele. Hamtakuwa na khofu. Yeye anajua msiyo yajua. Basi atakupeni kabla ya haya Ushindi karibuni. 

28. Yeye ndiye aliye mtuma Mtume wake kwa uwongofu na Dini ya Haki, ili aitukuze juu ya dini zote. Na Mwenyezi Mungu anatosha kuwa Shahidi. 

29. Muhammad ni Mtume wa Mwenyezi Mungu. Na walio pamoja naye wana nguvu mbele ya makafiri, na wanahurumiana wao kwa wao. Utawaona wakiinama na kusujudu wakitafuta fadhila na radhi za Mwenyezi Mungu. Alama zao zi katika nyuso zao, kwa athari ya kusujudu. Huu ndio mfano wao katika Taurati. Na mfano wao katika Injili ni kama mmea ulio toa chipukizi lake, kisha ukalitia nguvu, ukawa mnene, ukasimama sawa juu ya ubuwa wake, ukawafurahisha wakulima, ili kuwakasirisha kwa ajili yao makafiri. Mwenyezi Mungu amewaahidi walio amini na wakatenda mema katika wao msamaha na ujira mkubwa.

 

49 - AL H'UJURAAT

KWA JINA LA MWENYEZI MUNGU MWINGI WA REHEMA MWENYE KUREHEMU. 

 

1. Enyi mlio amini! Msitangulie mbele ya Mwenyezi Mungu na Mtume wake, na mcheni Mwenyezi Mungu. Hakika Mwenyezi Mungu ni Mwenye kusikia, Mwenye kujua. 

2. Enyi mlio amini! Msinyanyue sauti zenu kuliko sauti ya Nabii, wala msiseme naye kwa kelele kama mnavyo semezana nyinyi kwa nyinyi, visije vitendo vyenu vikaharibika, na hali hamtambui. 

3. Kwa hakika wanao teremsha sauti zao mbele ya Mtume wa Mwenyezi Mungu, hao ndio Mwenyezi Mungu amezisafisha nyoyo zao kwa uchamngu. Hao watakuwa na maghfira na ujira mkubwa. 

4. Hakika hao wanao kuita nawe uko nyuma ya vyumba, wengi wao hawana akili. 

5. Na lau wao wangeli ngojea mpaka uwatokee ingeli kuwa kheri kwao. Na Mwenyezi Mungu ni Mwenye maghfira, Mwenye kurehemu. 

6. Enyi mlio amini! Akikujieni mpotovu na khabari yoyote, ichunguzeni, msije mkawasibu watu kwa kuto jua, na mkawa tena wenye kujuta kwa mliyo yatenda. 

7. Na jueni kuwa Mtume wa Mwenyezi Mungu yuko nanyi. Lau angeli kut'iini katika mambo mengi, bila ya shaka mngeli taabika. Lakini Mwenyezi Mungu amekupendezeeni Imani, na akaipamba katika nyoyo zenu, na amekufanyeni muuchukie ukafiri, na upotovu, na uasi. Hao ndio walio ongoka, 

8. Kwa fadhila za Mwenyezi Mungu na neema zake. Na Mwenyezi Mungu ni Mwenye kujua, Mwenye hikima. 

9. Na ikiwa makundi mawili katika Waumini yanapigana, basi yapatanisheni. Na likiwa moja la hao linamdhulumu mwenzie, basi lipigeni linalo dhulumu mpaka lirejee kwenye amri ya Mwenyezi Mungu. Na likirudi basi yapatanisheni kwa uadilifu. Na hukumuni kwa haki. Hakika Mwenyezi Mungu anawapenda wanao hukumu kwa haki. 

10. Hakika Waumini ni ndugu, basi patanisheni baina ya ndugu zenu, na mcheni Mwenyezi Mungu ili mrehemewe. 

11. Enyi mlio amini! Wanaume wasiwadharau wanaume wenzao, wala wanawake wasiwadharau wanawake wenzao. Huenda hao wakawa bora kuliko wao. Wala msivunjiane hishima, wala msiitane kwa majina ya kejeli. Ni uovu kutumia jina baya baada ya kwisha amini. Na wasio tubu, hao ndio wenye kudhulumu. 

12. Enyi mlio amini! Jiepusheni na dhana nyingi, kwani baadhi ya dhana ni dhambi. Wala msipelelezane, wala msisengenyane nyinyi kwa nyinyi. Je! Yupo katika nyinyi anaye penda kuila nyama ya nduguye aliye kufa? Mnalichukia hilo! Na mcheni Mwenyezi Mungu. Hakika Mwenyezi Mungu ni Mwenye kupokea toba, Mwenye kurehemu. 

13. Enyi watu! Hakika Sisi tumekuumbeni kutokana na mwanamume na mwanamke. Na tumekujaalieni kuwa ni mataifa na makabila ili mjuane. Hakika aliye mtukufu zaidi kati yenu kwa Mwenyezi Mungu ni huyo aliye mchamngu zaidi katika nyinyi. Hakika Mwenyezi Mungu ni Mwenye kujua, Mwenye khabari. 

14. Mabedui wamesema: Tumeamini. Sema: Hamjaamini, lakini semeni: Tumesilimu. Kwani Imani haijaingia katika nyoyo zenu. Na mkimt'ii Mwenyezi Mungu na Mtume wake, hatakupunguzieni chochote katika vitendo vyenu. Hakika Mwenyezi Mungu ni Mwenye kusamehe, Mwenye kurehemu. 

15. Hakika Waumini ni wale walio muamini Mwenyezi Mungu na Mtume wake tena wasitie shaka kabisa, na wakapigana Jihadi katika Njia ya Mwenyezi Mungu kwa mali yao na nafsi zao. Hao ndio wakweli. 

16. Sema: Ati ndio mnamfundisha Mwenyezi Mungu Dini yenu, na hali Mwenyezi Mungu anayajua ya katika mbingu na ardhi, na Mwenyezi Mungu anajua kila kitu? 

17. Wanakusimbulia kuwa wamesilimu! Sema: Msinisimbulie kwa kusilimu kwenu. Bali Mwenyezi Mungu ndiye aliye kufanyieni hisani kwa kukuongoeni kwenye Imani, ikiwa nyinyi ni wakweli. 

18. Hakika Mwenyezi Mungu anajua siri za mbingu na ardhi. Na Mwenyezi Mungu anayaona myatendayo. 

 

50 - QAAF

KWA JINA LA MWENYEZI MUNGU MWINGI WA REHEMA MWENYE KUREHEMU. 

 

1. Qaaf. Naapa kwa Qur'ani tukufu! 

2. Bali wanastaajabu kwamba amewafikia mwonyaji kutoka miongoni mwao, na wakasema makafiri: Hili ni jambo la ajabu! 

3. Ati tukifa na tukawa udongo...? Kurejea huko kuko mbali! 

4. Hakika Sisi tunajua kiasi cha kila kinacho punguzwa na ardhi kutokana nao. Na kwetu kipo Kitabu kinacho hifadhi yote. 

5. Lakini waliikanusha Haki ilipo wajia; kwa hivyo wamo katika mambo ya mkorogo. 

6. Je! Hawaangalii mbingu zilizo juu yao! Vipi tulivyo zijenga, na tukazipamba. Wala hazina nyufa. 

7. Na ardhi tumeitandaza na tukaiwekea milima, na tukaiotesha mimea mizuri ya kila namna. 

8. Yawe haya ni kifumbua macho na ukumbusho kwa kila mja mwenye kuelekea. 

9. Na tumeteremsha kutoka mbinguni maji yaliyo barikiwa, na kwa hayo tukaotesha mabustani na nafaka za kuvunwa. 

10. Na mitende mirefu yenye makole yaliyo zaa kwa wingi, 

11. Ili iwe ni riziki kwa waja wangu. Na tukaifufua kwa maji nchi iliyo kuwa imekufa. Kama hivyo ndivyo utakavyo kuwa ufufuaji. 

12. Kabla yao walikadhibisha kaumu ya Nuhu na wakaazi wa Rassi na Thamudi. 

13. Na A'di na Firauni na kaumu ya Lut'i. 

14. Na wakaazi wa Machakani, na watu wa Tubbaa'. Wote hao waliwakanusha Mitume, kwa hivyo onyo likathibitika juu yao. 

15. Kwani tulichoka kwa kuumba mara ya kwanza. Bali wao wamo katika shaka tu juu ya umbo jipya. 

16. Na hakika tumemuumba mtu, nasi tunayajua yanayo mpitikia katika nafsi yake. Na Sisi tuko karibu naye kuliko mshipa wa shingoni mwake. 

17. Wanapo pokea wapokeaji wawili, wanao kaa kuliani na kushotoni. 

18. Hatamki neno ila karibu yake yupo mwangalizi tayari. 

19. Na uchungu wa kutoka roho utamjia kwa haki. Hayo ndiyo uliyo kuwa ukiyakimbia. 

20. Na litapulizwa baragumu. Hiyo ndiyo Siku ya Miadi. 

21. Na kila nafsi itakuja na pamoja nayo mchungaji na shahidi. 

22. (Aambiwe): Kwa hakika ulikuwa umeghafilika na haya; basi leo tumekuondolea pazia lako, na kwa hivyo kuona kwako leo ni kukali. 

23. Na mwenzake atasema: Huyu niliye naye mimi kesha tayarishwa. 

24. Mtupeni katika Jahannamu kila kafiri mwenye inda, 

25. Akatazaye kheri, arukaye mipaka, mwenye kutia shaka, 

26. Aliye weka mungu mwengine pamoja na Mwenyezi Mungu. Basi mtupeni katika adhabu kali. 

27. Mwenzake aseme: Ee Mola wetu Mlezi! Sikumpoteza mimi, bali yeye mwenyewe alikuwa katika upotovu wa mbali. 

28. (Mwenyezi Mungu) aseme: Msigombane mbele yangu. Nilikuleteeni mbele onyo langu. 

29. Mbele yangu haibadilishwi kauli, wala Mimi siwadhulumu waja wangu. 

30. Siku tutapo iambia Jahannamu: Je! Umejaa? Nayo itasema: Je! Kuna ziada? 

31. Na Pepo italetwa karibu kwa ajili ya wachamngu, haitakuwa mbali. 

32. Haya ndiyo mnayo ahidiwa kwa kila mwenye kurejea kwa Mwenyezi Mungu na akajilinda. 

33. Mwenye kumwogopa Mwingi wa Rehema hali kuwa hamwoni, na akaja kwa moyo ulio elekea- 

34. (Ataambiwa) ingieni kwa salama. Hiyo ndiyo siku ya daima dawamu. 

35. Humo watapata wakitakacho, na kwetu yako ya ziada. 

36. Na kaumu ngapi tuliziangamiza kabla yao walio kuwa na nguvu zaidi kuliko hawa! Nao walitanga tanga katika nchi nyingi. Je! Walipata pa kukimbilia? 

37. Hakika katika hayo upo ukumbusho kwa mwenye moyo au akatega sikio naye yupo anashuhudia. 

38. Na bila ya shaka Sisi tumeziumba mbingu na ardhi na vilio baina yao mnamo siku sita; na wala hayakutugusa machofu. 

39. Basi vumilia kwa hayo wasemayo, na mtakase kwa kumsifu Mola wako Mlezi kabla ya kuchomoza jua na kabla ya kuchwa. 

40. Na katika usiku pia mtakase, na baada ya kusujudu. 

41. Na sikiliza siku atapo nadi mwenye kunadi kutoka pahala karibu. 

42. Siku watakapo sikia ukelele wa haki. Hiyo ndiyo siku ya kufufuka. 

43. Hakika Sisi tunahuisha na tunafisha, na kwetu Sisi ndio marejeo. 

44. Siku itapo wapasukia ardhi mbio mbio! Mkusanyo huo kwetu ni mwepesi. 

45. Sisi tunajua kabisa wayasemayo. Wala wewe si mwenye kuwatawalia kwa ujabari. Basi mkumbushe kwa Qur'ani anaye liogopa onyo. 

 

51 - ADH-DHAARIYAAT

KWA JINA LA MWENYEZI MUNGU MWINGI WA REHEMA MWENYE KUREHEMU. 

 

1. Naapa kwa pepo zinazo tawanya, 

2. Na zinazo beba mizigo, 

3. Na zinazo kwenda kwa wepesi. 

4. Na zinazo gawanya kwa amri, 

5. Hakika mnayo ahidiwa bila ya shaka ni kweli, 

6. Na kwa hakika malipo bila ya shaka yatatokea. 

7. Naapa kwa mbingu zenye njia, 

8. Hakika nyinyi bila ya shaka mmo katika kauli inayo khitalifiana. 

9. Anageuzwa kutokana na haki mwenye kugeuzwa. 

10. Wazushi wameangamizwa. 

11. Ambao wameghafilika katika ujinga. 

12. Wanauliza: Ni lini hiyo siku ya malipo? 

13. Hiyo ni siku watakayo adhibiwa Motoni. 

14. Onjeni adhabu yenu! Haya ndiyo mliyo kuwa mkiyahimiza. 

15. Hakika wachamngu watakuwa katika Mabustani na chemchem. 

16. Wanapokea aliyo wapa Mola wao Mlezi. Kwa hakika hao walikuwa kabla ya haya wakifanya mema. 

17. Walikuwa wakilala kidogo tu usiku. 

18. Na kabla ya alfajiri wakiomba maghfira. 

19. Na katika mali yao ipo haki ya mwenye kuomba na asiye omba. 

20. Na katika ardhi zipo Ishara kwa wenye yakini. 

21. Na pia katika nafsi zenu - Je! Hamwoni? 

22. Na katika mbingu ziko riziki zenu na mliyo ahidiwa. 

23. Basi naapa kwa Mola Mlezi wa mbingu na ardhi, hakika haya ni kweli kama ilivyo kweli kuwa nyinyi mnasema. 

24. Je! Imekufikia hadithi ya wageni wa Ibrahim wanao hishimiwa? 

25. Walipo ingia kwake wakasema: Salama! Na yeye akasema: Salama! Nyinyi ni watu nisio kujueni. 

26. Akenda kwa ahali yake na akaja na ndama aliye nona. 

27. Akawakaribisha, akasema: Mbona hamli? 

28. Akahisi kuwaogopa katika nafsi yake. Wakasema: Usiwe na khofu, nao wakambashiria kupata kijana mwenye ilimu. 

29. Ndipo mkewe akawaelekea, na huku anasema na akijipiga usoni kwa mastaajabu, na kusema: Mimi ni kikongwe na tasa! 

30. Wakasema: Ndivyo vivyo hivyo alivyo sema Mola wako Mlezi. Hakika Yeye ni Mwenye hikima na Mwenye kujua.