Part 16

 

75. AKASEMA: Je! Sikukwambia kwamba hakika wewe huwezi kuvumilia kuwa pamoja nami? 

76. Akasema: Nikikuuliza kitu chochote baada ya haya usifuatane nami, kwani umekwisha pata udhuru kwangu. 

77. Basi wakatoka mpaka wakawafikia watu wa mji mmoja. Wakawaomba watu wake wawape chakula, nao wakakataa kuwakaribisha. Hapo wakakuta ukuta unataka kuanguka, (yule mja mwema) akausimamisha. (Musa) akasema: Ungeli taka ungeli chukua ujira kwa haya. 

78. (Yule mtu) akasema: Huku ndio kufarikiana baina yangu na wewe. Sasa nitakueleza maana ya yale uliyo kuwa huwezi kuyastahamilia. 

79. Ama ile jahazi ilikuwa ya masikini za Mungu wafanyao kazi baharini. Nilitaka kuiharibu, kwani nyuma yao alikuwako mfalme anaghusubu majahazi yote. 

80. Na ama yule kijana, wazazi wake walikuwa ni Waumini. Tukakhofu asije watia mashakani kwa uasi na ukafiri. 

81. Basi tulitaka Mola wao Mlezi awabadilishie aliye bora zaidi kuliko huyo kwa kutakasika, na aliye karibu zaidi kwa huruma. 

82. Na ama ukuta, huo ulikuwa ni wa vijana wawili mayatima kule mjini. Na chini yake ilikuwako khazina yao; na baba yao alikuwa ni mtu mwema. Basi Mola wako Mlezi alitaka wafikie utu uzima na wajitolee khazina yao wenyewe, kuwa ni rehema itokayo kwa Mola wako Mlezi. Wala mimi sikutenda hayo kwa amri yangu. Hiyo ndiyo tafsiri ya hayo ambayo wewe hukuweza kuyasubiria. 

83. Na wanakuuliza khabari za Dhul- Qarnaini. Waambie: Nitakusimulieni baadhi ya hadithi yake. 

84. Sisi tulimtilia nguvu katika ardhi na tukampa njia za kila kitu. 

85. Basi akaifuata njia. 

86. Hata alipo fika machwea-jua aliliona linatua katika checmchem yenye matope meusi. Na hapo akawakuta watu. Tukasema: Ewe Dhul-Qarnaini! Ama uwaadhibu au watwae kwa wema. 

87. Akasema: Ama aliye dhulumu basi tutamuadhibu, na kisha atarudishwa kwa Mola wake Mlezi amuadhibu adhabu isiyo juulikana. 

88. Na ama aliye amini na akatenda mema basi atapata malipo mazuri. Nasi tutamwambia lilio jepesi katika amri yetu. 

89. Kisha akaifuata njia. 

90. Hata alipo fika matokeo ya jua aliliona linawachomozea watu tusio wawekea pazia la kuwakinga nalo. 

91. Ndio hivyo hivyo. Na Sisi tulizijua vilivyo khabari zake zote. 

92. Kisha akaifuata njia. 

93. Hata alipo fika baina ya milima miwili, alikuta nyuma yake watu ambao takriban hawakuwa wanafahamu lolote. 

94. Wakasema: Ewe Dhul-Qarnaini! Hakika Juju-wa-maajuju wanafanya uharibifu katika nchi. Basi je, tukulipe ujira ili utujengee baina yetu na wao ngome? 

95. Akasema: Yale Mola wangu aliyo niwezesha ni bora zaidi. Lakini nyinyi nisaidieni kwa nguvu zenu. Nitakujengeeni kizuizi baina yenu na wao. 

96. Nileteeni vipande vya chuma. Hata alipo ijaza nafasi iliyo kati ya milima miwili, akasema: Vukuteni. Hata alipo kifanya (chuma) kama moto akasema: Nileteeni shaba iliyo yayuka niimwagie. 

97. Basi hawakuweza kuukwea, wala hawakuweza kuutoboa. 

98. Akasema: Hii ni rehema itokayo kwa Mola wangu Mlezi. Na itapo fika ahadi ya Mola wangu Mlezi atauvunja vunja. Na ahadi ya Mola wangu Mlezi ni kweli tu. 

99. Na siku hiyo tutawaacha wakisongana wao kwa wao. Na baragumu litapulizwa, na wote watakusanywa pamoja. 

100. Na siku hiyo tutawadhihirishia wazi Jahannamu makafiri waione. 

101. Wale ambao kwamba macho yao yalikuwa paziani hayanikumbuki, na wakawa hawawezi kusikia. 

102. Je, wanadhani walio kufuru ndio wawafanye waja wangu ndio walinzi wao badala yangu Mimi? Hakika Sisi tumeiandaa Jahannamu iwe ndipo mahala pa kuteremkia makafiri. 

103. Sema: Je, tukutajieni wenye khasara mno katika vitendo vyao? 

104. Ni wale ambao juhudi yao katika maisha ya dunia imepotea bure, nao wanadhani kwamba wanafanya kazi nzuri. 

105. Hao ni wale walio zikanusha Ishara za Mola wao Mlezi na kukutana naye. Kwa hivyo vitendo vyao vimepotea bure, na wala Siku ya Kiyama hatutawathamini kitu. 

106. Hiyo Jahannamu ni malipo yao kwa walivyo kufuru na wakafanyia kejeli Ishara zangu na Mitume wangu. 

107. Hakika wale walio amini na wakatenda mema mashukio yao yatakuwa kwenye Pepo za Firdausi. 

108. Watadumu humo; hawatataka kuondoka. 

109. Sema: Lau kuwa bahari ndio wino kwa maneno ya Mola wangu Mlezi, basi bahari ingeli malizika kabla ya kumalizika maneno ya Mola wangu Mlezi, hata tungeli ileta mfano wa hiyo kuongezea. 

110. Sema: Mimi ni mwanaadamu kama nyinyi. Ninaletewa Wahyi kwamba Mungu wenu ni Mungu Mmoja. Mwenye kutaraji kukutana na Mola wake Mlezi basi naatende vitendo vyema, wala asimshirikishe yeyote katika ibada ya Mola wake Mlezi. 

 

19 - MARYAM

KWA JINA LA MWENYEZI MUNGU MWINGI WA REHEMA MWENYE KUREHEMU. 

 

1. Kaf Ha Ya A'yn S'ad 

2. Huu ni Ukumbusho wa rehema ya Mola wako Mlezi kwa mja wake, Zakariya. 

3. Alipo mwita Mola wake Mlezi kwa siri. 

4. Akasema: Mola wangu Mlezi! Mafupa yangu yamedhoofika, na kichwa kinameremeta kwa mvi; wala, Mola wangu Mlezi, sikuwa mwenye bahati mbaya kwa kukuomba Wewe. 

5. Na hakika mimi nawakhofia jamaa zangu baada yangu. Na mke wangu ni tasa. Basi nipe mrithi kutoka kwako. 

6. Atakaye nirithi mimi na awarithi ukoo wa Yaaqub. Ewe Mola wangu Mlezi! Na umjaalie awe mwenye kuridhisha. 

7. (Akaambiwa): Ewe Zakariya! Hakika Sisi tunakubashiria mwana; jina lake ni Yahya. Hatujapata kumpa jina hilo yeyote kabla yake. 

8. Akasema: Ewe Mola wangu Mlezi! Vipi nitakuwa na mwana na hali mke wangu ni tasa, na mimi nimesha fikia ukongwe katika uzee? 

9. Akasema: Ndio hivyo hivyo amesema Mola wako Mlezi: Haya ni mepesi kwangu. Na hakika Mimi nilikwisha kuumba wewe zamani na hali hukuwa kitu. 

10. Akasema: Mola wangu Mlezi nijaalie Ishara. Akasema Ishara yako ni kuwa hutasema na watu kwa masiku matatu, na hali ni mzima. 

11. Basi akawatokea watu wake kutoka mihirabuni. Akawaashiria: Msabihini Mwenyezi Mungu asubuhi na jioni. 

12. Ewe Yahya! Kishike Kitabu kwa nguvu! Nasi tulimpa hikima angali mtoto. 

13. Na tukampa huruma itokayo kwetu, na utakaso, na akawa mchamungu. 

14. Na akawa mwema kwa wazazi wake, wala hakuwa jabari mua'si. 

15. Na amani iwe juu yake siku ya kuzaliwa, na siku ya kufa, na siku ya kufufuliwa. 

16. Na mtaje Maryamu katika Kitabu, pale alipo jitenga na jamaa zake mahali upande wa mashariki; 

17. Na akaweka pazia kujikinga nao. Tukampelekea Roho wetu, akajifananisha kwake sawa na mtu. 

18. (Maryamu) akasema: Hakika mimi najikinga kwa Mwingi wa Rehema aniepushe nawe, ukiwa ni mchamngu. 

19. (Malaika) akasema: Hakika mimi ni mwenye kutumwa na Mola wako Mlezi ili nikubashirie tunu ya mwana aliye takasika. 

20. Akasema: Nitampataje mwana hali mwanaadamu yeyote hajanigusa, wala mimi si kahaba? 

21. (Malaika) akasema: Ndio hivyo hivyo! Mola wako Mlezi amesema: Haya ni mepesi kwangu! Na ili tumfanye kuwa ni Ishara kwa watu, na Rehema itokayo kwetu, na hilo ni jambo lilio kwisha hukumiwa. 

22. Basi akachukua mimba yake, na akaondoka nayo mpaka mahali pa mbali. 

23. Kisha uchungu ukampeleka kwenye shina la mtende; akasema: Laiti ningeli kufa kabla ya haya, na nikawa niliye sahaulika kabisa! 

24. Pakatangazwa kutoka chini yake: Usihuzunike! Hakika Mola wako Mlezi amejaalia chini yako kijito kidogo cha maji! 

25. Na litikise kwako hilo shina la mtende, utakuangushia tende nzuri zilizo mbivu. 

26. Basi kula, na kunywa, na litue jicho lako. Na pindi ukimwona mtu yeyote basi sema: Hakika mimi nimeweka nadhiri kwa Mwenyezi Mungu ya kufunga; kwa hivyo leo sitasema na mtu. 

27. Akenda naye (mwanawe) kwa jamaa zake amembeba. Wakasema: Ewe Maryamu! Hakika umeleta kitu cha ajabu! 

28. Ewe dada yake Harun! Baba yako hakuwa mtu muovu, wala mama yako hakuwa kahaba. 

29. Akawaashiria (mtoto). Wakasema: Vipi tumsemeze aliye bado mdogo yumo katika mlezi? 

30. (Mtoto) akasema: Hakika mimi ni mtumwa wa Mwenyezi Mungu. Amenipa Kitabu, na amenifanya Nabii. 

31. Na amenijaalia ni mwenye kubarikiwa popote pale niwapo. Na ameniusia Sala na Zaka maadamu ni hai, 

32. Na nimtendee wema mama yangu. Wala hakunifanya niwe jeuri, mwovu. 

33. Na amani iko juu yangu siku niliyo zaliwa, na siku nitakayo kufa, na siku nitakayo fufuliwa kuwa hai. 

34. Huyo ndiye Isa mwana wa Maryamu. Ndiyo kauli ya haki ambayo wanaifanyia shaka. 

35. Haiwi kwa Mwenyezi Mungu kuwa na mwana, Subhanahu, Yeye ametakasika! Anapo lihukumia jambo basi huliambia tu: Kuwa! Likawa. 

36. Na hakika Mwenyezi Mungu ni Mola wangu Mlezi, na Mola wenu Mlezi. Basi muabuduni Yeye. Hii ndiyo Njia Iliyo Nyooka. 

37. Lakini makundi yakakhitalifiana wao kwa wao. Basi ole wao hao walio kufuru kwa kuhudhuria Siku iliyo kuu! 

38. Watasikia na wataona vizuri vilioje Siku watakayo tufikia! Lakini madhaalimu sasa wamo katika upotofu ulio dhaahiri. 

39. Na waonye siku ya majuto itapo katwa amri. Nao wamo katika ghafla, wala hawaamini. 

40. Hakika Sisi tutairithi ardhi na walio juu yake. Na kwetu watarejeshwa. 

41. Na mtaje katika Kitabu Ibrahim. Hakika yeye alikuwa mkweli, Nabii. 

42. Alipo mwambia baba yake: Ewe baba yangu! Kwa nini unaabudu visivyo sikia, na visivyo ona, na visivyo kufaa chochote? 

43. Ewe baba yangu! Kwa yakini imenifikia ilimu isiyo kufikia wewe. Basi nifuate mimi, nami nitakuongoza Njia Iliyo Sawa. 

44. Ewe baba yangu! Usimuabudu Shet'ani. Hakika Shet'ani ni mwenye kumuasi Mwingi wa Rehema. 

45. Ewe baba yangu! Hakika mimi naogopa isikupate adhabu inayo toka kwa Mwingi wa Rehema ukaja kuwa mwenziwe Shet'ani. 

46. (Baba) akasema: Unaichukia miungu yangu, ewe Ibrahim? Kama huachi, basi lazima nitakupiga mawe. Na niondokelee mbali kwa muda! 

47. (Ibrahim) akasema: Salamun a'laika! Amani iwe juu yako! Mimi nitakuombea msamaha kwa Mola wangu Mlezi. Hakika Yeye ananihurumia sana. 

48. Nami najitenga nanyi na hayo mnayo yaabudu badala ya Mwenyezi Mungu. Na ninamwomba Mola wangu Mlezi; asaa nisiwe mwenye kukosa bahati kwa kumwomba Mola wangu Mlezi. 

49. Basi alipo jitenga nao na yale waliyo kuwa wakiyaabudu badala ya Mwenyezi Mungu, tulimpa Is-haq na Yaaqub, na kila mmoja tukamfanya Nabii. 

50. Na tukawapa rehema zetu na tukawajaalia kupewa sifa za kweli tukufu. 

51. Na mtaje Musa katika Kitabu. Hakika yeye alikuwa ni mwenye kuchaguliwa, na alikuwa Mtume, Nabii. 

52. Na tulimwita upande wa kulia wa mlima na tukamsogeza kunong'ona naye. 

53. Nasi kwa rehema zetu tukampa nduguye, Harun, awe Nabii. 

54. Na mtaje katika Kitabu Ismail. Bila ya shaka yeye alikuwa ni mkweli wa ahadi, na alikuwa Mtume, Nabii. 

55. Na alikuwa akiwaamrisha watu wake Sala na Zaka, na alikuwa mbele ya Mola wake Mlezi mwenye kuridhiwa. 

56. Na mtaje katika Kitabu Idris. Hakika yeye alikuwa ni mkweli Nabii. 

57. Na tulimuinua daraja ya juu. 

58. Hao ndio alio waneemesha Mwenyezi Mungu miongoni mwa Manabii katika uzao wa Adam, na katika uzao wa wale tulio wapandisha pamoja na Nuhu, na katika uzao wa Ibrahim na Israil, na katika wale tulio waongoa na tukawateuwa. Wanapo somewa Aya za Mwingi wa Rehema huanguka kusujudu na kulia. 

59. Lakini wakaja baada yao walio wabaya, wakaacha Sala, na wakafuata matamanio. Basi watakuja kuta malipo ya ubaya. 

60. Isipo kuwa walio tubu, wakaamini, na wakatenda mema. Hao, basi, wataingia Peponi wala hawatadhulumiwa chochote. 

61. Bustani za milele alizo waahidi Rahmani waja wake katika siri. Hakika ahadi yake hapana shaka itafika. 

62. Humo hawatasikia upuuzi, ila Salama tu. Na watapata humo riziki zao asubuhi na jioni. 

63. Hiyo ndiyo Pepo tutayo warithisha katika waja wetu walio kuwa wachamngu. 

64. (Nao watasema:) Wala hatuteremki ila kwa amri ya Mola wako Mlezi. Ni yake Yeye yaliyoko mbele yetu na yaliyoko nyuma yetu, na yaliyomo katikati ya hayo. Na Mola wako Mlezi si mwenye kusahau. 

65. Mola Mlezi wa mbingu na ardhi na vilivyo baina yake. Basi muabudu Yeye tu, na udumu katika ibada yake. Je, mnamjua mwenye jina kama lake? 

66. Na mwanaadamu husema: Hivyo, nitakapo kufa, ni kweli nitafufuliwa niwe hai tena? 

67. Je! Hakumbuki mwanaadamu ya kwamba tulimuumba kabla, na hali hakuwa chochote? 

68. Basi naapa kwa Mola wako Mlezi! Kwa yakini tutawakusanya wao pamoja na mashet'ani; kisha tutawahudhurisha kuizunguka Jahannamu, nao wamepiga magoti! 

69. Kisha kwa yakini tutawatoa katika kila kundi wale miongoni mwao walio zidi kumuasi Arrahmani, Mwingi wa Rahema.. 

70. Tena hakika Sisi tunawajua vyema zaidi wanao stahiki kuunguzwa humo. 

71. Wala hapana yeyote katika nyinyi ila ni mwenye kuifikia. Hiyo ni hukumu ya Mola wako Mlezi ambayo lazima itimizwe. 

72. Kisha tutawaokoa wale walio mchamngu; na tutawaacha madhaalimu humo wamepiga magoti. 

73. Na wanapo somewa Aya zetu zilizo wazi, walio kufuru huwaambia walio amini: Lipi katika makundi mawili lenye cheo kizuri na lilio bora barazani? 

74. Na kaumu ngapi tuliziangamiza zilizo kuwa na mapambo mazuri zaidi na wazuri zaidi kwa kuwatazama! 

75. Sema: Walio katika upotofu basi Arrahmani Mwingi wa Rahema atawapururia muda mpaka wayaone waliyo onywa - ama ni adhabu au ni Saa. Hapo ndipo watapo jua ni nani mwenye makao mabaya na mwenye askari dhaifu. 

76. Na Mwenyezi Mungu huwazidishia uwongofu wenye kushika uwongofu. Na mema yenye kudumu ni bora katika malipo mbele ya Mola wako Mlezi na yana mwisho mwema. 

77. Je, umemwona aliye zikanya Ishara zetu na akasema: Kwa hakika mimi nitapewa mali na wana! 

78. Kwani yeye amepata khabari za ghaibu, au amechukua ahadi kwa Arrahmani Mwingi wa Rehema? 

79. Hasha! Tutaandika anayo yasema, tutamkunjulia muda wa adhabu. 

80. Na tutamrithi hayo anayo yasema, na atatufikia mtupu peke yake! 

81. Na wamechukua miungu mingine badala ya Mwenyezi Mungu ili ati iwape nguvu. 

82. Sivyo kabisa! Wataikataa hiyo ibada yao, na watakuwa ndio dhidi yao. 

83. Kwani huoni ya kwamba tumewatuma mashet'ani kwa makafiri wawachochee kwa uchochezi? 

84. Basi usiwafanyie haraka. Sisi tunawahisabia idadi ya siku zao. 

85. Siku tutayo wakusanya wachamngu kuwapeleka kwa Arrahmani Mwingi wa Rehema kuwa ni wageni wake. 

86. Na tukawachunga wakhalifu kuwapeleka Jahannamu hali ya kuwa wana kiu. 

87. Hawatakuwa na mamlaka ya uombezi ila wale walio chukua ahadi kwa Arrahmani Mwingi wa Rehema.. 

88. Na wao ati husema kuwa Arrahmani Mwingi wa Rehema ana mwana! 

89. Hakika mmeleta jambo la kuchusha mno! 

90. Zinakaribia mbingu kutatuka kwa hilo, na ardhi kupasuka, na milima kuanguka vipande vipande. 

91. Kwa kudai kwao kuwa Arrahmani Mwingi wa Rehema ana mwana. 

92. Wala hahitajii Arrahmani Mwingi wa Rehema kuwa na mwana. 

93. Hapana yeyote aliomo mbinguni na ardhini ila atafika kwa Arrahmani Mwingi wa Rehema kuwa ni mtumwa wake. 

94. Yeye hakika amewadhibiti na amewahisabu sawa sawa. 

95. Na kila mmoja katika wao atamfikia Siku ya Kiyama peke yake. 

96. Hakika walio amini na wakatenda mema Arrahmani Mwingi wa Rehema atawajaalia mapenzi. 

97. Na hakika tumeifanya nyepesi (Qur'ani) kwa ulimi wako, ili uwabashirie kwayo wachamngu, na uwaonye kwayo watu wabishi. 

98. Na kaumu ngapi tumezihiliki kabla yao. Je! Unawaona hata mmoja katika wao au unasikia hata mchakato wao? 

 

20 - T'AHA

KWA JINA LA MWENYEZI MUNGU MWINGI WA REHEMA MWENYE KUREHEMU. 

 

1. T'AHA! 

2. Hatukukuteremshia Qur'ani ili upate mashaka. 

3. Bali ni mawaidha kwa wenye kunyenyekea. 

4. Materemsho yatokayo kwa aliye umba ardhi na mbingu zilizo juu. 

5. Arrahmani, Mwingi wa Rehema, aliye tawala juu ya Kiti cha Enzi. 

6. Ni vyake vyote viliomo mbinguni na viliomo katika ardhi, na viliomo baina yao, na viliomo chini ya ardhi. 

7. Na ukinyanyua sauti kwa kusema...basi hakika Yeye anajua siri na duni kuliko siri. 

8. Mwenyezi Mungu! Hapana mungu isipo kuwa Yeye. Yeye ana majina mazuri kabisa. 

9. Na je! Imekufikia hadithi ya Musa? 

10. Alipo uona moto, akawaambia watu wake: Ngojeni! Mimi nimeuona moto, huenda nikakuleteeni kijinga kutoka huo moto, au nikapata uongofu kwenye moto. 

11. Basi alipo ufikia akaitwa: Ewe Musa! 

12. Hakika Mimi ndiye Mola wako Mlezi! Basi vua viatu vyako. Kwani upo katika bonde takatifu la T'uwa. 

13. Nami nimekuteua wewe; basi sikiliza unayo funuliwa. 

14. Hakika Mimi ndiye Mwenyezi Mungu. Hapana mungu ila Mimi tu. Basi niabudu Mimi, na ushike Sala kwa ajili ya kunikumbuka Mimi. 

15. Hakika Saa itakuja bila ya shaka. Nimekaribia kuificha, ili kila nafsi ilipwe kwa iliyo yafanya. 

16. Kwa hivyo asikukengeushe nayo yule ambaye haiamini na akafuata pumbao lake ukaja kuhiliki. 

17. Na nini hicho kilichomo mkononi mwako wa kulia, ewe Musa? 

18. Akasema: Hii ni fimbo yangu; naiegemea na ninawaangushia majani kondoo na mbuzi wangu. Tena inanifaa kwa matumizi mengine. 

19. Akasema: Itupe, ewe Musa! 

20. Akaitupa. Mara ikawa nyoka anaye kwenda mbio. 

21. Akasema: Ikamate, wala usiogope! Tutairudisha hali yake ya kwanza. 

22. Na uambatishe mkono wako kwenye ubavu. Utatoka mweupe pasipo kuwa na madhara yoyote. Hiyo ni ishara nyengine. 

23. Ili tukuonyeshe baadhi ya ishara zetu kubwa. 

24. Nenda kwa Firauni; kwani hakika yeye amepindukia mipaka. 

25. (Musa) akasema: Ewe Mola wangu Mlezi! Nikunjulie kifua changu, 

26. Na unifanyie nyepesi kazi yangu, 

27. Na ulifungue fundo lililo katika ulimi wangu, 

28. Wapate kufahamu maneno yangu. 

29. Na nipe waziri katika watu wangu, 

30. Harun, ndugu yangu. 

31. Kwake yeye niongeze nguvu zangu. 

32. Na umshirikishe katika kazi yangu. 

33. Ili tukutakase sana. 

34. Na tukukumbuke sana. 

35. Hakika Wewe unatuona. 

36. Akasema: Hakika Umepewa maombi yako, ewe Musa! 

37. Na hakika tulikwisha kufanyia hisani mara nyengine... 

38. Pale tulipo mfunulia mama yako yaliyo funuliwa, 

39. Ya kuwa mtie katika kisanduku, na kisha kitie mtoni, na mto utamfikisha ufukweni. Atamchukua adui yangu naye ni adui yake. Na nimekutilia mapenzi yanayo tokana kwangu, na ili ulelewe machoni mwangu. 

40. Dada yako alipo kwenda na akasema: Je! Nikujuulisheni mtu wa kuweza kumlea? Basi tukakurejesha kwa mama yako ili macho yake yaburudike, wala asihuzunike. Na ulimuuwa mtu, nasi tukakuokoa katika dhiki, na tukakujaribu kwa majaribio mengi. Ukakaa miaka kwa watu wa Madyana. Kisha ukaja kama ilivyo kadiriwa, ewe Musa! 

41. Na nimekuteuwa kwa ajili ya nafsi yangu. 

42. Nenda, wewe na ndugu yako, pamoja na ishara zangu, wala msichoke kunikumbuka. 

43. Nendeni kwa Firauni. Hakika yeye amepindukia mipaka. 

44. Mwambieni maneno laini, huenda akazingatia au akaogopa. 

45. Wakasema: Ewe Mola wetu Mlezi! Hakika sisi tunaogopa asije akapindukia mipaka juu yetu au kufanya jeuri. 

46. Akasema: Msiogope! Hakika Mimi ni pamoja nanyi. Nasikia na ninaona. 

47. Basi mwendeeni, na mwambieni: Hakika sisi ni Mitume wa Mola wako Mlezi! Basi waache Wana wa Israili watoke nasi, wala usiwaadhibu. Sisi tumekuletea ishara itokayo kwa Mola wako Mlezi. Na amani itakuwa juu ya aliye fuata uwongofu. 

48. Hakika tumefunuliwa sisi kwamba hapana shaka adhabu itamsibu anaye kadhibisha na akapuuza. 

49. (Firauni) akasema: Basi Mola wenu Mlezi ni nani, ewe Musa? 

50. Akasema: Mola wetu Mlezi ni yule aliye kipa kila kitu umbo lake, kisha akakiongoa. 

51. Akasema: Nini hali ya karne za kwanza? 

52. Akasema: Ilimu yake iko kwa Mola wangu Mlezi katika Kitabu. Mola wangu Mlezi hapotei wala hasahau. 

53. Ambaye amekufanyieni ardhi kuwa tandiko, na akakupitishieni humo njia, na akakuteremshieni kutoka mbinguni maji. Na kwa hayo tukatoa namna mbali mbali za mimema. 

54. Kuleni, na mchunge wanyama wenu. Hakika katika hayo zipo ishara kwa wenye akili. 

55. Kutokana nayo (ardhi) tumekuumbeni, na humo tunakurudisheni, na kutoka humo tutakutoeni mara nyengine. 

56. Na hakika tulimwonyesha ishara zetu zote. Lakini alikadhibisha na akakataa. 

57. Akasema: Ewe Musa! Hivyo umetujia kututoa katika nchi yetu kwa uchawi wako? 

58. Basi sisi hakika tutakueletea uchawi kama huo. Basi weka miadi baina yetu na wewe, ambayo tusiivunje sisi wala wewe, mahali patapo kuwa sawa. 

59. Akasema: Miadi yenu ni siku ya Sikukuu; na watu wakusanywe kabla ya adhuhuri. 

60. Basi Firauni akarudi na akatengeneza hila yake, kisha akaja. 

61. Musa akamwambia: Ole wenu! Msimzulie Mwenyezi Mungu uwongo, asije akakufutilieni mbali kwa adhabu. Na mwenye kuzua lazima ashindwe! 

62. Basi wakazozana kwa shauri yao wenyewe kwa wenyewe, na wakanong'ona kwa siri. 

63. Wakasema: Hakika hawa wawili ni wachawi, wanataka kukutoeni katika nchi yenu kwa uchawi wao, na waondoe mila zenu zilizo bora kabisa. 

64. Kwa hivyo kusanyeni hila zenu zote, kisha mfike kwa kujipanga safu, na kwa yakini atafuzu kweli kweli leo atakaye shinda. 

65. Wakasema: Ewe Musa! Je! Utatupa wewe, au tutakuwa sisi wa kwanza kutupa? 

66. Akasema: Bali tupeni nyinyi! Tahamaki kamba zao na fimbo zao zikaonekana mbele yake, kwa uchawi wao, kuwa zinapiga mbio. 

67. Basi Musa akaingia khofu nafsi yake. 

68. Tukasema: Usikhofu! Hakika wewe ndiye utakaye shinda. 

69. Na kitupe kilicho katika mkono wako wa kulia; kitavimeza walivyo viunda. Hakika walivyo unda ni hila za mchawi tu, na mchawi hafanikiwi popote afikapo. 

70. Basi wachawi wakaangushwa wanasujudu. Wakasema: Tumemuamini Mola Mlezi wa Harun na Musa! 

71. (Firauni) akasema: Oh! Mnamuamini kabla sijakupeni ruhusa? Hakika yeye ndiye mkubwa wenu aliye kufundisheni uchawi. Basi kwa yakini nitakukateni mikono yenu na miguu yenu kwa kutafautisha. Na nitakutundikeni misalabani katika vigogo vya mitende, na hapo kwa yakini mtajua ni nani katika sisi aliye mkali wa kuadhibu na kuiendeleza adhabu yake. 

72. Wakasema: Hatutokukhiari wewe kuliko ishara waziwazi zilizo tujia, na kuliko yule aliye tuumba. Basi hukumu utavyo hukumu; kwani wewe unahukumu haya ya maisha ya duniani tu. 

73. Hakika sisi tumemuamini Mola wetu Mlezi ili atusamehe makosa yetu na uchawi ulio tulazimisha kuufanya. Na Mwenyezi Mungu ndiye Mbora na Mwenye kudumu zaidi. 

74. Hakika ataye mjia Mola wake Mlezi naye ni mkhalifu, basi kwa yakini, yake huyo ni Jahannamu. Hafi humo wala haishi. 

75. Na atakaye mjia naye ni Muumini aliye tenda mema, basi hao ndio wenye vyeo vya juu. 

76. Bustani za milele zipitazo mito kati yake, wadumu humo. Na hayo ni malipo ya mwenye kujitakasa. 

77. Na tulimfunulia Musa: Toka usiku na waja wangu, na uwapigie njia kavu baharini. Usikhofu kukamatwa, wala usiogope. 

78. Firauni akawafuata pamoja na majeshi yake. Basi kiliwafudikiza humo baharini kilicho wafudikiza. 

79. Na Firauni aliwapoteza watu wake wala hakuwaongoa. 

80. Enyi Wana wa Israili! Hakika tulikuokoeni na adui yenu, na tukakuahidini upande wa kulia wa mlima. Na tulikuteremshieni Manna na Salwa. 

81. Kuleni katika vitu vizuri hivyo tulivyo kuruzukuni, wala msiruke mipaka katika hayo, isije ikakushukieni ghadhabu yangu. Na inaye mshukia ghadhabu yangu basi huyo ameangamia. 

82. Na hakika Mimi ni Mwingi wa Kusamehe kwa anaye tubia, na akaamini, na akatenda mema, tena akaongoka. 

83. Na nini kilicho kutia haraka ukawaacha watu wako, ewe Musa? 

84. Akasema: Hao wapo nyuma yangu wananifuatia. Na nimefanya haraka kukujia, Mola wangu Mlezi, ili uridhike. 

85. (Mwenyezi Mungu) akasema: Sisi tumewatia mtihani watu wako baada yako, na Msamaria amewapoteza. 

86. Musa akarudi kwa watu wake kwa ghadhabu na kusikitika. Akasema: Enyi watu wangu! Kwani Mola wenu Mlezi hakukuahidini ahadi nzuri? Je, umekuwa muda mrefu kwenu au mmetaka ikushukieni ghadhabu ya Mola wenu Mlezi, ndio maana mkavunja miadi yangu? 

87. Wakasema: Sisi hatukuvunja miadi yako kwa khiari yetu, lakini tulibebeshwa mizigo ya mapambo ya watu, basi tukaitupa. Na hivyo ndivyo alivyo toa shauri Msamaria. 

88. Na akawaundia ndama, kiwiliwili chenye sauti. Na wakasema: Huyu ndiye mungu wenu, na mungu wa Musa, lakini alisahau. 

89. Je! Hawakuona kuwa hakuwarudishia neno, wala hakuweza kuwadhuru wala kuwafaa? 

90. Na hakika Harun alikwisha waambia kabla yake: Enyi watu wangu! Hakika nyinyi mmetiwa mtihanini tu kwa kitu hiki. Na kwa yakini Mola wenu Mlezi ni Arrahmani, Mwingi wa Rehema. Basi nifuateni mimi, na t'iini amri yangu! 

91. Wakasema: Hatutaacha kumuabudu mpaka Musa atapo rejea kwetu. 

92. (Musa) akasema: Ewe Harun! Ni nini kilicho kuzuia, ulipo waona wamepotea, 

93. Hata usinifuate? Je, umeasi amri yangu? 

94. Akasema: Ewe mwana wa mama yangu! Usinishike ndevu zangu, wala kichwa changu. Kwa hakika naliogopa usije sema: Umewafarikisha Wana wa Israil, na hukungojea kauli yangu. 

95. (Musa) akasema: Ewe Msamaria! Unataka nini ? 

96. Akasema: Niliona wasiyo yaona wao, nikashika gao katika unyao wa Mtume. Kisha nikalitupa. Na hivi ndivyo ilivyo nielekeza nafsi yangu. 

97. (Musa) akasema: Basi ondoka! Na kwa yakini utakuwa katika maisha ukisema: Usiniguse. Na hakika una ahadi kwako isiyo vunjwa. Na mtazame huyo mungu wako uliye endelea kumuabudu - Sisi kwa hakika tutamchoma moto, kisha tutamtawanya baharini atawanyike. 

98. Hakika Mungu wenu ni Allah, Mwenyezi Mungu, tu. Hapana Mungu isipo kuwa Yeye. Ujuzi wake umeenea kila kitu. 

99. Namna hivi tunakuhadithia katika khabari za yaliyo tangulia. Na hakika tumekuletea kutoka kwetu mawaidha ya kukumbukwa. 

100. Atakaye jitenga nayo, basi kwa yakini Siku ya Kiyama atabeba mzigo. 

101. Wadumu humo. Na ni mzigo muovu kwao kuubeba Siku ya Kiyama! 

102. Siku litakapo pulizwa barugumu, na tukawakusanya wakhalifu Siku hiyo, hali macho yao ya kibuluu. 

103. Watanong'onezana wao kwa wao: Hamkukaa ila siku kumi tu. 

104. Sisi tunajua zaidi watakayo yasema, atakapo sema mbora wao katika mwendo: Nyinyi hamkukaa ila siku moja tu. 

105. Na wanakuuliza khabari za milima. Waambie: Mola wangu Mlezi ataivuruga vuruga. 

106. Na ataiacha tambarare, uwanda. 

107. Hutaona humo mdidimio wala muinuko. 

108. Siku hiyo watamfuata muitaji asiye na upotofu. Na sauti zote zitamnyenyekea Arrahmani Mwingi wa Rahema. Basi husikii ila mchakato na mnong'ono. 

109. Siku hiyo uombezi haufai kitu, ila wa aliye mruhusu Arrahmani Mwingi wa Rehema na akamridhia kusema. 

110. Yeye anajua yaliyo mbele yao, na yaliyo nyuma yao. Wala wao hawawezi kumjua Yeye vilivyo. 

111. Na zitadhalilika nyuso mbele ya Aliye Hai Milele, Mwangalizi Mkuu. Na atakuwa ameharibikiwa mwenye kubeba dhulma. 

112. Na anaye tenda mema, naye ni Muumini, basi hatakhofu kudhulumiwa wala kupunjwa. 

113. Na namna hivi tumeiteremsha Qur'ani kwa Kiarabu, na tumekariri humo maonyo ili wapate kuogopa na kujilinda na iwaletee makumbusho. 

114. Ametukuka Mwenyezi Mungu, Mfalme wa Haki. Wala usiifanyie haraka hii Qur'ani, kabla haujamalizika ufunuo wake. Na sema: Mola wangu Mlezi! Nizidishie ilimu. 

115. Na hapo zamani tuliagana na Adam, lakini alisahau, wala hatukuona kwake azma kubwa. 

116. Na tulipo waambia Malaika: Msujudieni Adam! Wakasujudu, isipo kuwa Iblisi, alikataa. 

117. Tukasema: Ewe Adam! Hakika huyu ni adui yako na wa mkeo. Basi asikutoeni katika Bustani hii, mkaingia mashakani. 

118. Hakika humo hutakuwa na njaa wala hutakuwa uchi. 

119. Na hakika hutapata kiu humo wala hutapata joto. 

120. Lakini Shet'ani alimtia wasiwasi, akamwambia: Ewe Adam! Nikujuulishe mti wa kuishi milele na ufalme usio koma? 

121. Basi wakaula wote wawili, na uchi wao ukawadhihirikia na wakaanza kujibandika majani ya Bustani. Na Adam akamuasi Mola wake Mlezi, na akapotea njia. 

122. Kisha Mola wake Mlezi akamteuwa, naye akamkubalia toba yake, naye akamwongoa. 

123. Akasema: Ondokeni humu nyote, hali ya kuwa ni maadui nyinyi kwa nyinyi. Na ukikufikieni uwongofu kutoka kwangu basi atakaye ufuata uwongofu wangu, hatapotea wala hatataabika. 

124. Na atakaye jiepusha na mawaidha yangu, basi kwa yakini atapata maisha yenye dhiki, na Siku ya Kiyama tutamfufua hali ya kuwa kipofu. 

125. Aseme: Ewe Mola wangu Mlezi! Mbona umenifufua kipofu, nami nilikuwa nikiona? 

126. (Mwenyezi Mungu) atasema: Ndivyo vivyo hivyo. Zilikufikia ishara zetu, nawe ukazisahau; na kadhaalika leo unasahauliwa. 

127. Na hivi ndivyo tutakavyo mlipa kila apitaye kiasi, na asiye amini ishara za Mola wake Mlezi. Na hakika adhabu ya Akhera ni kali zaidi, na inadumu zaidi. 

128. Je! Haikuwabainikia tu; vizazi vingapi tuliviangamiza kabla yao, nao wanatembea katika maskani zao? Hakika katika hayo zimo ishara kwa wenye akili. 

129. Na lau kuwa si neno lililo kwisha tangulia kutoka kwa Mola wako Mlezi na muda ulio wekwa, bila ya shaka inge fika adhabu (hapa hapa). 

130. Yavumilie haya wayasemayo. Na umtakase Mola wako Mlezi kwa kumsifu kabla ya kuchomoza jua, na kabla halijachwa, na nyakati za usiku pia umtakase, na ncha za mchana ili upate ya kukuridhisha. 

131. Wala usivikodolee macho tulivyo wastareheshea baadhi ya watu miongoni mwao, kwa ajili ya mapambo ya duniani, ili tuwajaribu. Na riziki ya Mola wako Mlezi ni bora na inadumu zaidi. 

132. Na waamrishe watu wako kusali, na uendelee mwenyewe kwa hayo. Sisi hatukuombi wewe riziki, bali Sisi ndio tunakuruzuku. Na mwisho mwema ni kwa mchamngu. 

133. Na walisema: Kwa nini hakutuletea muujiza kutoka kwa Mola wake Mlezi? Je! Haikuwafikilia dalili wazi ya yaliyomo katika Vitabu vya kale? 

134. Na lau kuwa tuliwaangamiza kwa adhabu kabla yake, wangeli sema: Ewe Mola wetu Mlezi! Kwa nini usituletee Mtume tukazifuata ishara zako kabla hatujadhilika na kuhizika. 

135. Sema: Kila mmoja anangoja. Basi ngojeni! Hivi karibuni mtajua nani mwenye njia sawa na nani aliye ongoka.