Part 27

 

31. AKASEMA: Basi ujumbe wenu ni nini, enyi mlio tumwa? 

32. Wakasema: Hakika sisi tumetumwa kwa watu wakosefu, 

33. Tuwatupie mawe ya udongo, 

34. Yaliyo tiwa alama kutoka kwa Mola wako Mlezi kwa ajili ya wanao pindukia mipaka. 

35. Kwa hivyo tutawatoa katika hao wale walio amini. 

36. Lakini hatukupata humo ila nyumba moja tu yenye Waislamu! 

37. Na tukaacha humo Ishara kwa ajili ya wanao iogopa adhabu chungu. 

38. Na katika khabari za Musa, tulipo mtuma kwa Firauni na hoja wazi. 

39. Lakini alipuuza kwa sababu ya nguvu zake na akasema: Huyu ni mchawi au mwendawazimu! 

40. Basi tukamkamata yeye na majeshi yake na tukawatupa baharini, na yeye ndiye wa kulaumiwa. 

41. Na katika khabari za A'di tulipo wapelekea upepo wa kukata uzazi. 

42. Haukuacha chochote ulicho kifikia ila ulikifanya kama kilio nyambuka. 

43. Na katika khabari za Thamudi walipo ambiwa: Jifurahisheni kwa muda mdogo tu. 

44. Wakaasi amri ya Mola wao Mlezi. Basi uliwanyakua moto wa radi nao wanaona. 

45. Basi hawakuweza kusimama wala hawakuwa wenye kujitetea. 

46. Na kaumu ya Nuhu hapo mbele. Hakika hao walikuwa watu wapotovu. 

47. Na mbingu tumezifanya kwa nguvu na uwezo na hakika Sisi bila ya shaka ndio twenye uwezo wa kuzitanua. 

48. Na ardhi tumeitandaza; basi watandazaji wazuri namna gani Sisi! 

49. Na katika kila kitu tumeumba kwa jozi ili mzingatie. 

50. Basi kimbilieni kwa Mwenyezi Mungu, hakika mimi ni mwonyaji kwenu wa kubainisha nitokae kwake. 

51. Wala msifanye kuwa kuna mungu mwengine pamoja na Mwenyezi Mungu. Hakika mimi ni mwonyaji kwenu wa kubainisha nitokae kwake. 

52. Basi ndio hivyo hivyo, hakuwajia kabla yao Mtume ila walisema: Huyu ni mchawi au mwendawazimu. 

53. Je! Wameambizana kwa haya? Bali hawa ni watu waasi. 

54. Basi waachilie mbali, nawe hulaumiwi. 

55. Na kumbusha, kwani ukumbusho huwafaa Waumini. 

56. Nami sikuwaumba majini na watu ila waniabudu Mimi. 

57. Na sitaki kwao riziki, wala sitaki wanilishe. 

58. Hakika Mwenyezi Mungu ndiye Mwenye kuruzuku, Mwenye nguvu, Madhubuti. 

59. Hakika walio dhulumu wana fungu lao la adhabu kama fungu la wenzao. Basi wasinihimize. 

60. Ole wao walio ikanusha siku yao waliyo ahidiwa. 

 

52 - ATT'UR

KWA JINA LA MWENYEZI MUNGU MWINGI WA REHEMA MWENYE KUREHEMU. 

 

1. Naapa kwa mlima wa T'ur, 

2. Na Kitabu kilicho andikwa 

3. Katika ngozi iliyo kunjuliwa, 

4. Na kwa Nyumba iliyo jengwa, 

5. Na kwa dari iliyo nyanyuliwa, 

6. Na kwa bahari iliyo jazwa, 

7. Hakika adhabu ya Mola wako Mlezi hapana shaka itatokea. 

8. Hapana wa kuizuia. 

9. Siku zitakapo tikisika mbingu kwa mtikiso, 

10. Na milima iwe inakwenda kwa mwendo mkubwa. 

11. Basi ole wao siku hiyo hao wanao kadhibisha, 

12. Ambao wanacheza katika mambo ya upuuzi. 

13. Siku watapo sukumwa kwenye Moto kwa msukumo wa nguvu, 

14. (Waambiwe): Huu ndio ule Moto mlio kuwa mkiukanusha! 

15. Je! Huu ni uchawi, au hamwoni tu? 

16. Uingieni, mkistahamili au msistahamili - ni mamoja kwenu. Hakika mnalipwa kwa mliyo kuwa mkiyatenda. 

17. Hakika wachamngu watakuwa katika Mabustani na neema, 

18. Wakifurahi kwa yale aliyo wapa Mola wao Mlezi. Na Mola wao Mlezi atawalinda na adhabu ya Motoni. 

19. Kuleni na kunyweni kwa raha kabisa kwa sababu ya mliyo kuwa mkiyatenda. 

20. Watakuwa wameegemea juu ya viti vya enzi vilivyo pangwa kwa safu. Na tutawaoza mahuru-l-aini. 

21. Na walio amini na dhuriya zao wakawafuata kwa Imani tutawakutanisha nao dhuriya zao, na wala hatutawapunja hata kidogo katika vitendo vyao. Kila mtu lazima atapata alicho kichuma. 

22. Na tutawapa matunda, na nyama kama watavyo penda. 

23. Watapeana humo bilauri zisio na vinywaji vya kuleta maneno ya upuuzi wala dhambi. 

24. Iwe wanawapitia watumishi wao kama kwamba ni lulu zilizomo katika chaza. 

25. Wataelekeana wakiulizana. 

26. Waseme: Tulikuwa zamani pamoja na ahali zetu tukiogopa; 

27. Basi Mwenyezi Mungu akatufanyia hisani na akatulinda na adhabu ya upepo wa Moto. 

28. Hakika sisi zamani tulikuwa tukimwomba Yeye tu. Hakika Yeye ndiye Mwema Mwenye kurehemu. 

29. Basi kumbusha! Kwani wewe, kwa neema ya Mola wako Mlezi, si kuhani wala mwendawazimu. 

30. Au wanasema: Huyu ni mtunga mashairi, tunamtarajia kupatilizwa na dahari. 

31. Sema: Tarajieni, na mimi pia ni pamoja nanyi katika kutarajia. 

32. Au hizo akili zao ndio zinawaamrisha haya, au wao basi ni watu majeuri tu? 

33. Au ndio wanasema: Ameitunga hii! Bali basi tu hawaamini! 

34. Basi nawalete masimulizi kama haya ikiwa wao wanasema kweli. 

35. Au wao wameumbwa pasipo kutokana na kitu chochote, au ni wao ndio waumbaji? 

36. Au wao wameziumba mbingu na ardhi? Bali hawana na yakini. 

37. Au wanazo khazina za Mola wako Mlezi au wao ndio wenye madaraka? 

38. Au wanazo ngazi za kusikilizia? Basi huyo msikilizaji wao na alete hoja ilio wazi! 

39. Au Yeye Mwenyezi Mungu ana wasichana, na nyinyi ndio mna wavulana? 

40. Au wewe unawaomba ujira, na kwa hivyo ndio wanaelemewa na uzito wa gharama? 

41. Au wanayo ilimu ya ghaibu, nao wameandika? 

42. Au wanataka kufanya vitimbi tu? Lakini hao walio kufuru ndio watakao tegeka. 

43. Au wanae mungu asiye kuwa Mwenyezi Mungu? Subhanallah! Ametaksika Mwenyezi Mungu na hao wanao washirikisha naye. 

44. Na hata wange ona pande linatoka mbinguni linaanguka wange sema: Ni mawingu yaliyo bebana. 

45. Basi waache mpaka wakutane na siku yao watakapo hilikishwa. 

46. Siku ambayo hila zao hazitawafaa hata kidogo, wala wao hawatanusuriwa. 

47. Na hakika walio dhulumu watapata adhabu nyengine isiyo kuwa hii, lakini wengi wao hawajui. 

48. Na ingojee hukumu ya Mola wako Mlezi. Kwani wewe hakika uko mbele ya macho yetu, na mtakase kwa kumsifu Mola wako Mlezi unapo simama, 

49. Na usiku pia mtakase, na zinapo kuchwa nyota. 

 

53 - ANNAJM

KWA JINA LA MWENYEZI MUNGU MWINGI WA REHEMA MWENYE KUREHEMU. 

 

1. Naapa kwa nyota inapo tua, 

2. Mwenzenu huyu hakupotea, wala hakukosea. 

3. Wala hatamki kwa matamanio. 

4. Hayakuwa haya ila ni ufunuo ulio funuliwa; 

5. Amemfundisha aliye mwingi wa nguvu, 

6. Mwenye kutua, akatulia, 

7. Naye yuko juu kabisa upeo wa macho. 

8. Kisha akakaribia na akateremka. 

9. Akawa ni kama baina ya mipinde miwili, au karibu zaidi. 

10. Akamfunulia mja wake (Mwenyezi Mungu) alicho mfunulia. 

11. Moyo haukusema uwongo uliyo yaona. 

12. Je! Mnabishana naye kwa aliyo yaona? 

13. Na akamwona mara nyingine, 

14. Penye Mkunazi wa mwisho. 

15. Karibu yake ndiyo ipo Bustani inayo kaliwa. 

16. Kilipo ufunika huo Mkunazi hicho kilicho ufunuika. 

17. Jicho halikuhangaika wala halikuruka mpaka. 

18. Kwa yakini aliona katika Ishara kubwa kabisa za Mola wake Mlezi. 

19. Je! Mmemuona Lata na Uzza? 

20. Na Manaat, mwingine wa tatu? 

21. Je! Nyinyi mnao wana wanaume na Yeye ndio awe na wanawake? 

22. Huo ni mgawanyo wa dhulma! 

23. Hayo hayakuwa ila ni majina mliyo wapa nyinyi na baba zenu. Mwenyezi Mungu hakuleta uthibitisho wowote juu ya hayo. Hawafuati ila dhana tu na kipendacho nafsi. Na kwa yakini uwongofu ulikwisha wafikia kutoka kwa Mola wao Mlezi. 

24. Ati mtu anakipata kila anacho kitamani? 

25. Mwenyezi Mungu tu ndiye Mwenye dunia na Akhera. 

26. Na wako Malaika wangapi mbinguni, ambao uombezi wao hautafaa chochote isipo kuwa baada ya Mwenyezi Mungu kutoa idhini kwa amtakaye na kumridhia. 

27. Hakika wasio amini Akhera bila ya shaka wao ndio wanawaita Malaika kwa majina ya kike. 

28. Nao hawana ujuzi wowote kwa hayo isipo kuwa wanafuata dhana tu. Na dhana haisaidii chochote mbele ya haki. 

29. Basi mwachilie mbali anaye upa kisogo ukumbusho wetu, na wala hataki ila maisha ya dunia. 

30. Huo ndio mwisho wao wa ujuzi. Hakika Mola wako Mlezi ndiye anaye mjua zaidi mwenye kuipotea njia yake, na Yeye ndiye anaye mjua zaidi mwenye kuongoka. 

31. Ni vya Mwenyezi Mungu vyote viliomo mbinguni na viliomo katika ardhi, ili awalipe walio tenda ubaya kwa waliyo yatenda, na walio tenda mema awalipe mema. 

32. Ambao wanajiepusha na madhambi makuu na vitendo vichafu, isipo kuwa makosa khafifu. Hakika Mola wako Mlezi ni Mkunjufu wa maghfira, naye anakujueni sana tangu alipo kuumbeni kutoka kwenye ardhi, na mlipo kuwa mimba matumboni mwa mama zenu. Basi msijisifu usafi. Yeye anamjua sana mwenye kujikinga na maovu. 

33. Je! Umemwona yule aliye geuka? 

34. Na akatoa kidogo, kisha akajizuia? 

35. Je! Anayo huyo ilimu ya ghaibu, basi ndio anaona? 

36. Au hakuambiwa yaliyomo katika Vitabu vya Musa? 

37. Na vya Ibrahimu aliye timiza ahadi? 

38. Ya kwamba hakika nafsi iliyo beba madhambi haibebi madhambi ya mwengine? 

39. Na ya kwamba hatapata mtu ila aliyo yafanya mwenyewe? 

40. Na kwamba vitendo vyake vitaonekana? 

41. Kisha ndio atalipwa malipo yake kwa ukamilifu. 

42. Na kwamba kwao Mola wako Mlezi ndio mwisho. 

43. Na kwamba Yeye ndiye anaye leta kicheko na kilio. 

44. Na kwamba Yeye ndiye anaye fisha na kuhuisha. 

45. Na kwamba Yeye ndiye aliye umba jozi, dume na jike 

46. Kutokana na mbegu ya uzazi inapo miminwa. 

47. Na kwamba ni juu yake ufufuo mwengine. 

48. Na kwamba ni Yeye ndiye anaye tosheleza na kukinaisha. 

49. Na kwamba hakika Yeye ndiye Mola Mlezi wa nyota ya Shii'ra. 

50. Na kwamba Yeye ndiye aliye waangamiza A'di wa kwanza, 

51. Na Thamudi hakuwabakisha, 

52. Na kabla yao kaumu ya Nuhu. Na hao hakika walikuwa ni madhaalimu zaidi, na waovu zaidi; 

53. Na miji iliyo pinduliwa, ni Yeye aliye ipindua. 

54. Vikaifunika vilivyo funika. 

55. Basi neema gani ya Mola wako Mlezi unayo ifanyia shaka? 

56. Hili ni Onyo katika maonyo yale yale ya zamani. 

57. Kiyama kimekaribia! 

58. Hapana wa kukifichua isipo kuwa Mwenyezi Mungu. 

59. Je! Mnayastaajabia maneno haya? 

60. Na mnacheka, wala hamlii? 

61. Nanyi mmeghafilika? 

62. Basi msujudieni Mwenyezi Mungu, na mumuabudu. 

 

54 - AL-QAMAR

KWA JINA LA MWENYEZI MUNGU MWINGI WA REHEMA MWENYE KUREHEMU. 

 

1. Saa imekaribia, na mwezi umepasuka! 

2. Na wakiona Ishara hugeuka upande na husema: Huu uchawi tu unazidi kuendelea. 

3. Na wamekanusha na wamefuata matamanio yao. Na kila jambo ni lenye kuthibiti. 

4. Na bila ya shaka zimewajia khabari zenye makaripio. 

5. Hikima kaamili; lakini maonyo hayafai kitu! 

6. Basi jiepushe nao. Siku atakapo ita mwitaji kuliendea jambo linalo chusha; 

7. Macho yao yatainama; watatoka makaburini kama nzige walio tawanyika, 

8. Wanamkimbilia mwitaji, na makafiri wanasema: Hii ni siku ngumu. 

9. Kabla yao kaumu ya Nuhu walikanusha; wakamkanusha mja wetu, na wakasema ni mwendawazimu, na akakaripiwa. 

10. Basi akamwomba Mola wake Mlezi akasema: Kwa hakika mimi nimeshindwa, basi ninusuru! 

11. Basi tukaifungua milango ya mbingu kwa maji yanayo miminika. 

12. Na tukazipasua ardhi kwa chemchem, yakakutana maji kwa jambo lilio kadiriwa. 

13. Na tukamchukua kwenye safina ya mbao na kamba. 

14. Ikawa inakwenda kwa nadhari yetu, kuwa ni malipo kwa alivyo kuwa amekanushwa. 

15. Na bila ya shaka tuliiacha iwe ni Ishara. Lakini je, yupo anaye kumbuka? 

16. Basi ilikuwaje adhabu yangu, na maonyo yangu. 

17. Na bila ya shaka Sisi tumeifanya Qur'ani iwe nyepesi kufahamika. Lakini yupo anaye kumbuka? 

18. Kina A'di walikanusha. Basi ilikuwaje adhabu yangu na maonyo yangu? 

19. Hakika Sisi tuliwapelekea upepo wa kimbunga katika siku korofi mfululizo, 

20. Ukiwang'oa watu kama vigogo vya mitende vilio ng'olewa. 

21. Basi ilikuwaje adhabu yangu na maonyo yangu? 

22. Na bila ya shaka Sisi tumeifanya Qur'ani nyepesi kufahamika; lakini yupo anaye kumbuka? 

23. Thamudi waliwakanusha Waonyaji. 

24. Wakasema: Ati tumfuate binaadamu mmoja katika sisi? Basi hivyo sisi tutakuwa katika upotofu na kichaa! 

25. Ni yeye tu aliye teremshiwa huo ukumbusho kati yetu sote? Bali huyu ni mwongo mwenye kiburi! 

26. Kesho watajua ni nani huyo mwongo mwenye kiburi. 

27. Hakika Sisi tutawapelekea ngamia jike ili kuwajaribu, basi watazame tu na ustahamili. 

28. Na waambie kwamba maji yatagawanywa baina yao; kila sehemu ya maji itahudhuriwa na aliye khusika. 

29. Basi wakamwita mtu wao akaja akamchinja. 

30. Basi ilikuwaje adhabu yangu na maonyo yangu! 

31. Hakika Sisi tuliwapelekea ukelele mmoja tu, wakawa kama mabuwa ya kujengea uwa. 

32. Na bila ya shaka Sisi tumeifanya Qur'ani iwe nyepesi kwa kukumbuka, lakini yupo akumbukaye? 

33. Kaumu Lut'i nao waliwakadhibisha Waonyaji. 

34. Hakika Sisi tukawapelekea kimbunga cha vijiwe, isipo kuwa wafuasi wa Lut'i. Hao tuliwaokoa karibu na alfajiri. 

35. Kwa neema inayo toka kwetu. Hivyo ndivyo tumlipavyo anaye shukuru. 

36. Na hakika yeye aliwaonya adhabu yetu; lakini wao waliyatilia shaka hayo maonyo. 

37. Na walimtaka awape wageni wake. Tukayapofua macho yao, na tukawaambia: Onjeni basi adhabu na maonyo yangu! 

38. Na iliwafikia wakati wa asubuhi adhabu yangu ya kuendelea. 

39. Basi onjeni adhabu na maonyo yangu! 

40. Na hakika tumeisahilisha Qur'ani kuikumbuka. Lakini yupo anaye kumbuka? 

41. Na Waonyaji waliwafikia watu wa Firauni. 

42. Walizikadhibisha Ishara zetu zote, nasi tukawashika kama anavyo shika Mwenye nguvu Mwenye uweza. 

43. Je! Makafiri wenu ni bora kuliko hao, au yameandikwa vitabuni kuwa nyinyi hamtiwi makosani? 

44. Au ndio wanasema: Sisi ni wengi tutashinda tu. 

45. Wingi wao huu utashindwa, na wao watasukumwa nyuma. 

46. Bali Saa ya Kiyama ndio miadi yao, na Saa hiyo ni nzito zaidi na chungu zaidi. 

47. Hakika wakosefu wamo katika upotofu na wazimu. 

48. Siku watakapo kokotwa Motoni kifudifudi waambiwe: Onjeni mguso wa Jahannamu! 

49. Kwa hakika Sisi tumekiumba kila kitu kwa kipimo. 

50. Na amri yetu haikuwa ila ni moja tu, kama kupepesa jicho. 

51. Na bila ya shaka tumekwisha waangamiza wenzenu. Lakini yupo anaye kumbuka? 

52. Na kila jambo walilo lifanya limo vitabuni. 

53. Na kila kidogo na kikubwa kimeandikwa. 

54. Hakika wachamngu watakuwa katika Mabustani na mito. 

55. Katika makalio ya haki kwa Mfalme Mwenye uweza. 

 

55 - ARRAH'MAN

KWA JINA LA MWENYEZI MUNGU MWINGI WA REHEMA MWENYE KUREHEMU. 

 

1. Arrah'man, Mwingi wa Rehema 

2. Amefundisha Qur'ani. 

3. Amemuumba mwanaadamu, 

4. Akamfundisha kubaini. 

5. Jua na mwezi huenda kwa hisabu. 

6. Na mimea yenye kutambaa, na miti, inanyenyekea. 

7. Na mbingu ameziinua, na ameweka mizani, 

8. Ili msidhulumu katika mizani. 

9. Na wekeni mizani kwa haki, wala msipunje katika mizani. 

10. Na ardhi ameiweka kwa ajili ya viumbe. 

11. Humo yamo matunda na mitende yenye mafumba. 

12. Na nafaka zenye makapi, na rehani. 

13. Basi ni ipi katika neema za Mola wenu Mlezi mnayo ikanusha 

14. Amemuumba mtu kwa udongo wa kinamo.. 

15. Na akawaumba majini kwa ulimi wa moto. 

16. Basi ni ipi katika neema za Mola wenu Mlezi mnayo ikanusha 

17. Mola Mlezi wa mashariki mbili na wa magharibi mbili. 

18. Basi ni ipi katika neema za Mola wenu Mlezi mnayo ikanusha? 

19. Anaziendesha bahari mbili zikutane; 

20. Baina yao kipo kizuizi, zisiingiliane. 

21. Basi ni ipi katika neema za Mola wenu Mlezi mnayo ikanusha? 

22. Katika hizo bahari mbili zinatoka lulu na marijani. 

23. Basi ni ipi katika neema za Mola wenu Mlezi mnayo ikanusha? 

24. Na ni vyake Yeye hivi viendavyo baharini vilivyo undwa kama vilima. 

25. Basi ni ipi katika neema za Mola wenu Mlezi mnayo ikanusha? 

26. Kila kilioko juu yake kitatoweka. 

27. Na atabakia Mwenyewe Mola wako Mlezi Mwenye utukufu na ukarimu. 

28. Basi ni ipi katika neema za Mola wenu Mlezi mnayo ikanusha? 

29. Vinamwomba Yeye vilivyomo katika mbingu na ardhi. Kila siku Yeye yumo katika mambo. 

30. Basi ni ipi katika neema za Mola wenu Mlezi mnayo ikanusha? 

31. Tutakuhisabuni enyi makundi mawili. 

32. Basi ni ipi katika neema za Mola wenu Mlezi mnayo ikanusha? 

33. Enyi makundi ya majini na watu! Mkiweza kupenya kwenye mbingu na ardhi, basi penyeni! Hamtapenya ila kwa kupewa madaraka. 

34. Basi ni ipi katika neema za Mola wenu Mlezi mnayo ikanusha? 

35. Mtapelekewa muwako wa moto na shaba; wala hamtashinda. 

36. Basi ni ipi katika neema za Mola wenu Mlezi mnayo ikanusha? 

37. Itakapo pasuka mbingu ikawa nyekundu kama mafuta. 

38. Basi ni ipi katika neema za Mola wenu Mlezi mnayo ikanusha? 

39. Siku hiyo hataulizwa dhambi zake mtu wala jini. 

40. Basi ni ipi katika neema za Mola wenu Mlezi mnayo ikanusha? 

41. Watajuulikana wakosefu kwa alama zao, basi watashikwa kwa nywele zao za utosini na kwa miguu. 

42. Basi ni ipi katika neema za Mola wenu Mlezi mnayo ikanusha? 

43. Hii ndiyo Jahannamu ambayo wakosefu wakiikanusha. 

44. Watakuwa wakizunguka baina ya hiyo na maji ya moto yanayo chemka. 

45. Basi ni ipi katika neema za Mola wenu Mlezi mnayo ikanusha? 

46. Na mwenye kuogopa kusimamishwa mbele ya Mola wake Mlezi atapata Bustani mbili. 

47. Basi ni ipi katika neema za Mola wenu Mlezi mnayo ikanusha? 

48. Bustani zenye matawi yaliyo tanda. 

49. Basi ni ipi katika neema za Mola wenu Mlezi mnayo ikanusha? 

50. Ndani yake zimo chemchem mbili zinazo pita. 

51. Basi ni ipi katika neema za Mola wenu Mlezi mnayo ikanusha? 

52. Humo katika kila matunda zimo namna mbili. 

53. Basi ni ipi katika neema za Mola wenu Mlezi mnayo ikanusha? 

54. Wawe wameegemea matandiko yenye bit'ana ya hariri nzito; na matunda ya Bustani hizo yapo karibu. 

55. Basi ni ipi katika neema za Mola wenu Mlezi mnayo ikanusha? 

56. Humo watakuwamo wanawake watulizao macho yao; hajawagusa mtu kabla yao wala jini. 

57. Basi ni ipi katika neema za Mola wenu Mlezi mnayo ikanusha? 

58. Kama kwamba wao ni yakuti na marijani. 

59. Basi ni ipi katika neema za Mola wenu Mlezi mnayo ikanusha. 

60. Ati yaweza kuwa malipo ya ihsani ila ihsani? 

61. Basi ni ipi katika neema za Mola wenu Mlezi mnayo ikanusha? 

62. Na zaidi ya hizo zipo Bustani nyengine mbili. 

63. Basi ni ipi katika neema za Mola wenu Mlezi mnayo ikanusha? 

64. Za kijani kibivu. 

65. Basi ni ipi katika neema za Mola wenu Mlezi mnayo ikanusha? 

66. Na chemchem mbili zinazo furika. 

67. Basi ni ipi katika neema za Mola wenu Mlezi mnayo ikanusha? 

68. Imo humo miti ya matunda, na mitende na mikomamanga. 

69. Basi ni ipi katika neema za Mola wenu Mlezi mnayo ikanusha? 

70. Humo wamo wanawake wema wazuri. 

71. Basi ni ipi katika neema za Mola wenu Mlezi mnayo ikanusha? 

72. Wanawake wazuri wanao tawishwa katika makhema. 

73. Basi ni ipi katika neema za Mola wenu Mlezi mnayo ikanusha? 

74. Hajawagusa mtu wala jini kabla yao. 

75. Basi ni ipi katika neema za Mola wenu Mlezi mnayo ikanusha? 

76. Wameegemea juu ya matakia ya kijani na mazulia mazuri. 

77. Basi ni ipi katika neema za Mola wenu Mlezi mnayo ikanusha? 

78. Limetukuka jina la Mola wako Mlezi Mwenye utukufu na ukarimu. 

 

56 - AL -WAAQIA'H

KWA JINA LA MWENYEZI MUNGU MWINGI WA REHEMA MWENYE KUREHEMU. 

 

1. Litakapo tukia hilo Tukio 

2. Hapana cha kukanusha kutukia kwake. 

3. Literemshalo linyanyualo, 

4. Itakapo tikiswa ardhi kwa mtikiso, 

5. Na milima itapo sagwasagwa, 

6. Iwe mavumbi yanayo peperushwa, 

7. Na nyinyi mtakuwa namna tatu:- 

8. Basi watakuwepo wa kuliani; je, ni wepi wa kuliani? 

9. Na wa kushotoni; je, ni wepi wa kushotoni? 

10. Na wa mbele watakuwa mbele. 

11. Hao ndio watakao karibishwa 

12. Katika Bustani zenye neema. 

13. Fungu kubwa katika wa mwanzo, 

14. Na wachache katika wa mwisho. 

15. Watakuwa juu ya viti vya fakhari vilivyo tonewa. 

16. Wakiviegemea wakielekeana. 

17. Wakitumikiwa na wavulana wa ujana wa milele, 

18. Kwa vikombe na mabirika na bilauri za vinywaji kutoka chemchem safi. 

19. Hawataumwa kichwa kwa vinywaji hivyo wala hawatoleweshwa. 

20. Na matunda wayapendayo, 

21. Na nyama za ndege kama wanavyo tamani. 

22. Na Mahurulaini, 

23. Walio kama mfano wa lulu zilio hifadhiwa. 

24. Ni malipo kwa waliyo kuwa wakiyatenda. 

25. Humo hawatasikia porojo wala maneno ya dhambi, 

26. Isipo kuwa maneno ya Salama, Salama. 

27. Na wale wa mkono wa kulia, ni yepi yatakuwa ya wa kuliani? 

28. Katika mikunazi isiyo na miba, 

29. Na migomba iliyo pangiliwa, 

30. Na kivuli kilicho tanda, 

31. Na maji yanayo miminika, 

32. Na matunda mengi, 

33. Hayatindikii wala hayakatazwi, 

34. Na matandiko yaliyo nyanyuliwa. 

35. Hakika Sisi tutawaumba (Mahurulaini) upya, 

36. Na tutawafanya vijana, 

37. Wanapendana na waume zao, hirimu moja. 

38. Kwa ajili ya watu wa kuliani. 

39. Fungu kubwa katika wa mwanzo, 

40. Na fungu kubwa katika wa mwisho. 3 

41. Na watu wa kushotoni; je ni yepi ya wa kushotoni? 

42. Katika upepo wa moto, na maji yanayo chemka, 

43. Na kivuli cha moshi mweusi, 

44. Si cha kuburudisha wala kustarehesha. 

45. Hakika hao walikuwa kabla ya haya wakiishi maisha ya anasa. 

46. Na walikuwa wakishikilia kufanya madhambi makubwa, 

47. Na walikuwa wakisema: Tutakapo kufa na tukawa udongo na mafupa, ati ndio tutafufuliwa? 

48. Au baba zetu wa zamani? 

49. Sema: Hakika wa zamani na wa mwisho 

50. Bila ya shaka watakusanywa kwa wakati wa siku maalumu. 

51. Kisha nyinyi, mlio potea, mnao kanusha, 

52. Kwa yakini mtakula mti wa Zaqqumu. 

53. Na kwa mti huo mtajaza matumbo. 

54. Na juu yake mtakunywa maji yanayo chemka. 

55. Tena mtakunywa kama wanavyo kunywa ngamia wenye kiu. 

56. Hiyo ndiyo karamu yao Siku ya Malipo. 

57. Sisi tumekuumbeni; basi hamsadiki? 

58. Je! Mnaiona mbegu ya uzazi mnayo idondokeza? 

59. Je! Mnaiumba nyinyi, au ni Sisi ndio Waumbaji? 

60. Sisi tumekuwekeeni mauti; na wala Sisi hatushindwi 

61. Kuwaleta wengine badala yenu na kukuumbeni nyinyi kwa umbo msilo lijua. 

62. Na bila ya shaka mlikwisha jua umbo la kwanza, basi kwa nini hamkumbuki? 

63. Je! Mnaona makulima mnayo yapanda? 

64. Je! Ni nyinyi mnayo yaotesha au ni Sisi ndio wenye kuotesha? 

65. Tungeli taka tungeli yafanya yakawa mapepe, mkabaki mnastaajabu, 

66. Mkisema: Hakika sisi tumegharimika; 

67. Bali sisi tumenyimwa. 

68. Je! Mnayaona maji mnayo yanywa? 

69. Je! Ni nyinyi mnayo yateremsha kutoka mawinguni au ni Sisi ndio wenye kuyateremsha? 

70. Tungeli penda tungeli yafanya ya chumvi. Basi mbona hamshukuru? 

71. Je! Mnauona moto mnao uwasha? 

72. Ni nyinyi mlio uumba mti wake au Sisi ndio Waumbaji? 

73. Sisi tumeufanya uwe ni ukumbusho na manufaa kwa walioko nyikani. 

74. Basi litakase jina la Mola wako Mlezi aliye Mkuu. 

75. Basi naapa kwa maanguko ya nyota, 

76. Na hakika bila ya shaka hichi ni kiapo kikubwa, laiti mngeli jua! 

77. Hakika hii bila ya shaka ni Qur'ani Tukufu, 

78. Katika Kitabu kilicho hifadhiwa. 

79. Hapana akigusaye ila walio takaswa. 

80. Ni uteremsho unao toka kwa Mola Mlezi wa walimwengu wote. 

81. Ni maneno haya ndiyo nyinyi mnayapuuza? 

82. Na badala ya kushukuru kwa riziki yenu mnafanya kuwa mnakadhibisha? 

83. Yawaje basi itakapo fika roho kwenye koo, 

84. Na nyinyi wakati huo mnatazama! 

85. Na Sisi tuko karibu zaidi naye kuliko nyinyi. 

86. Na lau kuwa nyinyi hamumo katika mamlaka yangu, 

87. Kwanini hamuirudishi hiyo roho, ikiwa nyinyi mnasema kweli? 

88. Basi akiwa miongoni mwa walio karibishwa, 

89. Basi ni raha, na manukato, na Bustani zenye neema. 

90. Na akiwa katika watu wa upande wa kulia, 

91. Basi ni Salamu kwako uliye miongoni mwa watu wa upande wa kulia. 

92. Na ama akiwa katika walio kadhibisha wapotovu, 

93. Basi karamu yake ni maji yanayo chemka, 

94. Na kutiwa Motoni. 

95. Hakika hii ndiyo haki yenye yakini. 

96. Basi litakase jina la Mola wako Mlezi aliye Mkubwa. 

 

57 - AL -H'ADIID

KWA JINA LA MWENYEZI MUNGU MWINGI WA REHEMA MWENYE KUREHEMU. 

 

1. Kinamsabihi kumtakasa Mwenyezi Mungu kila kiliomo ndani ya mbingu na ardhi. Na Yeye ndiye Mwenye nguvu, Mwenye hikima. 

2. Yeye ndiye Mwenye ufalme wa mbingu na ardhi. Anahuisha na anafisha. Na Yeye ni Mwenye uweza wa kila kitu. 

3. Yeye ndiye wa Mwanzo na ndiye wa Mwisho, naye ndiye wa Dhaahiri na wa Siri, naye ndiye Mjuzi wa kila kitu. 

4. Yeye ndiye aliye ziumba mbingu na ardhi katika siku sita; kisha akakaa vyema juu ya enzi. Anayajua yanayo ingia katika ardhi na yanayo toka humo, na yanayo teremka kutoka mbinguni, na yanayo panda humo. Naye yu pamoja nanyi popote mlipo. Na Mwenyezi Mungu ni Mwenye kuyaona mnayo yatenda. 

5. Ufalme wa mbingu na ardhi ni wake. Na mambo yote yanarejeshwa kwa Mwenyezi Mungu. 

6. Anaingiza usiku katika mchana, na anaingiza mchana katika usiku. Na Yeye ni Mwenye kuyajua yaliomo vifuani. 

7. Muaminini Mwenyezi Mungu na Mtume wake; na toeni katika alivyo kufanyeni nyinyi kuwa ni waangalizi wake. Basi walio amini miongoni mwenu, na wakatoa, wana malipo makubwa. 

8. Na mna nini hata hamumuamini Mwenyezi Mungu na hali Mtume anakuiteni mumuamini Mola wenu Mlezi? Naye amekwisha chukua ahadi yenu, ikiwa nyinyi ni Waumini. 

9. Yeye ndiye anaye mteremshia mja wake Aya zinazo bainisha wazi ili akutoeni gizani muingie kwenye nuru. Na hakika Mwenyezi Mungu kwenu ni Mpole, Mwenye kurehemu. 

10. Na mna nini hata hamtoi katika Njia ya Mwenyezi Mungu, na hali urithi wa mbingu na ardhi ni wa Mwenyezi Mungu? Hawawi sawa miongoni mwenu wenye kutoa kabla ya Ushindi na wakapigana vita. Hao wana daraja kubwa zaidi kuliko wale ambao walio toa baadae na wakapigana. Na wote hao Mwenyezi Mungu amewaahidia wema. Na Mwenyezi Mungu anazo khabari za mnayo yatenda. 

11. Ni nani atakaye mkopesha Mwenyezi Mungu mkopo mwema, ili amrudishie mardufu, na apate malipo ya ukarimu. 

12. Siku utakapo waona Waumini wanaume na Waumini wanawake, nuru yao iko mbele yao, na kuliani kwao: Furaha yenu leo - Bustani zipitazo mito kati yake mtakaa humo milele. Huko ndiko kufuzu kukubwa. 

13. Siku wanaafiki wanaume na wanaafiki wanawake watapo waambia walio amini: Tungojeni ili tupate mwangaza katika nuru yenu. Waambiwe: Rejeeni nyuma yenu mkaitafute nuru! Utiwe baina yao ukuta wenye mlango - ndani yake mna rehema, na nje upande wake wa mbele kuna adhabu. 

14. Watawaita wawaambie: Kwani vile hatukuwa pamoja nanyi? Watawaambia: Ndiyo, lakini mlijifitini wenyewe, na mkasitasita, na mkatia shaka, na matamanio ya nafsi zenu yakakudanganyeni. mpaka ilipo kuja amri ya Mwenyezi Mungu, na mdanganyifu akakudanganyeni msimfuate Mwenyezi Mungu. 

15. Basi leo haitapokelewa kwenu fidia, wala kwa wale walio kufuru. Makaazi yenu ni Motoni, ndio bora kwenu; na ni marejeo maovu yalioje! 

16. Je! Wakati haujafika bado kwa walio amini zikanyenyekea nyoyo zao kwa kumkumbuka Mwenyezi Mungu na haki iliyo teremka? Wala wasiwe kama walio pewa Kitabu kabla yao, muda wao ukawa mrefu, kwa hivyo nyoyo zao zikawa ngumu, na wengi wao wakawa wapotovu. 

17. Jueni kwamba Mwenyezi Mungu huifufua ardhi baada ya kufa kwake. Tumekubainishieni Ishara ili mpate kuzingatia. 

18. Kwa hakika wanaume wanao toa sadaka, na wanawake wanao toa sadaka, na wakamkopesha Mwenyezi Mungu mkopo mwema, watazidishiwa mardufu na watapata malipo ya ukarimu. 

19. Na walio muamini Mwenyezi Mungu na Mitume wake, hao ndio Masidiqi na Mashahidi mbele ya Mola wao Mlezi. Wao watapata malipo yao na nuru yao. Na walio kufuru na wakakadhibisha Ishara zetu, hao ndio watu wa Motoni. 

20. Jueni ya kwamba maisha ya dunia ni mchezo, na pumbao, na pambo, na kujifakhirisha baina yenu na kushindana kwa wingi wa mali na watoto. Mfano wake ni kama mvua ambayo huwafurahisha wakulima mimea yake, kisha hunyauka ukayaona yamepiga manjano kisha yakawa mabua. Na akhera kuna adhabu kali na maghfira kutoka kwa Mwenyezi Mungu na radhi. Na maisha ya dunia si chochote ila ni starehe ya udanganyifu. 

21. Kimbilieni msamaha wa Mola wenu Mlezi, na Pepo ambayo upana wake ni kama upana wa mbingu na ardhi, iliyo wekewa walio muamini Mwenyezi Mungu na Mitume wake. Hiyo ndiyo fadhila ya Mwenyezi Mungu, humpa amtakaye. Na Mwenyezi Mungu ni Mwenye fadhila kuu. 

22. Hautokei msiba katika ardhi wala katika nafsi zenu ila umekwisha andikwa katika Kitabu kabla hatujauumba. Hakika hayo kwa Mwenyezi Mungu ni mepesi. 

23. Ili msihuzunike kwa kilicho kupoteeni, wala msijitape kwa alicho kupeni. Na Mwenyezi Mungu hampendi kila anaye jivuna akajifakhirisha. 

24. Ambao wanafanya ubakhili, na wanaamrisha watu wafanye ubakhili. Na anaye geuka, basi Mwenyezi Mungu ni Mwenye kujitosha, Msifiwa. 

25. Kwa hakika tuliwatuma Mitume wetu kwa dalili waziwazi, na tukateremsha Kitabu pamoja nao na Mizani, ili watu wasimamie uadilifu, na tumeteremsha chuma chenye nguvu nyingi na manufaa kwa watu, na ili Mwenyezi Mungu amjue anaye mnusuru Yeye na Mitume wake kwa ghaibu. Hakika Mwenyezi Mungu ni Mwenye nguvu Mwenye kushinda. 

26. Na bila ya shaka tulimtuma Nuhu na Ibrahim, na tukaweka katika dhuriya zao Unabii na Kitabu. Basi wapo miongoni mwao walio ongoka, na wengi katika wao ni wapotovu. 

27. Tena tukafuatisha nyuma yao Mitume wengine, na tukamfuatisha Isa bin Mariamu, na tukampa Injili. Na tukajaalia katika nyoyo za walio mfuata upole na rehema. Na umonaki (utawa wa mapadri) wameuzua wao. Sisi hatukuwaandikia hayo, ila kutafuta radhi za Mwenyezi Mungu. Lakini hawakuufuata inavyo takiwa kuufuata. Basi wale walio amini katika wao tuliwapa ujira wao. Na wengi wao ni wapotovu. 

28. Enyi mlio amini! Mcheni Mwenyezi Mungu, na muaminini Mtume wake, atakupeni sehemu mbili katika rehema yake, na atakujaalieni muwe na nuru ya kwenda nayo. Na atakusameheni. Na Mwenyezi Mungu ni Mwenye kusamehe, Mwenye kurehemu. 

29. Ili watu wa Kitabu wajue kwamba wao hawana uweza wowote juu ya fadhila za Mwenyezi Mungu. Na fadhila zote zimo mikononi mwa Mwenyezi Mungu. Humpa amtakaye. Na Mwenyezi Mungu ndiye Mwenye fadhila kuu.