Part 30

 

78 - ANNABAA

KWA JINA LA MWENYEZI MUNGU MWINGI WA REHEMA MWENYE KUREHEMU. 

 

1. WANAULIZANA nini? 

2. Ile khabari kuu, 

3. Ambayo kwayo wanakhitalifiana. 

4. La! Karibu watakuja jua. 

5. Tena la! Karibu watakuja jua. 

6. Kwani hatukuifanya ardhi kama tandiko? 

7. Na milima kama vigingi? 

8. Na tukakuumbeni kwa jozi? 

9. Na tukakufanya kulala kwenu ni mapumziko? 

10. Na tukaufanya usiku ni nguo? 

11. Na tukaufanya mchana ni wa kuchumia maisha? 

12. Na tukajenga juu yenu saba zenye nguvu? 

13. Na tukaifanya taa yenye mwanga na joto; 

14. Na tukateremsha maji yanayo anguka kwa kasi kutoka mawinguni, 

15. Ili tutoe kwayo nafaka na mimea, 

16. Na mabustani yenye miti iliyo kamatana. 

17. Hakika siku ya uamuzi imewekewa wakati wake, 

18. Siku litapo pulizwa barugumu, nanyi mtakuja kwa makundi, 

19. Na mbingu zitafunguliwa, ziwe milango, 

20. Na milima itaondolewa na itakuwa kama sarabi. 

21. Hakika Jahannamu inangojea! 

22. Kwa walio asi ndio makaazi yao, 

23. Wakae humo karne baada ya karne, 

24. Hawataonja humo chochote kibaridi wala kinywaji, 

25. Ila maji yamoto sana na usaha, 

26. Ndio jaza muwafaka. 

27. Hakika hao hawakuwa wakitaraji kuwa kuna hisabu. 

28. Na wakikanusha Aya zetu kwa nguvu. 

29. Na kila kitu Sisi tumekidhibiti kwa kukiandika. 

30. Basi onjeni! Nasi hatutakuzidishieni ila adhabu! 

31. Hakika wachamngu wanastahiki kufuzu, 

32. Mabustani na mizabibu, 

33. Na wake walio lingana nao, 

34. Na bilauri zilizo jaa, 

35. Hawatasikia humo upuuzi wala uwongo - 

36. Malipo kutoka kwa Mola wako Mlezi, kipawa cha kutosha. 

37. Mola Mlezi wa mbingu na ardhi na vilio baina yao, Arrahman, Mwingi wa rehema; hawamiliki usemi mbele yake! 

38. Siku atakapo simama Roho na Malaika kwa safu. Hawatasema ila Mwingi wa rehema aliye mruhusu, na atasema yaliyo sawa tu. 

39. Hiyo ndiyo Siku ya haki. Basi anaye taka na ashike njia arejee kwa Mola wake Mlezi. 

40. Hakika tumekuhadharisheni adhabu iliyo karibu kufika; Siku ambayo mtu atakapo ona yaliyo tangulizwa na mikono yake; na kafiri atasema: Laiti ningeli kuwa udongo! 

 

79 - ANNAZIA'AT

KWA JINA LA MWENYEZI MUNGU MWINGI WA REHEMA MWENYE KUREHEMU. 

 

1. Naapa kwa wanao komoa kwa nguvu, 

2. Na kwa wanao toa kwa upole, 

3. Na wanao ogelea, 

4. Wakishindana mbio, 

5. Wakidabiri mambo. 

6. Siku kitapo tetemeka cha kutetemeka, 

7. Kifuate cha kufuatia. 

8. Siku hiyo nyoyo zitapiga piga, 

9. Macho yatainama chini. 

10. Sasa wanasema: Ati kweli tutarudishwa kwenye hali ya kwanza? 

11. Hata tukiwa mifupa iliyo bunguliwa? 

12. Wanasema: Basi marejeo hayo ni yenye khasara! 

13. Kwa hakika hayo ni ukelele mmoja tu, 

14. Mara watakuwa kwenye uwanda wa mkutano! 

15. Je! Imekufikia hadithi ya Musa? 

16. Mola wake Mlezi alipo mwita katika bonde takatifu la T'uwaa, akamwambia: 

17. Nenda kwa Firauni. Hakika yeye amezidi jeuri. 

18. Umwambie: Je! Unapenda kujitakasa? 

19. Nami nitakuongoa ufike kwa Mola wako Mlezi, upate kumcha. 

20. Basi alimwonyesha Ishara kubwa. 

21. Lakini aliikadhibisha na akaasi. 

22. Kisha alirudi nyuma, akaingia kufanya juhudi. 

23. Akakusanya watu akanadi. 

24. Akasema: Mimi ndiye Mola wenu Mlezi mkuu kabisa. 

25. Basi hapo Mwenyezi Mungu akamshika kumuadhibu kwa la mwisho na la mwanzo. 

26. Kwa hakika katika haya yapo mazingatio kwa wanao ogopa. 

27. Je! Ni vigumu zaidi kukuumbeni nyinyi au mbingu? Yeye ndiye aliye ijenga! 

28. Akainua kimo chake, na akaitengeneza vizuri. 

29. Na akautia giza usiku wake, na akautokeza mchana wake. 

30. Na juu ya hivyo ameitandaza ardhi. 

31. Akatoa ndani yake maji yake na malisho yake, 

32. Na milima akaisimamisha, 

33. Kwa nafuu yenu na mifugo yenu. 

34. Basi itakapo fika hiyo balaa kubwa, 

35. Siku ambayo mtu atakumbuka aliyo yafanya, 

36. Na Jahannamu itadhihirishwa kwa mwenye kuona, 

37. Basi ama yule aliye zidi ujeuri, 

38. Na akakhiari maisha ya dunia, 

39. Kwa hakika Jahannamu ndiyo makaazi yake! 

40. Na ama yule anaye ogopa kusimamishwa mbele ya Mola wake Mlezi, na akajizuilia nafsi yake na matamanio, 

41. Basi huyo, Pepo itakuwa ndiyo makaazi yake! 

42. Wanakuuliza Saa (ya Kiyama) itakuwa lini? 

43. Una nini wewe hata uitaje? 

44. Kwa Mola wako Mlezi ndio mwisho wake. 

45. Kwa hakika wewe ni mwonyaji tu kwa mwenye kuikhofu. 

46. Ni kama kwamba wao siku watapo iona (hiyo Saa) hawakukaa ila jioni moja tu, au mchana wake. 

 

80 - A'BASA

KWA JINA LA MWENYEZI MUNGU MWINGI WA REHEMA MWENYE KUREHEMU. 

 

1. Alikunja kipaji na akageuka, 

2. Kwa sababu alimjia kipofu! 

3. Na nini kitakujuulisha pengine yeye atatakasika? 

4. Au atawaidhika, na mawaidha yamfae? 

5. Ama ajionaye hana haja, 

6. Wewe ndio unamshughulikia? 

7. Na si juu yako kama hakutakasika.  

8. Ama anaye kujia kwa juhudi, 

9. Naye anaogopa, 

10. Ndio wewe unampuuza? 

11. Sivyo hivyo! Huku ni kukumbushana. 

12. Basi anaye penda akumbuke. 

13. Yamo katika kurasa zilizo hishimiwa, 

14. Zilizo inuliwa, zilizo takaswa. 

15. Zimo mikononi mwa Malaika waandishi, 

16. Watukufu, wema. 

17. Ameangamia mwanaadamu! Nini kinacho mkufurisha? 

18. Kwa kitu gani amemuumba? 

19. Kwa tone la manii, akamuumba na akamkadiria. 

20. Kisha akamsahilishia njia. 

21. Kisha akamfisha, akamtia kaburini. 

22. Kisha apendapo atamfufua. 

23. La! Hajamaliza aliyo muamuru. 

24. Hebu mtu na atazame chakula chake. 

25. Hakika Sisi tumemimina maji kwa nguvu, 

26. Tena tukaipasua pasua ardhi kwa nguvu, 

27. Kisha tukaotesha humo nafaka, 

28. Na zabibu, na mimea ya majani, 

29. Na mizaituni, na mitende, 

30. Na bustani zenye miti iliyo songana baraabara, 

31. Na matunda, na malisho ya wanyama; 

32. Kwa manufaa yenu na mifugo yenu. 

33. Basi utakapo kuja ukelele, 

34. Siku ambayo mtu atamkimbia nduguye, 

35. Na mamaye na babaye, 

36. Na mkewe na wanawe - 

37. Kila mtu miongoni mwao siku hiyo atakuwa na lake la kumtosha. 

38. Siku hiyo ziko nyuso zitazo nawiri, 

39. Zitacheka, zitachangamka; 

40. Na nyuso siku hiyo zitakuwa na mavumbi, 

41. Giza totoro litazifunika, 

42. Hao ndio makafiri watenda maovu. 

 

81 - ATTAKWIR

KWA JINA LA MWENYEZI MUNGU MWINGI WA REHEMA MWENYE KUREHEMU. 

 

1. Jua litakapo kunjwa, s 

2. Na nyota zikazimwa, 

3. Na milima ikaondolewa, 

4. Na ngamia wenye mimba pevu watakapo achwa wasishughulikiwe, 

5. Na wanyama wa mwituni wakakusanywa, 

6. Na bahari zikawaka moto, 

7. Na nafsi zikaunganishwa, 

8. Na msichana aliye zikwa hai atapo ulizwa, 

9. Kwa kosa gani aliuliwa? 

10. Na madaftari yatakapo enezwa, 

11. Na mbingu itapo tanduliwa, 

12. Na Jahannamu itapo chochewa, 

13. Na Pepo ikasogezwa, 

14. Kila nafsi itajua ilicho kihudhurisha. 

15. Naapa kwa nyota zinapo rejea nyuma, 

16. Zinazo kwenda, kisha zikajificha, 

17. Na kwa usiku unapo pungua, 

18. Na kwa asubuhi inapo pambazuka, 

19. Kwamba hakika bila ya shaka hii ni kauli ya Mjumbe mtukufu, 

20. Mwenye nguvu na mwenye cheo kwa huyo Mwenye Kiti cha Enzi, 

21. Anaye t'iiwa, tena muaminifu. 

22. Na wala huyu mwenzenu hana wazimu. 

23. Na hakika yeye alimwona kwenye upeo wa macho ulio safi. 

24. Wala yeye si bakhili kwa mambo ya ghaibu. 

25. Wala hii si kauli ya Shetani maluuni. 

26. Basi mnakwenda wapi? 

27. Haikuwa hii ila ni ukumbusho kwa walimwengu wote. 

28. Kwa yule miongoni mwenu anaye taka kwenda sawa. 

29. Wala nyinyi hamtataka isipo kuwa atake Mwenyezi Mungu Mola Mlezi wa walimwengu wote. 

 

82 - AL - INFIT'AAR

KWA JINA LA MWENYEZI MUNGU MWINGI WA REHEMA MWENYE KUREHEMU. 

 

1. Mbingu itapo chanika, 

2. Na nyota zitapo tawanyika, 

3. Na bahari zitakapo pasuliwa, 

4. Na makaburi yatapo fukuliwa, 

5. Hapo kila nafsi itajua ilicho tanguliza, na ilicho bakisha nyuma. 

6. Ewe mwanaadamu! Nini kilicho kughuri ukamwacha Mola wako Mlezi Mtukufu? 

7. Aliye kuumba, akakuweka sawa, akakunyoosha, 

8. Katika sura yoyote aliyo ipenda akakujenga. 

9. Sivyo hivyo! Bali nyinyi mnaikanusha Siku ya Malipo. 

10. Na hakika bila ya shaka wapo walinzi juu yenu, 

11. Waandishi wenye hishima, 

12. Wanayajua mnayo yatenda. 

13. Hakika wema bila ya shaka watakuwa katika neema, 

14. Na hakika waovu bila ya shaka watakuwa Motoni; 

15. Wataingia humo Siku ya Malipo. 

16. Na hawatoacha kuwamo humo. 

17. Na nini kitakacho kujuulisha Siku ya Malipo ni siku gani? 

18. Tena nini kitakacho kujuulisha Siku ya Malipo ni siku gani? 

19. Siku ambayo nafsi haitakuwa na madaraka yoyote juu ya nafsi; na amri yote siku hiyo ni ya Mwenyezi Mungu tu.

 

83 - AL - MUT'AFFIFIIN

KWA JINA LA MWENYEZI MUNGU MWINGI WA REHEMA MWENYE KUREHEMU. 

 

1. Ole wao hao wapunjao! 

2. Ambao wanapo jipimia kwa watu hudai watimiziwe. 

3. Na wao wanapo wapimia watu kwa kipimo au mizani hupunguza. 

4. Kwani hawadhani hao kwamba watafufuliwa 

5. Katika Siku iliyo kuu, 

6. Siku watapo msimamia watu Mola Mlezi wa walimwengu wote? 

7. Hasha! Hakika maandiko ya wakosefu bila ya shaka yamo katika Sijjin. 

8. Unajua nini Sijjin? 

9. Kitabu kilicho andikwa. 

10. Ole wao siku hiyo kwa wanao kadhibisha! 

11. Ambao wanaikadhibisha Siku ya Malipo. 

12. Wala haikadhibishi ila kila mwenye kuruka mipaka, mwenye dhambi. 

13. Anapo somewa Aya zetu husema: Ni visa vya watu wa kale! 

14. Hasha! Bali yametia kutu juu ya nyoyo zao hao walio kuwa wakiyachuma. 

15. Hasha! Hakika hao siku hiyo bila ya shaka watazuiliwa na neema za Mola wao Mlezi. 

16. Kisha wataingia Motoni! 

17. Kisha waambiwe: Haya ndiyo mliyo kuwa mkiyakadhabisha. 

18. Hasha! Hakika maandiko ya watu wema bila ya shaka yamo katika I'liyyin. 

19. Na nini kitakacho kujuvya nini I'liyyin? 

20. Kitabu kilicho andikwa. 

21. Wanakishuhudia walio karibishwa. 

22. Hakika watu wema bila ya shaka watakuwa katika neema. 

23. Wakae juu ya viti vya enzi wakiangalia. 

24. Utatambua katika nyuso zao mng'aro wa neema, 

25. Watanyweshwa kinywaji safi kiliyo tiwa muhuri, 

26. Muhuri wake ni miski. Na katika hayo washindanie wenye kushindana. 

27. Na mchanganyiko wake ni Tasniim, 

28. Chemchem watakayo inywa walio kurubishwa. 

29. Kwa hakika wale walio kuwa wakosefu walikuwa wakiwacheka walio amini. 

30. Na wanapo pita karibu yao wakikonyezana. 

31. Na wanapo rudi kwa watu wao hurudi nao wamefurahi. 

32. Na wanapo waona husema: Hakika hawa ndio khasa walio potea. 

33. Na wao hawakutumwa wawe walinzi juu yao. 

34. Basi leo walio amini ndio watawacheka makafiri, 

35. Nao wako juu ya viti vya enzi wakiangalia. 

36. Je! makafiri wamelipwa malipo ya yale waliyo kuwa wakiyatenda? 

 

84 - AL - INSHIQAAQ

KWA JINA LA MWENYEZI MUNGU MWINGI WA REHEMA MWENYE KUREHEMU. 

 

1. Itapo chanika mbingu, 

2. Na ikamsikiliza Mola wake Mlezi, na ikapasiwa kumsikiliza, 

3. Na ardhi itakapo tanuliwa, 

4. Na kuvitoa vilivyo kuwa ndani yake, ikawa tupu, 

5. Na ikamsikiliza Mola wake Mlezi, na ikapasiwa kumsikiliza, 

6. Ewe mtu! Hakika wewe unajikusuru kwa juhudi kumwendea Mola wako Mlezi, basi utamkuta. 

7. Ama atakaye pewa daftari lake kwa mkono wa kulia, 

8. Basi huyo atahisabiwa hisabu nyepesi, 

9. Na arudi kwa ahali zake na furaha. 

10. Na ama atakaye pewa daftari lake kwa nyuma ya mgongo wake, 

11. Basi huyo ataomba kuteketea. 

12. Na ataingia Motoni. 

13. Hakika alikuwa furahani kati ya jamaa zake. 

14. Huyo hakika alidhani kuwa hatarejea tena. 

15. Kwani? Hakika Mola wake Mlezi alikuwa akimwona! 

16. Basi ninaapa kwa wekundu wa jua linapo kuchwa, 

17. Na kwa usiku na unavyo vikusanya, 

18. Na kwa mwezi unapo pevuka, 

19. Lazima mtapanda t'abaka kwa t'abaka! 

20. Basi wana nini hawaamini? 

21. Na wanapo somewa Qur'ani hawasujudu? 

22. Bali walio kufuru wanakanusha tu. 

23. Na Mwenyezi Mungu anajua wanayo yadhamiria. 

24. Basi wabashirie adhabu chungu! 

25. Isipo kuwa wale walio amini na wakatenda mema; hao watakuwa na ujira usio malizika. 

 

85 - AL - BURUUJ

KWA JINA LA MWENYEZI MUNGU MWINGI WA REHEMA MWENYE KUREHEMU. 

 

1. Naapa kwa mbingu yenye Buruji! 

2. Na kwa siku iliyo ahidiwa! 

3. Na kwa shahidi na kinacho shuhudiwa! 

4. Wameangamizwa watu wa makhandaki 

5. Yenye moto wenye kuni nyingi, 

6. Walipo kuwa wamekaa hapo, 

7. Na wao ni mashahidi wa yale waliyo kuwa wakiwafanyia Waumini. 

8. Nao hawakuona baya lolote kwao ila kuwa wakimuamini Mwenyezi Mungu, Mwenye nguvu, Msifiwa, 

9. Ambaye anao ufalme wa mbingu na ardhi; na Mwenyezi Mungu ni shaahidi wa kila kitu. 

10. Hakika walio wafitini Waumini wanaume na Waumini wanawake, kisha hawakutubu, basi watapata adhabu ya Jahannamu na watapata adhabu ya kuungua. 

11. Hakika walio amini na wakatenda mema watapata Bustani zenye mito ipitayo kati yake. Huko ndiko kufuzu kukubwa. 

12. Hakika kutesa kwa Mola wako Mlezi ni kukali. 

13. Yeye ndiye anaye anzisha na ndiye anaye rejeza tena, 

14. Naye ni Mwenye kusamehe, Mwenye mapenzi, 

15. Mwenye Kiti cha Enzi, Mtukufu, 

16. Atendaye ayatakayo. 

17. Je! Zimekuwasilia khabari za majeshi? 

18. Ya Firauni na Thamudi? 

19. Lakini walio kufuru wamo katika kukadhibisha. 

20. Na Mwenyezi Mungu nyuma yao amewazunguka. 

21. Bali hii ni Qur'ani tukufu 

22. Katika Ubao Ulio Hifadhiwa. 

 

86 - ATT'AARIQ

KWA JINA LA MWENYEZI MUNGU MWINGI WA REHEMA MWENYE KUREHEMU. 

 

1. Naapa kwa mbingu na Kinacho kuja usiku! 

2. Na nini kitakacho kujuulisha ni nini hicho Kinacho kuja usiku? 

3. Ni Nyota yenye mwanga mkali. 

4. Hapana nafsi ila inayo mwangalizi. 

5. Hebu naajitazame mwanaadamu ameumbwa kwa kitu gani? 

6. Ameumbwa kwa maji yatokayo kwa kuchupa, 

7. Yatokayo baina ya mifupa ya mgongo na mbavu. 

8. Hakika Yeye ana uweza wa kumrudisha. 

9. Siku zitakapo dhihirishwa siri. 

10. Basi hatakuwa na nguvu wala msaidizi. 

11. Naapa kwa mbingu yenye marejeo! 

12. Na kwa ardhi inayo pasuka! 

13. Hakika hii ni kauli ya kupambanua. 

14. Wala si mzaha. 

15. Hakika wao wanapanga mpango. 

16. Na Mimi napanga mpango. 

17. Basi wape muhula makafiri - wape muhula pole pole. 

 

87 - AL - AA'LAA

KWA JINA LA MWENYEZI MUNGU MWINGI WA REHEMA MWENYE KUREHEMU. 

 

1. Litakase jina la Mola wako Mlezi aliye juu kabisa, 

2. Aliye umba, na akaweka sawa, 

3. Na ambaye amekadiria na akaongoa, 

4. Na aliye otesha malisho, 

5. Kisha akayafanya makavu, meusi. 

6. Tutakusomesha wala hutasahau, 

7. Ila akipenda Mwenyezi Mungu. Hakika Yeye anayajua yaliyo dhaahiri na yaliyo fichikana. 

8. Na tutakusahilishia yawe mepesi. 

9. Basi kumbusha, kama kukumbusha kunafaa. 

10. Atakumbuka mwenye kuogopa. 

11. Na atajitenga mbali nayo mpotovu, 

12. Ambaye atauingia Moto mkubwa. 

13. Tena humo hatakufa wala hawi hai. 

14. Hakika amekwisha fanikiwa aliye jitakasa. 

15. Na akakumbuka jina la Mola wake Mlezi, na akasali. 

16. Lakini nyinyi mnakhiari maisha ya dunia! 

17. Na Akhera ni bora na yenye kudumu zaidi. 

18. Hakika haya yamo katika Vitabu vya mwanzo, 

19. Vitabu vya Ibrahimu na Musa. 

 

88 - AL - GHAASHIYAH

KWA JINA LA MWENYEZI MUNGU MWINGI WA REHEMA MWENYE KUREHEMU. 

 

1. Je! Imekufikia khabari ya msiba wa kufudikiza? 

2. Siku hiyo nyuso zitainama, 

3. Zikifanya kazi, nazo taabani. 

4. Ziingie katika Moto unao waka - 

5. Zikinyweshwa kutoka chemchem inayo chemka. 

6. Hawatakuwa na chakula isipo kuwa kichungu chenye miba. 

7. Hakinenepeshi wala hakiondoi njaa. 

8. Siku hiyo nyuso nyengine zitakuwa kunjufu. 

9. Zitakuwa radhi kwa juhudi yao, 

10. Katika Bustani ya juu. 

11. Hawatasikia humo upuuzi. 

12. Humo imo chemchem inayo miminika. 

13. Humo vimo viti vilivyo nyanyuliwa, 

14. Na bilauri zilizo pangwa, 

15. Na matakia safu safu, 

16. Na mazulia yaliyo tandikwa. 

17. Je! Hawamtazami ngamia jinsi alivyo umbwa? 

18. Na mbingu jinsi ilivyo inuliwa? 

19. Na milima jinsi ilivyo thibitishwa? 

20. Na ardhi jinsi ilivyo tandazwa? 

21. Basi kumbusha! Hakika wewe ni Mkumbushaji. 

22. Wewe si mwenye kuwatawalia. 

23. Lakini anaye rudi nyuma na kukataa, 

24. Basi Mwenyezi Mungu atamuadhibu kwa adhabu iliyo kubwa kabisa! 

25. Hakika ni kwetu Sisi ndio marejeo yao. 

26. Kisha hakika ni juu yetu Sisi hisabu yao! 

 

89 - AL - FAJR

KWA JINA LA MWENYEZI MUNGU MWINGI WA REHEMA MWENYE KUREHEMU. 

 

1. Naapa kwa alfajiri, 

2. Na kwa masiku kumi, 

3. Na kwa viwili viwili na kimoja kimoja, 

4. Na kwa usiku unapo pita, 

5. Je! Hapana katika haya kiapo kwa mwenye akili? 

6. Kwani hukuona jinsi Mola wako Mlezi alivyo wafanya kina A'di? 

7. Wa Iram, wenye majumba marefu? 

8. Ambao haukuumbwa mfano wake katika nchi? 

9. Na Thamudi walio chonga majabali huko bondeni? 

10. Na Firauni mwenye vigingi? 

11. Ambao walifanya jeuri katika nchi? 

12. Wakakithirisha humo ufisadi? 

13. Basi Mola wako Mlezi aliwapiga mjeledi wa adhabu. 

14. Hakika Mola wako Mlezi yupo kwenye mavizio anawavizia. 

15. Ama mtu anapo jaribiwa na Mola wake Mlezi, akamkirimu na akamneemesha, husema: Mola wangu Mlezi amenikirimu! 

16. Na ama anapo mjaribu akampunguzia riziki yake, husema: Mola wangu Mlezi amenitia unyonge! 

17. Sivyo hivyo! Bali nyinyi hamuwakirimu mayatima, 

18. Wala hamhimizani kulisha masikini; 

19. Na mnakula urithi kwa ulaji wa pupa, 

20. Na mnapenda mali pendo la kupita kiasi. 

21. Sivyo hivyo! Itakapo vunjwa ardhi vipande vipande, 

22. Na akaja Mola wako Mlezi na Malaika safu safu, 

23. Na ikaletwa Jahannamu siku hiyo, siku hiyo mtu atakumbuka! Lakini kukumbuka huko kutamfaa nini? 

24. Atasema: Laiti ningeli jitangulizia kwa uhai wangu! 

25. Basi siku hiyo hataadhibu yeyote namna ya kuadhibu kwake. 

26. Wala hatafunga yeyote kama kufunga kwake. 

27. Ewe nafsi iliyo tua! 

28. Rejea kwa Mola wako Mlezi umeridhika, na umemridhisha. 

29. Basi ingia miongoni mwa waja wangu, 

30. Na ingia katika Pepo yangu. 

 

90 - AL - BALAD

KWA JINA LA MWENYEZI MUNGU MWINGI WA REHEMA MWENYE KUREHEMU. 

 

1. Naapa kwa Mji huu! 

2. Nawe unaukaa Mji huu. 

3. Na naapa kwa mzazi na alicho kizaa. 

4. Hakika tumemuumba mtu katika taabu. 

5. Ati anadhani hapana yeyote ataye muweza? 

6. Anasema: Nimeteketeza chungu ya mali. 

7. Ati anadhani ya kuwa hapana yeyote anaye mwona? 

8. Kwani hatukumpa macho mawili? 

9. Na ulimi, na midomo miwili? 

10. Na tukambainishia zote njia mbili? 

11. Lakini hakujitoma kwenye njia ya vikwazo vya milimani. 

12. Na nini kitakujuvya ni nini njia ya vikwazo vya milimani? 

13. Kumkomboa mtumwa; 

14. Au kumlisha siku ya njaa 

15. Yatima aliye jamaa, 

16. Au masikini aliye vumbini. 

17. Tena awe miongoni mwa walio amini na wakausiana kusubiri na wakausiana kuhurumiana. 

18. Hao ndio watu wa kheri wa kuliani. 

19. Lakini walio zikataa Ishara zetu, hao ndio watu wa shari wa kushotoni. 

20. Juu yao utakuwa Moto ulio fungiwa kila upande. 

 

91 - ASH-SHAMS

KWA JINA LA MWENYEZI MUNGU MWINGI WA REHEMA MWENYE KUREHEMU. 

 

1. Naapa kwa jua na mwangaza wake! 

2. Na kwa mwezi unapo lifuatia! 

3. Na kwa mchana unapo lidhihirisha! 

4. Na kwa usiku unapo lifunika! 

5. Na kwa mbingu na kwa aliye ijenga! 

6. Na kwa ardhi na kwa aliye itandaza! 

7. Na kwa nafsi na kwa aliye itengeneza! 

8. Kisha akaifahamisha uovu wake na wema wake, 

9. Hakika amefanikiwa aliye itakasa, 

10. Na hakika amekhasiri aliye iviza. 

11. Kina Thamudi walikadhibisha kwa sababu ya upotofu wao, 

12. Alipo simama mwovu wao mkubwa, 

13. Hapo Mtume wa Mwenyezi Mungu alipo waambia: Huyu ni ngamia wa Mwenyezi Mungu, mwacheni anywe maji fungu lake. 

14. Lakini walimkadhibisha na wakamchinja ngamia, kwa hivyo Mola wao Mlezi aliwaangamiza kwa sababu ya dhambi zao na akawafuta kabisa. 

15. Wala Yeye haogopi matokeo yake. 

 

92 - AL - LAYL

KWA JINA LA MWENYEZI MUNGU MWINGI WA REHEMA MWENYE KUREHEMU. 

 

1. Naapa kwa usiku unapo funika! 

2. Na mchana unapo dhihiri! 

3. Na kwa Aliye umba dume na jike! 

4. Hakika juhudi zenu bila ya shaka ni mbali mbali. 

5. Ama mwenye kutoa na akamchamngu, 

6. Na akaliwafiki lilio jema, 

7. Tutamsahilishia yawe mepesi. 

8. Na ama mwenye kufanya ubakhili, na asiwe na haja ya wenzake, 

9. Na akakanusha lilio jema, 

10. Tutamsahilishia yawe mazito! 

11. Na mali yake yatamfaa nini atapo kuwa anadidimia? 

12. Hakika ni juu yetu kuonyesha uwongofu. 

13. Na hakika ni yetu Sisi Akhera na dunia. 

14. Basi nakuonyeni na Moto unao waka! 

15. Hatauingia ila mwovu kabisa! 

16. Anaye kadhibisha na kupa mgongo. 

17. Na mchamngu ataepushwa nao, 

18. Ambaye hutoa mali yake kwa ajili ya kujitakasa. 

19. Na wala si kwa kuwa yupo yeyote aliye mfanyia hisani ndio anamlipa. 

20. Ila ni kutaka radhi ya Mola wake Mlezi aliye juu kabisa. 

21. Naye atakuja ridhika! 

 

93 - WADH-DHUH'AA

KWA JINA LA MWENYEZI MUNGU MWINGI WA REHEMA MWENYE KUREHEMU. 

 

1. Naapa kwa mchana! 

2. Na kwa usiku unapo tanda! 

3. Mola wako Mlezi hakukuacha, wala hakukasirika nawe. 

4. Na bila ya shaka wakati ujao utakuwa bora kwako kuliko ulio tangulia. 

5. Na Mola wako Mlezi atakupa mpaka uridhike. 

6. Kwani hakukukuta yatima akakupa makaazi? 

7. Na akakukuta umepotea akakuongoa? 

8. Akakukuta mhitaji akakutosheleza? 

9. Basi yatima usimwonee! 

10. Na anaye omba au kuuliza usimkaripie! 

11. Na neema za Mola wako Mlezi zisimlie. 

 

94 - ASH-SHARH'

KWA JINA LA MWENYEZI MUNGU MWINGI WA REHEMA MWENYE KUREHEMU. 

 

1. Hatukukunjulia kifua chako? 

2. Na tukakuondolea mzigo wako, 

3. Ulio vunja mgongo wako? 

4. Na tukakunyanyulia utajo wako? 

5. Basi kwa hakika pamoja na uzito upo wepesi, 

6. Hakika pamoja na uzito upo wepesi. 

7. Na ukipata faragha, fanya juhudi. 

8. Na Mola wako Mlezi ndio mshughulikie. 

 

95 - AT-TIN

KWA JINA LA MWENYEZI MUNGU MWINGI WA REHEMA MWENYE KUREHEMU. 

 

1. Naapa kwa tini na zaituni! 

2. Na kwa Mlima wa Sinai! 

3. Na kwa mji huu wenye amani! 

4. Bila ya shaka tumemuumba mtu kwa umbo lilio bora kabisa. 

5. Kisha tukamrudisha kuwa chini kuliko walio chini! 

6. Lakini wale walio amini na wakatenda mema, hao watapata ujira usio kwisha. 

7. Basi ni kipi baadaye kitacho kukukadhibishia malipo? 

8. Kwani Mwenyezi Mungu si muadilifu kuliko mahakimu wote? 

 

96 - AL - A'LAQ

KWA JINA LA MWENYEZI MUNGU MWINGI WA REHEMA MWENYE KUREHEMU. 

 

1. Soma kwa jina la Mola wako Mlezi aliye umba, 

2. Amemuumba binaadamu kwa tone la damu, 

3. Soma! Na Mola wako Mlezi ni Karimu kushinda wote! 

4. Ambaye amefundisha kwa kalamu. 

5. Kamfundisha mtu aliyo kuwa hayajui. 

6. Kwani! Hakika mtu bila ya shaka huwa jeuri 

7. Akijiona katajirika. 

8. Hakika kwa Mola wako Mlezi ndio marejeo. 

9. Umemwona yule anaye mkataza 

10. Mja anapo sali? 

11. Umeona kama yeye yuko juu ya uwongofu? 

12. Au anaamrisha uchamngu? 

13. Umeona kama yeye akikanusha na anarudi nyuma? 

14. Hajui ya kwamba Mwenyezi Mungu anaona? 

15. Kwani! Kama haachi, tutamkokota kwa shungi la nywele! 

16. Shungi la uwongo, lenye makosa! 

17. Basi na awaite wenzake! 

18. Nasi tutawaita Mazabania! 

19. Hasha! Usimt'ii! Nawe sujudu na ujongee! 

 

97 - AL - QADR

KWA JINA LA MWENYEZI MUNGU MWINGI WA REHEMA MWENYE KUREHEMU. 

 

1. Hakika Sisi tumeiteremsha Qur'ani katika Laylatul Qadri, Usiku wa Cheo Kitukufu. 

2. Na nini kitacho kujuulisha nini Laylatul Qadri? 

3. Laylatul Qadri ni bora kuliko miezi elfu. 

4. Huteremka Malaika na Roho katika usiku huo kwa idhini ya Mola wao Mlezi kwa kila jambo. 

5. Amani usiku huo mpaka mapambazuko ya alfajiri. 

 

98 - AL - BAYYINAH

KWA JINA LA MWENYEZI MUNGU MWINGI WA REHEMA MWENYE KUREHEMU. 

 

1. Hawakuwa walio kufuru miongoni mwa Watu wa Kitabu na washirikina waache walio nayo mpaka iwajie bayana, 

2. Yaani Mtume aliye toka kwa Mwenyezi Mungu anaye wasomea kurasa zilizo takasika, 

3. Ndani yake mna maandiko yaliyo nyooka. 

4. Wala hawakufarikiana walio pewa Kitabu ila baada ya kuwajia hiyo bayana. 

5. Nao hawakuamrishwa kitu ila wamuabudu Mwenyezi Mungu kwa kumtakasia Dini, wawe waongofu, na washike Sala, na watoe Zaka. Na hiyo ndiyo Dini madhubuti. 

6. Hakika walio kufuru miongoni mwa Watu wa Kitabu na washirikina wataingia katika Moto wa Jahannamu wadumu milele humo. Hao ndio viumbe waovu kabisa. 

7. Hakika walio amini na wakatenda mema, hao ndio bora wa viumbe. 

8. Malipo yao kwa Mola wao Mlezi ni Bustani za daima, zipitazo mito kati yake. Wakae humo milele. Mwenyezi Mungu yu radhi nao, na wao waradhi naye. Hayo ni kwa anaye mwogopa Mola wake Mlezi. 

 

99 - AZ-ZILZALAH

KWA JINA LA MWENYEZI MUNGU MWINGI WA REHEMA MWENYE KUREHEMU. 

 

1. Itakapo tetemeshwa ardhi kwa mtetemeko wake! 

2. Na itakapo toa ardhi mizigo yake! 

3. Na mtu akasema: Ina nini? 

4. Siku hiyo itahadithia khabari zake. 

5. Kwa sababu Mola wake Mlezi ameifunulia! 

6. Siku hiyo watu watatoka kwa mfarakano wakaonyweshwe vitendo vyao! 

7. Basi anaye tenda chembe ya wema, atauona! 

8. Na anaye tenda chembe ya uovu atauona! 

 

100 - AL - A'ADIYAAT

KWA JINA LA MWENYEZI MUNGU MWINGI WA REHEMA MWENYE KUREHEMU. 

 

1. Naapa kwa farasi wendao mbio wakipumua, 

2. Na wakitoa moto kwa kupiga kwato zao chini, 

3. Wakishambulia wakati wa asubuhi, 

4. Huku wakitimua vumbi, 

5. Na wakijitoma kati ya kundi, 

6. Hakika mwanaadamu ni mtovu wa fadhila kwa Mola wake Mlezi! 

7. Na hakika yeye mwenyewe bila ya shaka ni shahidi wa hayo! 

8. Naye hakika bila ya shaka ana nguvu za kupenda mali! 

9. Kwani hajui watakapo fufuliwa waliomo makaburini? 

10. Na yakakusanywa yaliomo vifuani? 

11. Kuwa hakika Mola wao Mlezi siku hiyo bila ya shaka atakuwa na khabari zao wote! 

 

101 - AL - QAARIA'H

KWA JINA LA MWENYEZI MUNGU MWINGI WA REHEMA MWENYE KUREHEMU. 

 

1. Inayo gonga! 

2. Nini Inayo gonga? 

3. Na nini kitacho kujuilisha nini Inayo gonga? 

4. Siku ambayo watu watakuwa kama nondo walio tawanyika; 

5. Na milima itakuwa kama sufi zilizo chambuliwa! 

6. Basi yule ambaye mizani yake itakuwa nzito, 

7. Huyo atakuwa katika maisha ya kupendeza. 

8. Na yule ambaye mizani yake itakuwa khafifu, 

9. Huyo maskani yake yatakuwa Moto wa Hawiya! 

10. Na nini kitacho kujuilisha nini hiyo? 

11. Ni Moto mkali! 

 

102 - AT-TAKAATHUR

KWA JINA LA MWENYEZI MUNGU MWINGI WA REHEMA MWENYE KUREHEMU. 

 

1. Kumekushughulisheni kutafuta wingi, 

2. Mpaka mje makaburini! 

3. Sivyo hivyo! Mtakuja jua! 

4. 4, Tena sivyo hivyo! Mtakuja jua! 

5. Sivyo hivyo! Lau mngeli jua kwa ujuzi wa yakini, 

6. Basi bila ya shaka mtaiona Jahannamu! 

7. Tena, bila ya shaka, mtaiona kwa jicho la yakini. 

8. Tena bila ya shaka mtaulizwa siku hiyo juu ya neema. 

 

103 - AL - A'S'R

KWA JINA LA MWENYEZI MUNGU MWINGI WA REHEMA MWENYE KUREHEMU. 

 

1. Naapa kwa Zama! 

2. Hakika binaadamu bila ya shaka yumo katika khasara, 

3. Ila wale walio amini, na wakatenda mema, na wakausiana kwa haki, na wakausiana kusubiri. 

 

104 - AL - HUMAZAH

KWA JINA LA MWENYEZI MUNGU MWINGI WA REHEMA MWENYE KUREHEMU. 

 

1. Ole wake kila safihi, msengenyaji!

2. Aliye kusanya mali na kuyahisabu.

3. Anadhani ya kuwa mali yake yatambakisha milele!

4. Hasha! Atavurumishwa katika H'ut'ama.

5. Na nani atakujuvya ni nini H'ut'ama?

6. Moto wa Mwenyezi Mungu ulio washwa.

7. Ambao unapanda nyoyoni.

8. Hakika huo utafungiwa nao 

9. Kwenye nguzo zilio nyooshwa. 

 

105 - AL - FIIL

KWA JINA LA MWENYEZI MUNGU MWINGI WA REHEMA MWENYE KUREHEMU. 

 

1. Kwani hukuona jinsi Mola wako Mlezi alivyo watenda wale wenye tembo? 

2. Kwani hakujaalia vitimbi vyao kuharibika? 

3. Na akawapelekea ndege makundi kwa makundi, 

4. Wakiwatupia mawe ya udongo wa Motoni, 

5. Akawafanya kama majani yaliyo liwa! 

 

106 - QURAISH

KWA JINA LA MWENYEZI MUNGU MWINGI WA REHEMA MWENYE KUREHEMU. 

 

1. Kwa walivyo zoea Maqureshi, 

2. Kuzoea kwao safari za siku za baridi na siku za joto. 

3. Basi nawamuabudu Mola Mlezi wa Nyumba hii, 

4. Ambaye anawalisha wasipate njaa, na anawalinda na khofu. 

 

107 - AL - MAAU'N

KWA JINA LA MWENYEZI MUNGU MWINGI WA REHEMA MWENYE KUREHEMU. 

 

1. Je! Umemwona anaye kadhibisha Malipo? 

2. Huyo ndiye anaye msukuma yatima, 

3. Wala hahimizi kumlisha masikini. 

4. Basi, ole wao wanao sali, 

5. Ambao wanapuuza Sala zao; 

6. Ambao wanajionyesha, 

7. Nao huku wanazuia msaada. 

 

108 - AL - KAWTHAR

KWA JINA LA MWENYEZI MUNGU MWINGI WA REHEMA MWENYE KUREHEMU. 

 

1. Hakika tumekupa kheri nyingi. 

2. Basi sali na uchinje kwa ajili ya Mola wako Mlezi. 

3. Hakika anaye kuchukia ndiye aliye mpungufu 

 

109 - AL - KAFIRUN

KWA JINA LA MWENYEZI MUNGU MWINGI WA REHEMA MWENYE KUREHEMU. 

 

1. Sema: Enyi makafiri! 

2. Siabudu mnacho kiabudu; 

3. Wala nyinyi hamuabudu ninaye muabudu. 

4. Wala sitaabudu mnacho abudu. 

5. Wala nyinyi hamuabudu ninaye muabudu. 

6. Nyinyi mna dini yenu, nami nina Dini yangu. 

 

110 - ANNAS'R

KWA JINA LA MWENYEZI MUNGU MWINGI WA REHEMA MWENYE KUREHEMU. 

 

1. Itakapo kuja nusura ya Mwenyezi Mungu na ushindi, 

2. Na ukaona watu wanaingia katika Dini ya Mwenyezi Mungu kwa makundi, 

3. Zitakase sifa za Mola wako Mlezi, na umwombe msamaha; hakika Yeye ndiye anaye pokea toba. 

 

111 - AL - MASAD

KWA JINA LA MWENYEZI MUNGU MWINGI WA REHEMA MWENYE KUREHEMU. 

 

1. Imeangamia mikono ya Abu Lahab, na yeye pia ameangamia. 

2. Hayatamfaa mali yake, wala alivyo vichuma. 

3. Atauingia Moto wenye mwako. 

4. Na mkewe, mchukuzi wa kuni, 

5. Shingoni mwake iko kamba iliyo sokotwa. 

 

112 - AL - IKHLAS'

KWA JINA LA MWENYEZI MUNGU MWINGI WA REHEMA MWENYE KUREHEMU. 

 

1. Sema: Yeye Mwenyezi Mungu ni wa pekee. 

2. Mwenyezi Mungu Mkusudiwa. 

3. Hakuzaa wala hakuzaliwa. 

4. Wala hana anaye fanana naye hata mmoja. 

 

113 - AL - FALAQ

KWA JINA LA MWENYEZI MUNGU MWINGI WA REHEMA MWENYE KUREHEMU. 

 

1. Sema: Najikinga kwa Mola Mlezi wa mapambazuko, 

2. Na shari ya alivyo viumba, 

3. Na shari ya giza la usiku liingiapo, 

4. Na shari ya wanao pulizia mafundoni, 

5. Na shari ya hasidi anapo husudu. 

 

114 - ANNAS

KWA JINA LA MWENYEZI MUNGU MWINGI WA REHEMA MWENYE KUREHEMU. 

 

1. Sema: Ninajikinga kwa Mola Mlezi wa wanaadamu, 

2. Mfalme wa wanaadamu, 

3. Mungu wa wanaadamu, 

4. Na shari ya wasiwasi wa Shetani, Khannas, 

5. Anaye tia wasiwasi katika vifua vya watu, 

6. Kutokana na majini na wanaadamu.