Part 23

 

28. Na hatukuwateremshia kaumu yake baada yake jeshi kutoka mbinguni, wala si wenye kuteremsha. 

29. Hakukuwa ila ukelele mmoja tu; na mara walizimwa! 

30. Nawasikitikia waja wangu. Hawajii Mtume ila wao humkejeli. 

31. Je! Hawaoni umma ngapi tulizo ziangamiza kabla yao? Hakika hao hawarejei tena kwao. 

32. Na hapana mmoja ila wote watakusanywa waletwe mbele yetu. 

33. Na Ishara hiyo kwao - ardhi iliyo kufa, nasi tukaifufua, na tukatoa ndani yake nafaka, wakawa wanazila! 

34. Na tukafanya ndani yake mabustani ya mitende na mizabibu, na tukatimbua chemchem ndani yake, 

35. Ili wale matunda yake, na hayo hayakufanywa na mikono yao! Basi je, hawashukuru? 

36. Subhana, Ametakasika, aliye umba dume na jike vyote katika vinavyo mea katika ardhi na katika nafsi zao, na katika wasivyo vijua. 

37. Na usiku ni Ishara kwao. Tunauvua humo mchana, mara wao wanakuwa gizani. 

38. Na jua linakwenda kwa kiwango chake. Hayo ni makadirio ya Mwenye nguvu, Mwenye kujua. 

39. Na mwezi tumeupimia vituo, mpaka unakuwa kama karara kongwe. 

40. Haliwi jua kuufikia mwezi, wala usiku kuupita mchana. Na vyote vinaogelea katika njia zao. 

41. Na ni Ishara kwao kwamba Sisi tuliwapakia dhuriya zao katika jahazi ilio sheheni. 

42. Na tukawaumbia kutoka mfano wake wanavyo vipanda. 

43. Na tukitaka tunawazamisha, wala hapana wa kuwasaidia, wala hawaokolewi, 

44. Isipo kuwa kwa rehema zitokazo kwetu na starehe kwa muda. 

45. Na wanapo ambiwa: Jilindeni na yalioko mbele yenu na yalioko nyuma yenu, ili mpate kurehemewa... 

46. Na haiwafikii Ishara yoyote katika Ishara za Mola wao Mlezi ila wao huwa ni wenye kuipuuza. 

47. Na wanapo ambiwa: Toeni katika aliyo kupeni Mwenyezi Mungu, walio kufuru huwaambia walio amini: Je! Tuwalishe ambao Mwenyezi Mungu angependa angeli walisha mwenyewe? Nyinyi hammo ila katika upotofu ulio dhaahiri. 

48. Na wanasema: Ahadi hii itatokea lini, ikiwa nyinyi ni wakweli? 

49. Hawangojei ila ukelele mmoja tu utakao wachukua nao wamo kuzozana. 

50. Basi hawataweza kuusia, wala kwa watu wao hawarejei. 

51. Na litapulizwa barugumu, mara watatoka makaburini wakikimbilia kwa Mola wao Mlezi. 

52. Watasema: Ole wetu! Nani aliye tufufua kwenye malazi yetu? Haya ndiyo aliyo yaahidi Mwingi wa Rehema na wakasema kweli Mitume. 

53. Haitakuwa ila ukelele mmoja tu, mara wote watahudhuruishwa mbele yetu. 

54. Basi leo nafsi yoyote haitadhulumiwa kitu, wala hamtalipwa ila yale mliyo kuwa mkiyatenda. 

55. Hakika watu wa Peponi leo wamo shughulini, wamefurahi. 

56. Wao na wake zao wamo katika vivuli wameegemea juu ya viti vya fakhari. 

57. Watapata humo kila namna ya matunda na watapata kila watakacho kitaka. 

58. "Salama!" Hiyo ndiyo kauli itokayo kwa Mola Mlezi Mwenye kurehemu. 

59. Na enyi wakosefu! Jitengeni leo! 

60. Je! Sikuagana nanyi, enyi wanaadamu, kuwa msimuabudu Shet'ani? Hakika yeye ni adui dhaahiri kwenu. 

61. Na ya kwamba mniabudu Mimi? Hii ndiyo Njia Iliyo Nyooka. 

62. Na bila ya shaka yeye amekwisha lipoteza kundi kubwa miongoni mwenu. Je, hamkuwa mkifikiri? 

63. Hii basi ndiyo Jahannamu mliyo kuwa mkiahidiwa. 

64. Ingieni leo kwa vile mlivyo kuwa mkikufuru. 

65. Leo tunaviziba vinywa vyao, na iseme nasi mikono yao, na itoe ushahidi miguu yao kwa waliyo kuwa wakiyachuma. 

66. Na tungeli penda tungeli yafutilia mbali macho yao, wakawa wanaiwania njia. Lakini wange ionaje? 

67. Na tungeli taka tunge wageuza sura hapo hapo walipo, basi wasinge weza kwenda wala kurudi. 

68. Na tunaye mzeesha tunamrudisha nyuma katika umbo. Basi je! hawazingatii? 

69. Wala hatukumfundisha (Muhammad) mashairi, wala hayatakikani kwake hayo. Haukuwa huu ila ni ukumbusho na Qur'ani inayo bainisha. 

70. Ili imwonye aliye hai, na neno litimie juu ya makafiri. 

71. Je! Hawaoni kwamba tumewaumbia kutokana na iliyo fanya mikono yetu wanyama wa mifugo, na wao wakawa wenye kuwamiliki. 

72. Na Sisi tukawadhalilishia. Basi baadhi yao wako wanao wapanda, na baadhi yao wanawala. 

73. Na wao wanapata kwao manufaa na vinywaji. Basi je, hawashukuru? 

74. Na wameishika miungu mingine badala ya Mwenyezi Mungu ili ati wapate kusaidiwa! 

75. Hawataweza kuwasaidia. Bali hao ndio watakuwa askari wao watakao hudhurishwa. 

76. Basi maneno yao yasikuhuzunishe. Hakika Sisi tunayajua wanayo yaweka siri na wanayo yatangaza. 

77. Kwani mwanaadamu haoni ya kwamba Sisi tumemuumba yeye kutokana na tone la manii? Kisha sasa yeye ndio amekuwa ndiye mgomvi wa dhaahiri! 

78. Na akatupigia mfano, na akasahau kuumbwa kwake, akasema: Ni nani huyo atakaye ihuisha mifupa nayo imekwisha mung'unyika? 

79. Sema: Ataihuisha huyo huyo aliye iumba hapo mara ya mwanzo. Na Yeye ni Mjuzi wa kila kuumba. 

80. Aliye kujaalieni kupata moto kutokana na mti wa kijani nanyi mkawa kwa huo mnawasha. 

81. Kwani aliye ziumba mbingu na ardhi hawezi kuwaumba mfano wao? Kwani! Naye ndiye Muumbaji Mkuu, Mjuzi. 

82. Hakika amri yake anapo taka kitu ni kukiambia tu: Kuwa! Na kikawa. 

83. Basi Ametakasika yule ambaye mkononi mwake umo Ufalme wa kila kitu; na kwake Yeye mtarejeshwa. 

 

37 - ASS'AFFAT

KWA JINA LA MWENYEZI MUNGU MWINGI WA REHEMA MWENYE KUREHEMU. 

 

1. Naapa kwa wanao jipanga kwa safu. 

2. Na kwa wenye kukataza mabaya. 

3. Na kwa wenye kusoma Ukumbusho. 

4. Hakika Mungu wenu bila ya shaka ni Mmoja. 

5. Mola Mlezi wa mbingu na ardhi, na yaliyomo kati yao, na ni Mola Mlezi wa mashariki zote. 

6. Hakika Sisi tumeipamba mbingu ya karibu kwa pambo la nyota. 

7. Na kulinda na kila shet'ani a'si. 

8. Wasiweze kuwasikiliza viumbe watukufu. Na wanafukuzwa huko kila upande. 

9. Wakifurushwa. Na wanayo adhabu ya kudumu. 

10. Isipo kuwa anaye nyakua kitu kidogo, na mara humfwatia kimondo kinacho ng'ara. 

11. Hebu waulize: Je! Wao ni wenye umbo gumu zaidi au hao wengine tulio waumba. Hakika Sisi tuliwaumba wao kwa udongo unao nata. 

12. Bali unastaajabu, na wao wanafanya maskhara. 

13. Na wanapo kumbushwa hawakumbuki. 

14. Na wanapo ona Ishara, wanafanya maskhara. 

15. Na husema: Haya si chochote ila ni uchawi tu ulio dhaahiri. 

16. Ati tukisha kufa na tukawa udongo na mifupa ndio kweli tutafufuliwa? 

17. Hata baba zetu wa zamani? 

18. Sema: Naam! Hali nanyi ni madhalili. 

19. Huko utapigwa ukelele mmoja tu! Na hapo ndio wataona! 

20. Watasema: Ole wetu! Hii ndiyo Siku ya Malipo. 

21. Hii ndiyo Siku ya Hukumu mliyo kuwa mkiikadhibisha. 

22. Wakusanyeni walio dhulumu, na wake zao, na hao walio kuwa wakiwaabudu - 

23. Badala ya Mwenyezi Mungu. Waongozeni njia ya Jahannamu! 

24. Na wasimamisheni. Hakika hao watasailiwa: 

25. Mna nini? Mbona hamsaidiani? 

26. Bali hii leo, watasalimu amri. 

27. Watakabiliana wao kwa wao kuulizana. 

28. Watasema: Kwa hakika nyinyi mlikuwa mkitujia upande wa kulia. 

29. Watasema (wakubwa): Bali nyinyi wenyewe hamkuwa Waumini. 

30. Sisi hatukuwa na mamlaka juu yenu, bali nyinyi wenyewe mlikuwa wapotovu. 

31. Basi hukumu ya Mola wetu Mlezi imekwisha tuthibitikia. Hakika bila ya shaka tutaonja tu adhabu. 

32. Tulikupotezeni kwa sababu sisi wenyewe tulikuwa wapotovu. 

33. Basi wao kwa hakika siku hiyo watashirikiana katika adhabu pamoja. 

34. Hivyo ndivyo tutakavyo wafanyia wakosefu. 

35. Wao walipo kuwa wakiambiwa La ilaha illa 'Llahu Hapana mungu ila Mwenyezi Mungu tu, wakijivuna. 

36. Na wakisema: Hivyo sisi tuiache miungu yetu kwa ajili ya huyu mtunga mashairi mwendawazimu? 

37. Bali huyu amekuja kwa Haki, na amewasadikisha Mitume. 

38. Hakika nyinyi bila ya shaka mtaionja adhabu chungu. 

39. Wala hamlipwi ila hayo mliyo kuwa mkiyafanya. 

40. Isipo kuwa waja wa Mwenyezi Mungu walio khitariwa. 

41. Hao ndio watakao pata riziki maalumu, 

42. Matunda, nao watahishimiwa. 

43. Katika Bustani za neema. 

44. Wako juu ya viti wamekabiliana. 

45. Wanazungushiwa kikombe chenye kinywaji cha chemchem 

46. Kinywaji cheupe, kitamu kwa wanywao. 

47. Hakina madhara, wala hakiwaleweshi. 

48. Na watakuwa nao wanawake wenye macho ya staha mazuri. 

49. Hao wanawake kama mayai yaliyo hifadhika. 

50. Waingie kuulizana wenyewe kwa wenyewe. 

51. Aseme msemaji mmoja miongoni mwao: Hakika mimi nalikuwa na rafiki 

52. Aliye kuwa akinambia: Hivyo wewe ni katika wanao sadiki 

53. Ati tukisha kufa tukawa udongo na mafupa, ndio tutalipwa na kuhisabiwa? 

54. Atasema: Je! Nyie mnawaona? 

55. Basi atachungulia amwone katikati ya Jahannamu. 

56. Atasema: Wallahi! Ulikaribia kunipoteza. 

57. Na lau kuwa si neema ya Mola wangu Mlezi bila ya shaka ningeli kuwa miongoni mwa walio hudhurishwa. 

58. Je! Sisi hatutakufa, 

59. Isipo kuwa kifo chetu cha kwanza? Wala sisi hatutaadhibiwa. 

60. Hakika huku bila ya shaka ndiko kufuzu kukubwa. 

61. Kwa mfano wa haya nawatende watendao. 

62. Je! Kukaribishwa hivi si ndio bora, au mti wa Zaqqum? 

63. Hakika Sisi tumeufanya huo kuwa ni mateso kwa walio dhulumu. 

64. Hakika huo ni mti unao toka katikati ya Jahannamu. 

65. Mashada ya matunda yake kama kwamba vichwa vya mashet'ani. 

66. Basi hakika bila ya shaka hao watayala hayo, na wajaze matumbo. 

67. Kisha juu yake wanyweshwe mchanganyo wa maji yamoto yaliyo chemka. 

68. Kisha hakika marejeo yao bila ya shaka yatakuwa kwenye Jahannamu. 

69. Hakika waliwakuta baba zao wamepotea. 

70. Na wao wakafanya haraka kufuata nyayo zao. 

71. Na bila ya shaka walikwisha potea kabla yao wengi wa watu wa zamani. 

72. Na Sisi hakika tuliwapelekea waonyaji. 

73. Basi hebu angalia ulikuwaje mwisho wa walio onywa. 

74. Isipo kuwa waja wa Mwenyezi Mungu walio khitariwa. 

75. Na hakika Nuhu alitwita, na Sisi ni bora wa waitikiaji. 

76. Na tulimwokoa yeye na ahali zake kutokana na msiba mkubwa. 

77. Na tuliwajaalia dhuriya zake ndio wenye kubakia. 

78. Na tukamwachia (sifa njema) kwa walio kuja baadaye. 

79. Iwe salama kwa Nuhu ulimwenguni kote! 

80. Kwa hakika hivi ndivyo tunavyo walipa wanao fanya mema. 

81. Hakika yeye ni katika waja wetu walio amini. 

82. Kisha tukawazamisha wale wengine. 

83. Na hakika Ibrahim alikuwa katika kundi lake, 

84. Alipo mjia Mola wake Mlezi kwa moyo mzima. 

85. Alimwambia baba yake na watu wake: Mnaabudu nini? 

86. Kwa kuzua tu mnataka miungu mingine badala ya Mwenyezi Mungu? 

87. Mnamdhania nini Mola Mlezi wa walimwengu wote? 

88. Kisha akapiga jicho kutazama nyota. 

89. Akasema: Hakika mimi ni mgonjwa! 

90. Nao wakamwacha, wakampa kisogo. 

91. Basi akaiendea miungu yao kwa siri, akaiambia: Mbona hamli? 

92. Mna nini hata hamsemi? 

93. Kisha akaigeukia kuipiga kwa mkono wa kulia. 

94. Basi wakamjia upesi upesi. 

95. Akasema: Hivyo mnaviabudu vitu mnavyo vichonga wenyewe? 

96. Na hali Mwenyezi Mungu ndiye aliye kuumbeni nyinyi na hivyo mnavyo vifanya! 

97. Wakasema: Mjengeeni jengo, na kisha mtupeni motoni humo! 

98. Basi walitaka kumfanyia vitimbi, lakini tukawafanya wao ndio wa chini. 

99. Na akasema: Hakika mimi nahama, nakwenda kwa Mola wangu Mlezi; Yeye ataniongoa. 

100. Ewe Mola wangu Mlezi! Nitunukie aliye miongoni mwa watenda mema. 

101. Basi tukambashiria mwana aliye mpole. 

102. Basi alipo fika makamo ya kwenda na kurudi pamoja naye, alimwambia: Ewe mwanangu! Hakika mimi nimeona usingizini kuwa ninakuchinja. Basi angalia wewe, waonaje? Akasema: Ewe baba yangu! Tenda unavyo amrishwa, utanikuta mimi, Inshallah, katika wanao subiri. 

103. Basi wote wawili walipo jisalimisha, na akamlaza juu ya kipaji. 

104. Tulimwita: Ewe Ibrahim! 

105. Umekwisha itimiliza ndoto. Hakika hivi ndivyo tunavyo walipa wanao tenda mema. 

106. Hakika haya ni majaribio yaliyo dhaahiri. 

107. Basi tukamtolea fidia kwa dhabihu mtukufu. 

108. Na tukamwachia (sifa njema) kwa watu walio kuja baadaye. 

109. Iwe salama kwa Ibrahim! 

110. Hivi ndivyo tunavyo walipa wanao fanya mema. 

111. Hakika yeye ni katika waja wetu walio amini. 

112. Na tukambashiria kuzaliwa Is-haqa, naye ni Nabii miongoni mwa watu wema. 

113. Na tukambarikia yeye na Is-haqa. Na miongoni mwa dhuriya zao walitokea wema na wenye kudhulumu nafsi zao waziwazi. 

114. Na kwa hakika tuliwafanyia hisani Musa na Haruni. 

115. Na tukawaokoa wao na watu wao kutokana na dhiki kubwa. 

116. Na tukawanusuru; na wakawa wao ndio wenye kushinda. 

117. Na tukawapa wawili hao Kitabu kinacho bainisha. 

118. Na tukawaongoa kwenye Njia Iliyo Nyooka. 

119. Na tukawaachia (sifa njema) katika watu walio kuja baadaye. 

120. Iwe salama kwa Musa na Haruni! 

121. Hakika hivyo ndivyo tunavyo walipa walio wema. 

122. Hakika wawili hao ni katika waja wetu walio amini. 

123. Na hakika Ilyas bila ya shaka alikuwa miongoni mwa Mitume. 

124. Alipo waambia watu wake: Hamwogopi? 

125. Mnamwomba Baa'li na mnamwacha Mbora wa waumbaji, 

126. Mwenyezi Mungu, Mola Mlezi wenu na Mola Mlezi wa baba zenu wa zamani? 

127. Wakamkadhibisha. Basi kwa hakika watahudhurishwa; 

128. Isipo kuwa waja wa Mwenyezi Mungu walio safishwa. 

129. Na tumemwachia (sifa nzuri) kwa walio kuja baadaye. 

130. Iwe salama kwa Ilyas. 

131. Hakika hivyo ndivyo tunavyo walipa walio wema. 

132. Hakika yeye ni katika waja wetu walio amini. 

133. Na hakika Lut'i bila ya shaka ni miongoni mwa Mitume. 

134. Tulipo mwokoa yeye na ahali zake wote, 

135. Isipo kuwa mwanamke mkongwe katika wale walio bakia nyuma. 

136. Kisha tukawaangamiza wale wengineo. 

137. Na hakika nyinyi mnawapitia wakati wa asubuhi, 

138. Na usiku. Basi je! Hamyatii akilini? 

139. Na hakika Yunus alikuwa miongoni mwa Mitume. 

140. Alipo kimbia katika jahazi lilio sheheni. 

141. Akaingia katika kupigiwa kura, na akawa katika walio shindwa. 

142. Samaki akammeza hali ya kuwa ni mwenye kulaumiwa. 

143. Na ingeli kuwa hakuwa katika wanao mtakasa Mwenyezi Mungu, 

144. Bila ya shaka angeli kaa ndani yake mpaka siku ya kufufuliwa. 

145. Lakini tulimtupa ufukweni patupu, hali yu mgonjwa. 

146. Na tukauotesha juu yake mmea wa kabila ya mung'unye. 

147. Na tulimtuma kwa watu laki moja au zaidi. 

148. Basi wakaamini, na tukawastarehesha kwa muda. 

149. Basi waulize: Ati Mola wako Mlezi ndiye mwenye watoto wa kike, na wao wanao watoto wa kiume? 

150. Au tumewaumba Malaika kuwa ni wanawake, na wao wakashuhudia? 

151. Ati ni kwa uzushi wao ndio wanasema: 

152. Mwenyezi Mungu amezaa! Ama hakika bila ya shaka hao ni waongo! 

153. Ati amekhiari watoto wa kike kuliko wanaume? 

154. Mna nini? Mnahukumu vipi nyinyi? 

155. Hamkumbuki? 

156. Au mnayo hoja iliyo wazi? 

157. Basi leteni Kitabu chenu kama mnasema kweli. 

158. Na wameweka makhusiano ya nasaba baina yake na majini; na majini wamekwisha jua bila ya shaka kuwa wao watahudhurishwa. 

159. Subhana 'Llah Ametakasika Mwenyezi Mungu na hayo wanayo msingizia. 

160. Isipo kuwa waja wa Mwenyezi Mungu walio safishwa. 

161. Basi hakika nyinyi na mnao waabudu 

162. Hamwezi kuwapoteza 

163. Isipo kuwa yule atakaye ingia Motoni. 

164. Na hapana katika sisi ila anapo mahali pake maalumu. 

165. Na hakika bila ya shaka sisi ndio wajipangao safu. 

166. Na hakika sisi ndio wenye kusabihi kutakasa. 

167. Na walikuwapo walio kuwa wakisema: 

168. Tungeli kuwa na Ukumbusho kama wa watu wa zamani, 

169. Bila ya shaka tungeli kuwa ni waja wa Mwenyezi Mungu wenye ikhlasi. 

170. Lakini waliukataa. Basi watakuja jua. 

171. Na bila ya shaka neno letu lilikwisha tangulia kwa waja wetu walio tumwa. 

172. Ya kuwa wao bila ya shaka ndio watakao nusuriwa. 

173. Na kwamba jeshi letu ndilo litakalo shinda. 

174. Basi waachilie mbali kwa muda. 

175. Na watazame, nao wataona. 

176. Je! Wanaihimiza adhabu yetu? 

177. Basi itakapo shuka uwanjani kwao, itakuwa asubuhi mbaya kwa walio onywa. 

178. Na waache kwa muda. 

179. Na tazama, na wao wataona. 

180. Subhana Rabbi'l'Izzat Ametakasika Mola Mlezi Mwenye enzi na yale wanayo mzulia. 

181. Na Salamu juu ya Mitume. 

182. Na sifa njema zote ni za Mwenyezi Mungu Mola Mlezi wa walimwengu wote. 

 

38 - S'AAD

KWA JINA LA MWENYEZI MUNGU MWINGI WA REHEMA MWENYE KUREHEMU. 

 

1. S'ad, Naapa kwa Qur'ani yenye mawaidha. 

2. Lakini walio kufuru wamo katika majivuno na upinzani 

3. Mataifa mangapi tumeyaangamiza kabla yao, na wakapiga kelele, lakini wakati wa kuokoka ulikwisha pita. 

4. Na walistaajabu kuwajia mwonyaji anaye tokana nao wenyewe, na makafiri wakasema: Huyu ni mchawi, mwongo. 

5. Amewafanya miungu wote kuwa ni Mungu Mmoja tu? Hakika hili ni jambo la ajabu. 

6. Na wakaondoka wakubwa wao wakiwaambia: Nendeni zenu na dumuni na miungu yenu, kwani hili ni jambo lililo pangwa. 

7. Sisi hatukusikia haya katika mila hii ya mwisho. Haya si chochote ila ni uzushi tu. 

8. Ati yeye tu ndiye aliye teremshiwa mawaidha peke yake katika sisi? Lakini hao wana shaka na mawaidha yangu, bali hawajaionja adhabu yangu. 

9. Au wanazo wao khazina za rehema za Mola wako Mlezi, Mwenye nguvu, Mpaji? 

10. Au wao wana ufalme wa mbingu na ardhi na viliomo kati yao? Basi nawazipande njia za kwendea huko! 

11. Hao ni askari watao shindwa miongoni mwa makundi yatayo shindwa. 

12. Walikanusha kabla yao kaumu ya Nuhu, na kina A'adi na Firauni mwenye majengo. 

13. Na Thamud na kaumu Lut'i na watu wa Machakani. Hayo ndiyo makundi. 

14. Hao wote waliwakadhibisha Mitume; basi wakastahiki adhabu yangu. 

15. Na hawa hawangojei ila ukelele mmoja tu usio na muda. 

16. Na wao husema: Mola wetu Mlezi! Tuletee upesi sehemu yetu ya adhabu kabla ya Siku ya Hisabu. 

17. Subiri kwa hayo wayasemayo, na umkumbuke mja wetu Daudi, mwenye nguvu. Hakika yeye alikuwa mwingi wa kutubia. 

18. Hakika tuliidhalilisha milima pamoja naye ikisabihi jioni na asubuhi pamoja naye. 

19. Na pia ndege walio kusanywa makundi kwa makundi; wote walikuwa wanyenyekevu kwake. 

20. Na tukautia nguvu ufalme wake, na tukampa hikima, na kukata hukumu. 

21. Na je! Imekufikia khabari ya wagombanao walipo pindukia ukuta kuingia chumbani? 

22. Walipo muingilia Daudi, naye akawaogopa. Wakasema: Usiogope! Sisi ni wagombanao wawili, mmoja wetu amemdhulumu mwenziwe. Basi tuhukumu kwa haki, wala usipendelee. Na utuongoe kwenye njia iliyo sawa. 

23. Hakika huyu ndugu yangu ana kondoo wa kike tisiini na tisa; na mimi ninaye kondoo mke mmoja. Akasema: Nipe huyo nikufugie! Na amenishinda kwa maneno. 

24. Akasema: Kweli amekudhulumu kwa kumtaka kondoo wako mmoja kuongezea kwenye kondoo wake. Na hakika washirika wengi hudhulumiana wao kwa wao, isipo kuwa walio amini na wakatenda mema. Na hao ni wachache. Na Daudi akajua kuwa tumemfanyia mtihani. Basi akamwomba msamaha Mola wake Mlezi, na akaanguka kusujudu na kutubia. 

25. Basi tukamsamehe kwa hayo. Naye kwa hakika anao mkaribisho mkubwa na marejeo mazuri kwetu. 

26. Ewe Daudi! Hakika Sisi tumekufanya wewe uwe Khalifa katika nchi. Basi wahukumu watu kwa haki, wala usifuate matamanio yakakupoteza kwenye Njia ya Mwenyezi Mungu. Hakika wanao ipotea Njia ya Mwenyezi Mungu wakaiacha, watapata adhabu kali kwa sababu ya kusahau kwao Siku ya Hisabu. 

27. Na hatukuziumba mbingu na ardhi na viliomo ndani yao bure. Hiyo ni dhana ya walio kufuru. Ole wao walio kufuru kwa Moto utao wapata. 

28. Je! Tuwafanye walio amini na wakatenda mema kama wafanyao uharibifu katika nchi? Au tuwafanye wachamngu kama waovu? 

29. Na hiki Kitabu, tumekuteremshia wewe, kimebarikiwa, ili wazizingatie Aya zake, na wawaidhike wenye akili. 

30. Na Daudi tukamtunukia Suleiman. Alikuwa mja mwema. Na hakika alikuwa mwingi wa kutubia. 

31. Alipo pelekewa jioni farasi wasimamao kidete, tayari kutoka shoti; 

32. Basi akasema: Navipenda vitu vizuri kwa kumkumbuka Mola wangu Mlezi. Kisha wakafichikana nyuma ya boma. 

33. (Akasema:) Nirudishieni! Akaanza kuwapapasa miguu na shingo. 

34. Na tulimtia mtihanini Suleiman, na tukauweka mwili juu ya kiti chake, kisha akarejea kwa kutubu. 

35. Akasema: Mola wangu Mlezi! Nisamehe na unipe ufalme usio mwelekea yeyote baada yangu. Hakika Wewe ndiye Mpaji. 

36. Basi tukaufanya upepo umtumikie, ukenda kwa amri yake, popote alipo taka kufika. 

37. Na tukayafanya mashet'ani yamtumikie, wote wajenzi na wapiga mbizi. 

38. Na wengine wafungwao kwa minyororo. 

39. Hichi ndicho kipawa chetu. Basi toa au zuia, bila ya hisabu. 

40. Na hakika yeye kwetu Sisi ana cheo cha kukaribishwa kwetu, na pahala pazuri pa kurejea. 

41. Na mkumbuke mja wetu Ayubu alipo mwita Mola wake Mlezi akasema: Kwa hakika Shet'ani amenifikishia udhia na adhabu. 

42. (Akaambiwa:) Piga-piga ardhi kwa mguu wako! Basi haya maji baridi ya kuogea na ya kunywa. 

43. Na tukampa ahali zake na wengine kama wao pamoja nao, kuwa ni rehema itokayo kwetu, na iwe kumbusho kwa watu wenye akili. 

44. Na shika kicha cha vijiti tu mkononi mwako, kisha ndio upigie nacho, wala usivunje kiapo. Hakika tulimkuta mwenye subira, mbora wa waja, kwa hakika alikuwa mwingi wa kutubu. 

45. Na wakumbuke waja wetu, Ibrahim na Is-haqa na Yaa'qubu walio kuwa na nguvu na busara. 

46. Sisi tumewakhusisha wao kwa sifa ya ukumbusho wa Akhera. 

47. Na hakika wao kwetu sisi ni wateuliwa walio bora. 

48. Na mkumbuke Ismail na Alyasaa na Dhulkifli, na wote hao ni katika walio bora. 

49. Huu ni ukumbusho. Na hakika wachamngu wana marudio mazuri. 

50. Bustani za milele zitazo funguliwa milango yao kwa ajili yao. 

51. Humo wataegemea matakia, wawe wanaagiza humo matunda mengi na vinywaji. 

52. Na pamoja nao wake zao wenye kutuliza macho, hirimu zao. 

53. Haya ndiyo mliyo ahidiwa kwa Siku ya Hisabu. 

54. Hakika hii ndiyo riziki yetu isiyo malizika. 

55. Ndio hivi! Na hakika wenye kuasi bila ya shaka watapata marudio maovu kabisa; 

56. Nayo ni Jahannamu! Wataingia humo. Nacho hicho ni kitanda kiovu mno cha kulalia. 

57. Ndio hivi! Basi na wayaonje maji ya moto na ya usaha! 

58. Na adhabu nyenginezo za namna hii. 

59. Hili ndilo kundi litakalo ingia pamoja nanyi. Hapana makaribisho mema kwao. Hakika hao wanaingia Motoni. 

60. Waseme: Lakini nyinyi! Hamna mapokezi mazuri! Nyinyi ndio mlio tusabibisha haya, napo ni pahala paovu kabisa! 

61. Waseme: Mola wetu Mlezi! Aliye tusabibisha haya mzidishie adhabu mara mbili Motoni. 

62. Watasema: Tuna nini hata hatuwaoni wale watu ambao tukiwahisabu ndio katika waovu? 

63. Tulikosea tulipo wafanyia maskhara, au macho yetu tu hayawaoni ? 

64. Hakika hayo bila ya shaka ndiyo makhasimiano ya watu wa Motoni. 

65. Sema: Hakika mimi ni mwonyaji tu; na hapana mungu ila Mwenyezi Mungu Mmoja, Mtenda nguvu, 

66. Mola Mlezi wa mbingu na ardhi na viliomo baina yake, Mwenye nguvu, Mwenye kusamehe. 

67. Sema: Hii ni khabari kubwa kabisa. 

68. Ambayo nyinyi mnaipuuza. 

69. Sikuwa na ilimu ya mambo ya viumbe wakuu watukufu walipo kuwa wakishindana. 

70. Haikufunuliwa kwangu isipo kuwa ya kwamba hakika mimi ni mwonyaji dhaahiri. 

71. Mola wako Mlezi alipo waambia Malaika: Hakika Mimi nitaumba mtu kutokana na udongo. 

72. Na nitakapo mkamilisha na kumpulizia roho inayo tokana nami, basi muangukieni kwa kumt'ii. 

73. Basi Malaika wakat'ii wote pamoja. 

74. Isipo kuwa Iblisi; alijivuna na akawa katika makafiri. 

75. Mwenyezi Mungu akamwambia: Ewe Iblisi! Kipi kilicho kuzuia kumt'ii yule niliye muumba kwa mikono yangu? Je! Umejiona mkubwa, au umekuwa katika wakuu kweli? 

76. Akasema: Mimi ni bora kuliko yeye. Umeniumba kwa moto, na yeye umemuumba kwa udongo. 

77. Akasema: Basi toka humo, kwani hakika wewe umelaanika. 

78. Na hakika laana yangu itakuwa juu yako mpaka Siku ya Malipo. 

79. Akasema: Mola wangu Mlezi! Nipe muhula mpaka siku watayo fufuliwa viumbe. 

80. Mwenyezi Mungu akasema: Basi umekwisha kuwa miongoni mwa walio pewa muhula, 

81. Mpaka siku ya wakati maalumu. 

82. Akasema (Iblisi): Naapa kwa utukufu wako, bila ya shaka nitawapoteza wote, 

83. Isipo kuwa wale waja wako miongoni mwao walio khitariwa. 

84. Akasema: Haki! Na haki ninaisema. 

85. Bila ya shaka nitaijaza Jahannamu kwa wewe na kwa hao wote wenye kukufuata miongoni mwao. 

86. Sema (Ewe Mtume) : Sikuombeni ujira juu ya haya, wala mimi si katika wadanganyifu. 

87. Hayakuwa haya ila ni mawaidha kwa walimwengu wote. 

88. Na bila ya shaka mtajua khabari zake baada ya muda. 

 

39 - AZZUMAR

KWA JINA LA MWENYEZI MUNGU MWINGI WA REHEMA MWENYE KUREHEMU. 

 

1. Mteremsho wa Kitabu hiki umetokana na Mwenyezi Mungu, Mwenye nguvu, Mwenye hikima. 

2. Hakika Sisi tumekuteremshia Kitabu hiki kwa Haki. Basi muabudu Mwenyezi Mungu ukimsafia Dini Yeye tu. 

3. Hakika Dini Safi ni ya Mwenyezi Mungu tu. Na wale wanao wafanya wenginewe kuwa ni walinzi wakisema: Sisi hatuwaabudu ila wapate kutujongeza tu kumkaribia Mwenyezi Mungu - Hakika Mwenyezi Mungu atahukumu baina yao katika wanayo khitalifiana. Hakika Mwenyezi Mungu hamwongoi aliye mwongo kafiri. 

4. Lau kuwa Mwenyezi Mungu angeli taka kuwa na mwana, basi bila ya shaka angeli teua amtakaye katika alio waumba. Subhanahu, Ametakasika na hayo! Yeye ni Mwenyezi Mungu Mmoja, Mtenda atakalo. 

5. Ameumba mbingu na ardhi kwa Haki. Hufunika usiku juu ya mchana, na hufunika mchana juu ya usiku. Na amefanya jua na mwezi vitumike. Kila kimojapo kinakwenda kwa kipindi kilicho wekewa. Jueni mtanabahi! Yeye ndiye Mwenye nguvu, Mwenye kusamehe! 

6. Amekuumbeni kutokana na nafsi moja. Kisha akamfanya mwenziwe katika nafsi ile ile. Na akakuleteeni wanyama wa mifugo jozi nane. Anakuumbeni katika matumbo ya mama zenu, umbo baada ya umbo, katika viza vitatu. Huyu ndiye Mwenyezi Mungu Mola wenu Mlezi. Ufalme ni wake. Hapana mungu isipo kuwa Yeye. Basi nyinyi mnageuzwa wapi? 

7. Mkikufuru basi Mwenyezi Mungu si mwenye haja nanyi, lakini hafurahii kufuru kwa waja wake. Na mkishukuru Yeye hufurahika nanyi. Wala mbebaji habebi mzigo wa mwingine. Kisha marejeo yenu ni kwa Mola wenu Mlezi. Hapo atakwambieni mliyo kuwa mkiyafanya. Hakika Yeye ni Mwenye kuyajua vyema yaliyomo vifuani. 

8. Na taabu inapo mfikia mtu humwomba Mola wake Mlezi naye ameelekea kwake. Kisha akimpa neema kutoka kwake, husahau yale aliyo kuwa akimwitia zamani, na akamfanyia Mwenyezi Mungu washirika ili apoteze watu njia yake. Sema: Starehe na ukafiri wako kwa muda mchache. Kwani hakika wewe utakuwa miongoni mwa watu wa Motoni. 

9. Je! Afanyae ibada nyakati za usiku kwa kusujudu na kusimama akitahadhari na Akhera, na akitaraji rehema za Mola wake Mlezi...Sema: Ati watakuwa sawa wale wanao jua na wale wasio jua? Hakika wanao kumbuka ni watu wenye akili. 

10. Sema: Enyi waja wangu mlio amini! Mcheni Mola wenu Mlezi. Wale wafanyao wema katika dunia hii watapata wema. Na ardhi ya Mwenyezi Mungu ni kunjufu. Hakika wenye subira watapewa ujira wao bila ya hisabu. 

11. Sema: Hakika mimi nimeamrishwa nimuabudu Mwenyezi Mungu kwa kumsafishia Dini Yeye tu. 

12. Na nimeamrishwa niwe wa mwanzo wa Waislamu. 

13. Sema: Hakika mimi ninaogopa adhabu ya Siku Kubwa nikimuasi Mola wangu Mlezi. 

14. Sema: Mwenyezi Mungu tu namuabudu kwa kumsafishia Yeye tu Dini yangu. 

15. Basi nyinyi abuduni mpendacho badala yake Yeye. Sema: Hakika walio khasirika ni wale walio jikhasiri nafsi zao na ahali zao Siku ya Kiyama. Tambueni kuwa hiyo ndiyo khasara iliyo dhaahiri. 

16. Yatawekwa juu yao mat'abaka ya moto, na chini yao mat'abaka. Kwa hayo Mwenyezi Mungu anawakhofisha waja wake. Enyi waja wangu! Nicheni Mimi! 

17. Na wale wanao jiepusha na ibada potovu, na wakarejea kwa Mwenyezi Mungu, watapata bishara njema. Basi wabashirie waja wangu. 

18. Ambao husikiliza maneno, wakafuata lilio bora yao. Hao ndio alio waongoa Mwenyezi Mungu, na hao ndio wenye akili. 

19. Je! Yule mwenye kustahiki hukumu ya adhabu, je, wewe unaweza kumwokoa aliyomo katika Moto? 

20. Lakini walio mcha Mola wao Mlezi watapata ghorofa zilizo jengwa juu ya ghorofa; chini yake hupita mito. Ndiyo ahadi ya Mwenyezi Mungu. Mwenyezi Mungu havunji ahadi yake. 

21. Je! Huoni kwamba Mwenyezi Mungu ameteremsha maji kutoka mbinguni. Kisha akayapitisha kwenye chemchem katika ardhi, kisha kwa maji hayo akatoa mimea yenye rangi mbali mbali? Kisha hunyauka ukaiona imekuwa kimanjano, na kisha huifanya mapepe. Bila ya shaka katika hayo upo ukumbusho kwa wenye akili. 

22. Je! Yule ambaye Mwenyezi Mungu amemfungulia kifua chake kwa Uislamu, na akawa yuko kwenye nuru itokayo kwa Mola wake Mlezi (ni sawa na mwenye moyo mgumu?) Basi ole wao wenye nyoyo ngumu zisio mkumbuka Mwenyezi Mungu! Hao wamo katika upotofu wa dhaahiri. 

23. Mwenyezi Mungu ameteremsha hadithi nzuri kabisa, Kitabu chenye kufanana na kukaririwa; husisimua kwacho ngozi za wenye kumkhofu Mola wao Mlezi. Kisha ngozi zao na nyoyo zao hulainika kwa kumkumbuka Mwenyezi Mungu. Huo ndio uwongofu wa Mwenyezi Mungu, na kwa huo humwongoa amtakaye. Na ambaye ameachwa na Mwenyezi Mungu kupotea, basi hapana wa kumwongoa. 

24. Je! Atakaye kuwa anapambana kwa uso wake na adhabu mbaya kabisa Siku ya Kiyama (ni sawa na watenda wema?) Na wataambiwa wenye kudhulumu: Onjeni hayo mliyo kuwa mkiyachuma! 

25. Walio kuwa kabla yao walikadhibisha , na ikawajia adhabu kutoka pahala wasipo patambua. 

26. Basi Mwenyezi Mungu akawaonjesha hizaya katika uhai wa duniani. Na bila ya shaka adhabu ya Akhera ni kubwa zaidi; laiti wangeli jua! 

27. Na bila ya shaka tumewapigia watu mifano ya kila namna katika hii Qur'ani ili wapate kukumbuka. 

28. Qur'ani ya Kiarabu isiyo na upogo, ili wamche Mungu. 

29. Mwenyezi Mungu amepiga mfano wa mtu mwenye mabwana washirika wanao gombana, na wa mtu mwengine aliye khusika na bwana mmoja tu. Je! Wako sawa katika hali zao? Alhamdulillahi, Sifa njema zote ni za Mwenyezi Mungu! Lakini wengi wao hawajui. 

30. Kwa hakika wewe utakufa, na wao watakufa. 

31. Kisha bila ya shaka mtagombana Siku ya Kiyama mbele ya Mola wenu Mlezi.