Part 19

 

21. NA WALISEMA wale wasio taraji kukutana nasi: Mbona sisi hatuteremshiwi Malaika au hatumwoni Mola wetu Mlezi? Kwa yakini hawa wamejiona bora nafsi zao, na wamepanda kichwa vikubwa mno! 

22. Siku watakayo waona Malaika haitakuwa furaha siku hiyo kwa wakosefu. Na watasema: Mungu apishe mbali! 

23. Na tutayaendea yale waliyo yatenda katika vitendo vyao, tuvifanye kama mavumbi yaliyo tawanyika. 

24. Watu wa Peponi siku hiyo watakuwa katika makaazi bora na mahali penye starehe nzuri. 

25. Na siku zitapo funguka mbingu kwa mawingu, na wateremshwe Malaika kwa wingi, 

26. Ufalme wa haki siku hiyo utakuwa wa Arrahman, Mwingi wa Rehema, na itakuwa siku ngumu kwa makafiri. 

27. Na siku ambayo mwenye kudhulumu atajiuma mikono yake, na huku anasema: Laiti ningeli shika njia pamoja na Mtume! 

28. Ee Ole wangu! Laiti nisingeli mfanya fulani kuwa rafiki! 

29. Amenipoteza, nikaacha Ukumbusho, baada ya kwisha nijia, na kweli Shet'ani ni khaini kwa mwanaadamu. 

30. Na Mtume alikuwa akisema: Ee Mola wangu Mlezi! Hakika watu wangu wameifanya hii Qur'ani ni kihame. 

31. Na vivi hivi tumemfanyia kila Nabii adui miongoni mwa wakosefu, na Mola wako Mlezi anatosha kuwa Mwenye kuongoa na Mwenye kunusuru. 

32. Na wakasema walio kufuru: Kwa nini hakuteremshiwa Qur'ani kwa jumla moja? Hayo ni hivyo ili tuuthibitishe moyo wako, na ndio tumeisoma kwa mafungu. 

33. Wala hawatakuletea mfano wowote, ila na Sisi tutakuletea (jawabu) kwa haki, na tafsiri iliyo bora. 

34. Wale ambao watakao kusanywa na kubururwa kifudifudi mpaka kwenye Jahannamu, hao watakuwa na mahali pabaya, ndio wenye kuipotea sana njia. 

35. Na hakika tulimpa Musa Kitabu na tukamweka pamoja naye nduguye, Harun, kuwa waziri. 

36. Tukawaambia: Nendeni kwa watu walio kanusha Ishara zetu. Basi tukawateketeza kabisa. 

37. Na watu wa Nuhu, walipo wakanusha Mitume, tuliwazamisha, na tukawafanya ni Ishara kwa watu. Na tumewaandalia wenye kudhulumu adhabu chungu. 

38. Na tuliwaangamiza kina A'di na Thamudi na watu wa Rass na vizazi vingi vilivyo kuwa kati yao. 

39. Na wote tuliwapigia mifano, na wote tuliwaangamiza kabisa kabisa. 

40. Na kwa yakini wao wanafika kwenye nchi ilio teremshiwa mvua mbaya. Basi, je, hawakuwa wakiiona? Bali walikuwa hawataraji kufufuliwa. 

41. Na wanapo kuona hawakuchukulii ila ni mzaha tu, na (wanasema): Ati ndiye huyu Mwenyezi Mungu aliye mtuma kuwa Mtume? 

42. Kwa hakika alikuwa karibu kutupoteza tuiache miungu yetu, ingeli kuwa hatukushikamana nayo kwa kuvumilia. Bado watakuja jua, watakapo iona adhabu, ni nani aliye potea njia. 

43. Je! Umemwona aliye yafanya matamanio yake kuwa ndio mungu wake? Basi je, wewe utakuwa ni wakili wake? 

44. Au wewe unadhani kwamba wengi wao wanasikia au wanaelewa? Hao hawakuwa ila ni kama nyama hoa tu, bali wao wamepotea zaidi njia. 

45. Je! Huoni jinsi Mola wako Mlezi anavyo kitandaza kivuli. Na angeli taka angeli kifanya kikatulia tu. Kisha tumelifanya jua kuwa ni kiongozi wake. 

46. Kisha tunakivutia kwetu kidogo kidogo. 

47. Naye ndiye aliye kufanyieni usiku kuwa ni vazi, na usingizi kuwa mapumziko, na akakufanyieni mchana ni kufufuka. 

48. Naye ndiye anaye zituma pepo kuwa bishara njema kabla ya rehema yake, na tunayateremsha kutoka mbinguni maji safi. 

49. Ili kwa hayo tuihuishe nchi iliyo kufa, na tuwanyweshe wanyama na watu wengi tulio waumba. 

50. Na kwa yakini tumeisarifu kati yao wapate kukumbuka. Lakini watu wengi wanakataa ila kukufuru. 

51. Na tungeli taka tungeli peleka katika kila mji Mwonyaji. 

52. Basi usiwat'ii makafiri. Na pambana nao kwayo kwa Jihadi kubwa. 

53. Naye ndiye aliye zipeleka bahari mbili, hii tamu mno, na hii ya chumvi chungu. Na akaweka baina yao kinga na kizuizi kizuiacho. 

54. Naye ndiye aliye muumba mwanaadamu kutokana na maji, akamjaalia kuwa na nasaba na ushemeji. Na Mola wako Mlezi ni Muweza. 

55. Na wanayaabudu badala ya Mwenyezi Mungu yasiyo wafaa wala yasiyo wadhuru. Na kafiri daima ni msaidizi wa kumpinga Mola wake Mlezi. 

56. Nasi hatukukutuma ila kuwa ni Mbashiri na Mwonyaji. 

57. Sema: Sikukuombeni ujira juu yake; ila atakaye na ashike njia iendayo kwa Mola wake Mlezi. 

58. Na mtegemee Aliye Hai, ambaye hafi. Na umtukuze kwa sifa zake. Na yatosha kwake kuwa yeye ni Mwenye khabari za dhambi za waja wake. 

59. Ambaye ameziumba mbingu na ardhi, na viliomo ndani yake kwa siku sita. Kisha akatawala juu ya A'rshi, Arrahman, Mwingi wa Rehema! Uliza khabari zake kwa wamjuaye. 

60. Na wanapo ambiwa: Msujudieni Arrahman! Wao husema: Ni nani Arrahman? Je! Tumsujudie unaye tuamrisha wewe tu? Na huwazidishia chuki. 

61. Ametukuka aliye zijaalia nyota mbinguni, na akajaalia humo taa na mwezi unao ng'ara. 

62. Naye ndiye aliye fanya usiku na mchana kufuatana kwa nafuu ya anaye taka kukumbuka, au anaye taka kushukuru. 

63. Na waja wa Arrahman Mwingi wa Rehema ni wale wanao tembea ulimwenguni kwa staha, na wajinga wakiwasemeza hujibu: Salama! 

64. Na wale wanao kesha kwa ajili ya Mola wao Mlezi kwa kusujudu na kusimama. 

65. Na wale wanao sema: Mola wetu Mlezi! Tuondolee adhabu ya Jahannamu. Hakika adhabu yake ikimpata mtu haimwachi. 

66. Hakika hiyo ni kituo na makao mabaya. 

67. Na wale ambao wanapo tumia hawatumii kwa fujo wala hawafanyi ubakhili, bali wanakuwa katikati baina ya hayo. 

68. Na wale wasio mwomba mungu mwengine pamoja na Mwenyezi Mungu, wala hawaui nafsi aliyo iharimisha Mwenyezi Mungu isipo kuwa kwa haki, wala hawazini - na atakaye fanya hayo atapata madhara, 

69. Atazidishiwa adhabu Siku ya Kiyama, na atadumu humo kwa kufedheheka. 

70. Isipo kuwa atakaye tubu, na akaamini, na akatenda vitendo vyema. Basi hao Mwenyezi Mungu atayabadilisha maovu yao yawe mema. Na Mwenyezi Mungu ni Mwenye kusamehe, Mwenye kurehemu. 

71. Na aliye tubu na akafanya mema, basi hakika huyo ametubu kweli kweli kwa Mwenyezi Mungu. 

72. Na wale ambao hawatoi ushahidi wa uwongo, na pindi wapitapo penye upuuzi, hupita kwa hishima yao. 

73. Na wale ambao wanapo kumbushwa Ishara za Mola wao Mlezi hawajifanyi viziwi nazo, na vipofu. 

74. Na wale wanao sema: Mola wetu Mlezi! Tupe katika wake zetu na wenetu yaburudishayo macho, na utujaalie tuwe waongozi kwa wachamngu. 

75. Hao ndio watakao lipwa makao ya juu kwa kuwa walisubiri, na watakuta humo maamkio na salamu. 

76. Wadumu humo - kituo na makao mazuri kabisa. 

77. Sema: Mola wangu Mlezi asinge kujalini lau kuwa si kuomba kwenu. Lakini nyinyi mmemkadhibisha. Basi adhabu lazima iwe. 

 

26 - ASH-SHUA'RAA

KWA JINA LA MWENYEZI MUNGU MWINGI WA REHEMA MWENYE KUREHEMU. 

 

1. T'aa Siin Miim. (T'.S.M.) 

2. Hizi ni Aya za Kitabu kinacho bainisha. 

3. Huenda labda ukajikera nafsi yako kwa kuwa hawawi Waumini. 

4. Tunge penda tungeli wateremshia kutoka mbinguni Ishara zikanyenyekea shingo zao. 

5. Wala hauwafikii ukumbusho mpya kutoka kwa Arrahman ila wao hujitenga nao. 

6. Kwa yakini wamekanusha; kwa hivyo zitakuja wafikia khabari za yale waliyo kuwa wakiyafanyia mzaha. 

7. Je! Hawakuiona ardhi, mimea mingapi tumeiotesha humo, ya kila namna nzuri? 

8. Hakika katika haya zipo Ishara. Lakini wengi wao hawakuwa wenye kuamini. 

9. Na hakika Mola wako Mlezi ndiye Yeye Mwenye nguvu Mwenye kurehemu. 

10. Na Mola wako Mlezi, alipo mwita Musa, akamwambia: Fika kwa watu madhaalimu, 

11. Watu wa Firauni. Hawaogopi? 

12. Akasema: Hakika mimi nachelea wasinikanushe. 

13. Na kifua changu kina dhiki, na ulimi wangu haukunjuki vyema. Basi mtumie ujumbe Harun. 

14. Na wao wana kisasi juu yangu, kwa hivyo naogopa wasije kuniuwa. 

15. Akasema: Siyo hivyo kabisa! Nendeni na miujiza yetu. Hakika Sisi tu pamoja nanyi, tunasikiliza. 

16. Basi mfikieni Firauni na mwambieni: Hakika sisi ni Mitume wa Mola Mlezi wa walimwengu wote. 

17. Waachilie Wana wa Israili wende nasi. 

18. (Firauni) akasema: Sisi hatukukulea wewe utotoni, na ukakaa kwetu katika umri wako miaka mingi? 

19. Na ukatenda kitendo chako ulicho tenda, nawe ukawa miongoni mwa wasio na shukrani? 

20. (Musa) akasema: Nilitenda hayo hapo nilipo kuwa miongoni mwa wale walio potea. 

21. Basi nikakukimbieni nilipo kuogopeni, tena Mola wangu Mlezi akanitunukia hukumu, na akanijaalia niwe miongoni mwa Mitume. 

22. Na hiyo ndiyo neema ya kunisumbulia, na wewe umewatia utumwani Wana wa Israili? 

23. Firauni akasema: Na nani huyo Mola Mlezi wa walimwengu wote? 

24. Akasema: Ndiye Mola Mlezi wa mbingu na ardhi, na viliomo baina yao, ikiwa nyinyi ni wenye yakini. 

25. (Firauni) akawaambia walio mzunguka: Hamsikilizi? 

26. (Musa) akasema: Ndiye Mola wenu Mlezi, na Mola Mlezi wa baba zenu wa kwanza. 

27. (Firauni) akasema: Hakika huyu Mtume wenu aliye tumwa kwenu ni mwendawazimu. 

28. (Musa) akasema: Ndiye Mola Mlezi wa Mashariki na Magharibi na viliomo baina yao, ikiwa nyinyi mnatia akilini. 

29. (Firauni) akasema: Ukimfuata mungu mwengine asiye kuwa mimi, basi bila ya shaka nitakufunga gerezani. 

30. Akasema: Je! Ijapo kuwa nitakuletea kitu cha kubainisha wazi? 

31. Akasema: Kilete basi, kama wewe ni katika wasemao kweli. 

32. Basi akaitupa fimbo yake, mara ikawa nyoka wa kuonekana dhaahiri. 

33. Na akautoa mkono wake, na mara ukawa mweupe kwa watazamao. 

34. (Firauni) akawaambia waheshimiwa walio mzunguka: Hakika huyu ni mchawi mtaalamu. 

35. Anataka kukutoeni katika nchi yenu kwa uchawi wake. Basi mna shauri gani? 

36. Wakasema: Mpe muda yeye na nduguye na uwatume mijini wapigao mbiu ya mgambo. 

37. Wakuletee kila mchawi bingwa mtaalamu. 

38. Basi wakakusanywa wachawi wakati na siku maalumu. 

39. Na watu wakaambiwa: Je! Mtakusanyika? 

40. Huenda tutawafuata wachawi wakiwa wao ndio watakao shinda. 

41. Basi walipo kuja wachawi wakamwambia Firauni: Je! Tutapata ujira tukiwa sisi ndio tulio shinda? 

42. Naam! Na hakika mtakuwa katika watu wa mbele. 

43. Musa akwaambia: Tupeni mnavyo taka kutupa. 

44. Basi wakatupa kamba zao na fimbo zao, na wakasema: Kwa nguvu za Firauni hakika sisi hapana shaka ni wenye kushinda. 

45. Musa tena akatupa fimbo yake, nayo mara ikavimeza walivyo vizua. 

46. Hapo wachawi walipinduka wakasujudu. 

47. Wakasema: Tunamuamini Mola Mlezi wa walimwengu wote. 

48. Mola Mlezi wa Musa na Harun. 

49. (Firauni) akasema: Je! Mmemuamini kabla sijakuruhusuni? Bila ya shaka yeye basi ndiye mkubwa wenu aliye kufunzeni uchawi. Basi mtakuja jua! Nitakata mikono yenu na miguu yenu kwa kutafautisha. Na nitakubandikeni misalabani nyote. 

50. Wakasema: Haidhuru, kwani sisi ni wenye kurejea kwa Mola wetu Mlezi. 

51. Hakika sisi tunatumai Mola wetu Mlezi atatusamehe makosa yetu, kwa kuwa ndio wa kwanza wa kuamini. 

52. Na tulimuamrisha Musa kwa wahyi: Nenda na waja wangu wakati wa usiku. Kwa hakika mtafuatwa. 

53. Basi Firauni akawatuma mijini wapiga mbiu za mgambo. 

54. (Wakieneza): Hakika hawa ni kikundi kidogo. 

55. Nao wanatuudhi. 

56. Na sisi ni wengi, wenye kuchukua hadhari. 

57. Basi tukawatoa katika mabustani na chemchem, 

58. Na makhazina, na vyeo vya hishima, 

59. Kadhaalika; na tukawarithisha hayo Wana wa Israili. 

60. Basi wakawafuata lilipo chomoza jua. 

61. Na yalipo onana majeshi mawili haya, watuwa Musa wakasema: Hakika sisi bila ya shaka tumepatikana! 

62. (Musa) akasema: Hasha! Hakika yu pamoja nami Mola wangu Mlezi. Yeye ataniongoa! 

63. Tulimletea wahyi Musa tukamwambia: Piga bahari kwa fimbo yako. Basi ikatengana, na kila sehemu ikawa kama mlima mkubwa. 

64. Na tukawajongeza hapo wale wengine. 

65. Tukawaokoa Musa na walio kuwa pamoja naye wote. 

66. Kisha tukawazamisha hao wengine. 

67. Hakika bila ya shaka katika hayo ipo Ishara; lakini wengi wao si katika wenye kuamini. 

68. Na kwa hakika Mola wako Mlezi ndiye Mwenye nguvu Mwenye kurehemu. 

69. Na wasomee khabari za Ibrahim. 

70. Alipo mwambia baba yake na kaumu yake: Mnaabudu nini? 

71. Wakasema: Tunaabudu masanamu, daima tunayanyenyekea. 

72. Akasema: Je! Yanakusikieni mnapo yaita? 

73. Au yanakufaeni, au yanakudhuruni? 

74. Wakasema: Bali tumewakuta baba zetu wakifanya hivyo hivyo. 

75. Je! Mmewaona hawa mnao waabudu- 

76. Nyinyi na baba zenu wa zamani? 

77. Kwani hakika hao ni adui zangu, isipo kuwa Mola Mlezi wa walimwengu wote. 

78. Ambaye ndiye aliye niumba, na Yeye ndiye ananiongoa, 

79. Na ambaye ndiye ananilisha na kuninywesha. 

80. Na ninapo ugua ni Yeye ndiye anaye niponesha. 

81. Na ambaye atanifisha, na kisha atanihuisha. 

82. Na ambaye ndiye ninaye mtumai kunisamehe makosa yangu Siku ya Malipo. 

83. 83, Mola wangu Mlezi! Nitunukie hukumu na uniunganishe na watendao mema. 

84. Na unijaalie nitajwe kwa wema na watu watakao kuja baadaye. 

85. Na unijaalie katika warithi wa Bustani za neema. 

86. Na umsamehe baba yangu, kwani hakika alikuwa miongoni mwa wapotovu. 

87. Wala usinihizi Siku watapo fufuliwa. 

88. Siku ambayo kwamba mali hayato faa kitu wala wana. 

89. Isipo kuwa mwenye kumjia Mwenyezi Mungu na moyo safi. 

90. Na Pepo itasogezwa kwa wachamngu. 

91. Na Jahannamu itadhihirishwa kwa wapotovu. 

92. Na wataambiwa: Wako wapi mlio kuwa mkiwaabudu 

93. Badala ya Mwenyezi Mungu? Je! Wanakusaidieni, au wanajisaidia wenyewe? 

94. Basi watavurumizwa humo wao na hao wakosefu, 

95. Na majeshi ya Ibilisi yote. 

96. Watasema, na hali ya kuwa wanazozana humo: 

97. Wallahi! Kwa yakini tulikuwa katika upotovu ulio dhaahiri, 

98. Tulipo kufanyeni ni sawa na Mola Mlezi wa walimwengu wote. 

99. Na hawakutupoteza ila wale wakosefu. 

100. Basi hatuna waombezi. 

101. Wala rafiki wa dhati. 

102. Laiti tungeli pata kurejea tena tungeli kuwa katika Waumini. 

103. Hakika katika haya ipo Ishara, lakini wengi wao hawakuwa wenye kuamini. 

104. Na hakika Mola wako Mlezi ndiye Mwenye nguvu Mwenye kurehemu. 

105. Kaumu ya Nuhu waliwakadhibisha Mitume. 

106. Alipo waambia ndugu yao, Nuhu: Je! Hamchimngu? 

107. Hakika mimi kwenu ni Mtume muaminifu. 

108. Basi Mcheni Mwenyezi Mungu, na nit'iini mimi. 

109. Na sikutakini juu yake ujira, kwani ujira wangu hauko ila kwa Mola Mlezi wa walimwengu wote. 

110. Basi Mcheni Mwenyezi Mungu, na nit'iini mimi. 

111. Wakasema: Je! Tukuamini wewe, hali wanao kufuata ni watu wa chini? 

112. Akasema: Nayajuaje waliyo kuwa wakiyafanya? 

113. Hisabu yao haiko ila kwa Mola wao Mlezi, laiti mngeli tambua! 

114. Wala mimi si wa kuwafukuza Waumini. 

115. Mimi si cho chote ila ni Mwonyaji wa dhaahiri shaahiri. 

116. Wakasema: Ikiwa huachi, ewe Nuhu, bila ya shaka utapigwa mawe. 

117. Akasema: Mola wangu Mlezi! Hakika watu wangu wamenikanusha. 

118. Basi hukumu baina yangu na wao kwa hukumu yako, na uniokoe mimi na walio pamoja nami, Waumini. 

119. Kwa hivyo tukamwokoa yeye na walio kuwa pamoja naye katika marikebu iliyo sheheni. 

120. Kisha tukawazamisha baadaye walio bakia. 

121. Hakika katika haya ipo Ishara, lakini si wengi wao walio kuwa Waumini. 

122. Na hakika Mola wako Mlezi ndiye Yeye Mwenye nguvu Mwenye kurehemu. 

123. Kina A'd waliwakanusha Mitume. 

124. Alipo waambia ndugu yao, Hud: Je! Hamchimngu? 

125. Hakika mimi kwenu ni Mtume muaminifu. 

126. Basi mcheni Mwenyezi Mungu, na nit'iini mimi. 

127. Wala sikutakeni juu yake ujira, kwani ujira wangu hauko ila kwa Mola Mlezi wa walimwengu wote. 

128. Je! Mnajenga juu ya kila mnyanyuko kumbusho la kufanyia upuuzi? 

129. Na mnajenga majengo ya fakhari kama kwamba mtaishi milele! 

130. Na mnapo tumia nguvu mnatumia nguvu kwa ujabari. 

131. Basi mcheni Mwenyezi Mungu, na nit'iini. 

132. Na mcheni aliye kupeni haya mnayo yajua. 

133. Amekupeni wanyama wa kufuga na wana. 

134. Na mabustani na chemchem. 

135. Hakika mimi ninakukhofieni adhabu ya Siku Kubwa. 

136. Wakasema: Ni mamoja kwetu, ukitupa mawaidha au hukuwa miongoni mwa watoao mawaidha. 

137. Haya si chochote ila ni mtindo wa watu wa tokea zamani. 

138. Wala sisi hatutaadhibiwa. 

139. Wakamkanusha; nasi tukawaangamiza. Hakika bila ya shaka katika haya ipo Ishara. Lakini hawakuwa wengi wao wenye kuamini. 

140. Na hakika Mola wako Mlezi ndiye Mwenye nguvu Mwenye kurehemu. 

141. Kina Thamud waliwakanusha Mitume. 

142. Alipo waambia ndugu yao Saleh: Je! Hamumchimngu? 

143. Hakika mimi kwenu ni Mtume muaminifu. 

144. Basi mcheni Mwenyezi Mungu, na nit'iini. 

145. Wala sikutakini ujira juu yake. Ujira wangu hauko ila kwa Mola Mlezi wa walimwengu wote. 

146. Je! Mtaachwa salama usalimina katika haya yaliyopo hapa? 

147. Katika mabustani, na chemchem? 

148. Na konde na mitende yenye makole yaliyo wiva. 

149. Na mnachonga milimani majumba kwa ustadi. 

150. Basi mcheni Mwenyezi Mungu, na nit'iini mimi. 

151. 151, Wala msit'ii amri za walio pindukia mipaka, 

152. Ambao wanafanya ufisadi katika nchi, wala hawatengenezi. 

153. Wakasema: Hakika wewe ni miongoni mwa walio rogwa. 

154. Wewe si chochote ila ni mtu kama sisi. Basi lete Ishara ukiwa wewe ni miongoni mwa wasemao kweli. 

155. Akasema: Huyu ngamia jike; awe na zamu yake ya kunywa, na nyinyi muwe na zamu yenu ya kunywa katika siku maalumu. 

156. Wala msimguse kwa uwovu, isije ikakushikeni adhabu ya Siku Kubwa. 

157. Lakini wakamuuwa, na wakawa wenye kujuta. 

158. Basi ikawapata adhabu. Hakika katika hayo ipo Ishara. Lakini hawakuwa wengi wao wenye kuamini. 

159. Na hakika Mola wako Mlezi ndiye Mwenye nguvu Mwenye kurehemu. 

160. Watu wa Lut'i waliwakanusha Mitume. 

161. Alipo waambia ndugu yao, Lut'i: Je! Hamumchimngu? 

162. Hakika mimi kwenu ni Mtume muaminifu kwenu. 

163. Basi mcheni Mwenyezi Mungu na nit'iini mimi. 

164. Wala mimi sikutakini ujira juu yake; ujira wangu hauko ila kwa Mola Mlezi wa walimwengu wote. 

165. Je! Katika viumbe vyote mnawaingilia wanaume? 

166. Na mnaacha alicho kuumbieni Mola wenu Mlezi katika wake zenu? Ama kweli nyinyi ni watu mnao ruka mipaka! 

167. Wakasema: Ewe Lut'i! Usipo acha, hapana shaka utakuwa miongoni mwa wanao tolewa mji! 

168. Akasema: Hakika mimi ni katika wanao kichukia hichi kitendo chenu. 

169. Mola wangu Mlezi! Niokoe mimi na ahali zangu na haya wayatendayo. 

170. Basi tukamwokoa yeye na ahali zake wote, 

171. Isipo kuwa kikongwe katika walio kaa nyuma. 

172. Kisha tukawaangamiza wale wengine. 

173. Na tukawanyeshea mvua, basi ni ovu mno mvua ya waliyo onywa. 

174. Hakika katika hayo ipo Ishara. Na hawakuwa wengi wao wenye kuamini. 

175. Na hakika Mola wako Mlezi bila ya shaka ndiye Mwenye nguvu, Mwenye kurehemu. 

176. Watu wa Machakani waliwakanusha Mitume. 

177. Shuaibu alipo waambia: Je! Hamfanyi mkamchamngu? 

178. Hakika mimi kwenu ni Mtume muaminifu. 

179. Basi mcheni Mwenyezi Mungu, na nit'iini mimi. 

180. Wala sikutakini ujira juu yake. Ujira wangu hauko ila kwa Mola Mlezi wa walimwengu wote. 

181. Timizeni kipimo sawa sawa, wala msiwe katika wanao punja. 

182. Na pimeni kwa haki iliyo nyooka; 

183. Wala msiwapunje watu vitu vyao, wala msifanye jeuri kwa ufisadi. 

184. Na mcheni aliye kuumbeni nyinyi na vizazi vilivyo tangulia. 

185. Wakasema: Hakika wewe ni katika walio rogwa. 

186. Na wewe si chochote ila ni mtu tu kama sisi, na kwa yakini tunakuona wewe ni katika waongo. 

187. Hebu tuangushie vipande kutoka mbinguni ikiwa wewe ni miongoni mwa wasemao kweli. 

188. Akasema: Mola wangu Mlezi anajua zaidi mnayo yatenda. 

189. Basi walimkanusha, na ikawashika adhabu ya siku ya kivuli. Hakika hiyo ilikuwa adhabu ya siku kubwa. 

190. Hakika katika hayo ipo Ishara, lakini hawakuwa wengi wao wenye kuamini. 

191. Na hakika Mola wako Mlezi bila ya shaka ndiye Yeye Mwenye nguvu Mwenye kurehemu. 

192. Na bila ya shaka hii ni Uteremsho wa Mola Mlezi wa walimwengu wote. 

193. Ameuteremsha Roho muaminifu, 

194. Juu ya moyo wako, ili uwe katika Waonyaji, 

195. Kwa ulimi wa Kiarabu ulio wazi. 

196. Na hakika bila ya shaka haya yamo katika Vitabu vya kale. 

197. Je! Haikuwa kwao ni Ishara kwamba wanayajua haya wanazuoni wa Wana wa Israili? 

198. Na lau kuwa tungeli iteremsha juu ya mmoja wa wasio kuwa Waarabu, 

199. Na akawasomea, wasingeli kuwa wenye kuamini. 

200. Namna hivi tunaingiza katika nyoyo za wakosefu. 

201. Hawataiamini mpaka waione adhabu chungu. 

202. Basi itawafikia kwa ghafla, na hali hawana khabari. 

203. Na watasema: Je, tutapewa muhula? 

204. Basi, je, wanaihimiza adhabu yetu? 

205. Waonaje kama tukiwastarehesha kwa miaka, 

206. Kisha yakawafikia waliyo kuwa wakiahidiwa, 

207. Yatawafaa nini yale waliyo stareheshewa? 

208. Wala hatukuangamiza mji wo wote ila ulikuwa na waonyaji - 

209. Kuwa ni ukumbusho. Wala Sisi hatukuwa wenye kudhulumu. 

210. Wala Mashet'ani hawakuteremka nayo, 

211. Wala haitakiwi kwao, na wala hawawezi. 

212. Hakika hao wametengwa na kusikia. 

213. Basi usimwombe mungu mwingine pamoja na Mwenyezi Mungu ukawa miongoni mwa watakao adhibiwa. 

214. Na uwaonye jamaa zako walio karibu nawe. 

215. Na watwae kwa upole wanao kufuata miongoni mwa Waumini. 

216. Na ikiwa watakuasi basi sema: Mimi najitenga mbali na hayo mnayo yatenda. 

217. Na umtegemee Mtukufu Mwenye nguvu Mwenye kurehemu. 

218. Ambaye anakuona unapo simama, 

219. Na mageuko yako kati ya wanao sujudu. 

220. Hakika Yeye ndiye Mwenye kusikia Mwenye kujua. 

221. Je! Nikwambieni nani wanawashukia Mashet'ani? 

222. Wanamshukia kila mzushi mkubwa mwingi wa dhambi. 

223. Wanawapelekea yale wanayo yasikia; na wengi wao ni waongo. 

224. Na watungaji mashairi ni wapotofu ndio wanawafuata. 

225. Je! Huwaoni kwamba wao wanatangatanga katika kila bonde? 

226. Na kwamba wao husema wasiyo yatenda? 

227. Isipo kuwa wale walio amini, na wakatenda mema, na wakamkumbuka Mwenyezi Mungu kwa wingi, na wakajitetea wanapo dhulumiwa. Na wanao dhulumu watakuja jua mgeuko gani watakao geuka. 

 

27 - AN-NAML

KWA JINA LA MWENYEZI MUNGU MWINGI WA REHEMA MWENYE KUREHEMU. 

 

1. T'aa Siin. (T'.S.), Hizi ni Aya za Qur'ani na Kitabu kinacho bainisha; 

2. Uwongofu na bishara kwa Waumini, 

3. Ambao wanashika Sala, na wanatoa Zaka, na Akhera wana yakini nayo. 

4. Kwa hakika wale wasio iamini Akhera tumewapambia vitendo vyao, kwa hivyo wanatangatanga ovyo. 

5. Hao ndio watapata adhabu mbaya kabisa, na hao katika Akhera ndio watapata khasara zaidi. 

6. Na hakika wewe unafundishwa Qur'ani inayo tokana kwake Mwenye hikima Mwenye kujua. 

7. (Kumbuka) Musa alipo waambia ahali zake: Hakika nimeona moto, nitakwenda nikuleteeni khabari, au nitakuleteeni kijinga kinacho waka ili mpate kuota moto. 

8. Basi alipo fika ilinadiwa: Amebarikiwa aliomo katika moto huu na walioko pembezoni mwake. Na ametakasika Mwenyezi Mungu, Mola Mlezi wa walimwengu wote. 

9. Ewe Musa! Hakika Mimi ndiye Mwenyezi Mungu, Mwenye nguvu, Mwenye hikima. 

10. Na itupe fimbo yako! Alipo iona ikitikisika kama nyoka, aligeuka nyuma wala hakungoja. Ewe Musa! Usikhofu! Hakika hawakhofu mbele yangu Mitume. 

11. Lakini aliye dhulumu, kisha akabadilisha wema baada ya ubaya, basi Mimi ni Mwenye kusamehe Mwenye kurehemu. 

12. Na ingiza mkono wako katika mfuko wako, utatoka mweupe bila ya maradhi. Ni katika Ishara tisa za kumpelekea Firauni na kaumu yake. Hakika hao walikuwa watu waovu. 

13. Basi zilipo wafikia Ishara zetu hizo zenye kuonyesha, wakasema: Huu ni uchawi dhaahiri. 

14. Na wakazikataa kwa dhulma na kujivuna, na hali ya kuwa nafsi zao zina yakini nazo. Basi angalia ulikuwaje mwisho wa mafisadi! 

15. Na hakika tuliwapa Daudi na Sulaiman ilimu, na wakasema: Alhamdu Lillahi, Kuhimidiwa kote ni kwa Mwenyezi Mungu aliye tufadhilisha kuliko wengi katika waja wake Waumini. 

16. Na Sulaiman alimrithi Daudi, na akasema: Enyi watu! Tumefunzwa usemi wa ndege, na tumepewa kila kitu. Hakika hii ni fadhila iliyo dhaahiri. 

17. Na alikusanyiwa Sulaiman majeshi yake ya majini, na watu, na ndege; nayo yakapangwa kwa nidhamu. 

18. Mpaka walipo fika kwenye bonde la wadudu chungu, alisema mdudu chungu mmoja: Enyi wadudu chungu! Ingieni majumbani mwenu, asikupondeni Sulaiman na majeshi yake bila ya wao kutambua. 

19. Basi (Sulaiman) akatabasamu akacheka kwa neno hili, na akasema: Ee Mola wangu Mlezi! Nizindue niishukuru neema yako uliyo nineemesha mimi na wazazi wangu, na nipate kutenda mema uyapendayo, na uniingize kwa rehema yako katika waja wako wema. 

20. Na akawakagua ndege, na akasema: Imekuwaje, mbona simwoni Hud-hud, au amekuwa miongoni mwa walio ghibu? 

21. Kwa yakini nitamuadhibu kwa adhabu kali, au nitamchinja, au aniletee hoja ya kutosha. 

22. Basi (Hud-hud) akakaa si mbali na akasema: Nimegundua usilo gundua wewe, na ninakujia hivi kutoka nchi ya Sabai, na nakuletea khabari za yakini. 

23. Hakika mimi nimemkuta mwanamke anawatawala, naye amepewa kila kitu, na anacho kiti cha enzi kikubwa. 

24. Nimemkuta yeye na watu wake wanalisujudia jua badala ya Mwenyezi Mungu; na Shet'ani amewapambia vitendo vyao na akawazuilia Njia. Kwa hivyo hawakuongoka, 

25. Na hawamsujudii Mwenyezi Mungu ambaye huyatoa yaliyo fichikana katika mbingu na ardhi, na anayajua mnayo yaficha na mnayo yatangaza. 

26. Mwenyezi Mungu - hapana mungu ila Yeye, Mola Mlezi wa A'rshi tukufu.. 

27. Akasema (Sulaiman): Tutatazama umesema kweli au wewe ni miongoni mwa waongo. 

28. Nenda na barua yangu hii na uwafikishie, kisha waache na utazame watarejesha nini. 

29. (Malkia) akasema: Enyi wahishimiwa! Hakika nimeletewa barua tukufu. 

30. Imetoka kwa Sulaiman nayo ni: Kwa jina la Mwenyezi Mungu, Mwingi wa rehema, Mwenye kurehemu. 

31. Msinifanyie jeuri, na fikeni kwangu nanyi mmekwisha kuwa wenye kusalimu amri. 

32. Akasema: Enyi wahishimiwa! Nipeni shauri katika jambo langu hili, kwani mimi sikati shauri yoyote mpaka mhudhurie. 

33. Wakasema: Sisi ni wenye nguvu na wakali kwa vita; na amri iko kwako, basi tazama ni nini unaamrisha. 

34. Akasema: Hakika wafalme wanapo uingia mji wanauharibu, na wanawafanya wale watukufu wake kuwa wanyonge. Na hivyo ndivyo watendavyo. 

35. Lakini mimi nitawapelekea zawadi, nami nitangoja watakayo rudi nayo wajumbe. 

36. Basi alipo fika (mjumbe) kwa Sulaiman, alisema (Sulaiman): Hivyo ndio nyinyi mnanisaidia kwa mali? Aliyo nipa Mwenyezi Mungu ni bora zaidi kuliko aliyo kupeni nyinyi. Lakini nyinyi mnafurahia hii zawadi yenu. 

37. Rejea kwao! Kwa yakini sisi tutawajia kwa majeshi wasio yaweza kuyakabili. Na hakika tutawatoa humo na hali wao wamekuwa madhalili na wanyonge. 

38. Akasema: Enyi wahishimiwa! Ni nani kati yenu atakaye niletea kiti chake cha enzi kabla hawajanijia nao wamekwisha salimu amri. 

39. Akasema: Afriti, katika majini: Mimi nitakuletea kabla hujainuka pahala pako hapo. Na mimi kwa hakika nina nguvu na muaminifu. 

40. Akasema mwenye ilimu ya Kitabu: Mimi nitakuletea kabla ya kupepesa jicho lako. Basi alipo kiona kimewekwa mbele yake, akasema: Haya ni katika fadhila zake Mola wangu Mlezi, ili anijaribu nitashukuru au nitakufuru. Na mwenye kushukuru, kwa hakika, anashukuru kwa manufaa ya nafsi yake; na anaye kufuru, kwa hakika Mola wangu Mlezi ni Mkwasi na Karimu. 

41. Akasema: Mgeuzieni kiti chake cha enzi hiki, tuone ataongoka, au atakuwa miongoni mwa wasio ongoka. 

42. Basi (Malkia) alipo fika akaambiwa: Je! Kiti chako cha enzi ni kama hiki? Akasema: Kama kwamba ndicho hichi. (Sulaiman na watu wake wakasema): Na sisi tumepewa ilimu kabla yake (Malkia), na tukawa Waislamu. 

43. Na yale aliyo kuwa akiyaabudu badala ya Mwenyezi Mungu yalimzuilia. Hakika yeye (Malkia) alikuwa katika kaumu ya makafiri. 

44. Akaambiwa: Liingie behewa la hili jumba. Alipo liona alidhani ni maji, na akapandisha nguo mpaka kwenye miundi yake. (Sulaiman) akasema: Hakika hilo ni behewa lilio sakafiwa kwa viyoo! Akasema (Malkia): Mola wangu Mlezi! Mimi nimejidhulumu nafsi yangu, na sasa nanyenyekea pamoja na Sulaiman kwa Mwenyezi Mungu, Mola Mlezi wa walimwengu wote. 

45. Na kwa kina Thamud tulimtuma ndugu yao Saleh kuwaambia: Muabuduni Mwenyezi Mungu. Basi wakawa makundi mawili yanayo gombana. 

46. Akasema: Enyi watu wangu! Kwa nini mnauhimiza uwovu kabla ya wema? Kwa nini hamuombi msamaha kwa Mwenyezi Mungu ili mrehemewe? 

47. Wakasema: Tuna kisirani nawe na wale walio pamoja nawe. Yeye akasema: Uaguzi wa ukorofi wenu uko kwa Mwenyezi Mungu; lakini nyinyi ni watu mnao jaribiwa. 

48. Na walikuwamo mjini watu tisa wakifanya ufisadi katika nchi wala hawafanyi la maslaha. 

49. Wakasema: Apishaneni kwa Mwenyezi Mungu tutamshambulia usiku yeye na ahali zake; kisha tutamwambia mrithi wake: Sisi hatukuona maangamizo ya watu wake, na sisi bila ya shaka tunasema kweli. 

50. Basi wakapanga mipango yao, na Sisi tukapanga mipango yetu, na wao hawatambui. 

51. Basi angalia ulivyo kuwa mwisho wa mipango yao, ya kwamba tuliwaangamiza wao pamoja na watu wao wote. 

52. Basi hizo nyumba zao ni tupu kwa sababu ya walivyo dhulumu. Hakika bila ya shaka katika hayo ipo Ishara kwa watu wanao jua. 

53. Na tukawaokoa wale walio amini na walio kuwa wanamchamngu. 

54. Na Lut'i alipo waambia watu wake: Je! Mnafanya uchafu nanyi mnaona? 

55. Hivyo nyinyi mnawaingilia wanaume kwa matamanio badala ya wanawake? Hakika nyinyi ni watu mnao fanya ujinga kabisa!